Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninaweza Kukabilianaje na Mahangaiko?

Ninaweza Kukabilianaje na Mahangaiko?

 Ni nini hukufanya upate mahangaiko?

 Je, maelezo yafuatayo yanafunua jinsi wewe unavyohisi nyakati fulani?

 “Ninajiuliza hivi kila wakati: ‘Itakuwaje ikiwa . . . ?’ ‘Itakuwaje ikiwa tutapata aksidenti ya gari?’ ‘Itakuwaje ikiwa ndege tuliyopanda itaanguka?’ Mimi huhangaika kuhusu mambo ambayo kwa kawaida hayamhangaishi mtu.”​—Charles.

 “Mimi huhangaika kila wakati, ni kama buku anayekimbia kwenye tairi linalozunguka mahali pamoja. Ninafanya kazi nyingi na yenye kuchosha lakini sitimizi chochote!”​—Anna.

 “Watu wanaponiambia nifurahi kwamba bado nipo shuleni, ninajiambia, ‘Hawajui tu jinsi shule ilivyo na mikazo mingi!’”​—Daniel.

 “Mimi ni kama sufuria iliyo jikoni ikiwa imefunikwa kabisa. Kila wakati ninahangaika kuhusu jambo litakalofuata au jambo nitakalofanya baadaye.”​—Laura.

 Ukweli wa mambo: Tunaishi katika kipindi ambacho Biblia huita “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Timotheo 3:1) Hivyo, mahangaiko yanaweza kuwaathiri vijana kama tu yanavyowaathiri watu wazima.

 Je, kuhangaika ni vibaya nyakati zote?

 Jibu ni la. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba ni sawa kuhangaika ili kuwafurahisha watu tunaowapenda.​—1 Wakorintho 7:​32-34; 2 Wakorintho 11:28.

 Pia, ukweli wa mambo ni kwamba mahangaiko yanaweza kutusukuma kufanya mengi zaidi. Kwa mfano, labda utafanya mtihani juma lijalo. Mahangaiko yatakuchochea ujitayarishie mtihani huo juma hili​—na huenda hilo litakusaidia kupita mtihani!

 Pia, kiasi fulani cha mahangaiko kinaweza kukuonya ikiwa unakabili hatari. Tineja anayeitwa Serena anasema hivi: “Unaweza kuwa na mahangaiko kwa sababu unafanya jambo lisilofaa na unahitaji kufanya marekebisho ili dhamiri yako itulie.​—Linganisha Yakobo 5:14.

 Ukweli wa mambo: Mahangaiko yanaweza kukusaidia​—maadamu yanakuongoza kufanya jambo linalofaa.

 Lakini vipi ikiwa mahangaiko yanafanya akili yako ijae maoni yasiyo sahihi?

Mahangaiko yanaweza kukufanya uhisi kana kwamba umepotea ndani ya vijia vinavyojipindapinda bila mahali pa kutokea, lakini mtu aliye na mtazamo tofauti anaweza kukusaidia kupata njia ya kutokea

 Mfano: Richard, mwenye umri wa miaka 19 anasema hivi: “Akili yangu hufanya kazi kupita kiasi ninapofikiria matokeo mbalimbali ya hali fulani inayonihangaisha. Mimi hufikiria hali hiyo tena na tena mpaka ninaingiwa na wasiwasi kabisa.”

 Biblia inasema kwamba “moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama.” (Methali 14:30) Kwa upande mwingine, mahangaiko yanaweza kutokeza dalili mbaya mwilini kutia ndani maumivu ya kichwa, kizunguzungu, kusokotwa na tumbo, na moyo kupiga haraka isivyo kawaida.

 Unaweza kufanya nini ikiwa mahangaiko yanakuumiza badala ya kukusaidia?

 Unachoweza kufanya

  •   Chunguza sababu ya mahangaiko yako. “Kufikiria kwa uzito kuhusu wajibu wako ni jambo moja; kuhangaika kupita kiasi kuhusu wajibu huo ni jambo tofauti. Hilo hunikumbusha kuhusu usemi unaosema, Mahangaiko ni kama kiti cha kubembea. Unatumia nguvu, lakini hauendi popote.”​—Katherine.

     Biblia inasema hivi: “Ni nani kati yenu kwa kuhangaika anaweza kuongeza kipimo cha mkono mmoja kwenye uhai wake?”​—Mathayo 6:27.

     Maana yake: Ikiwa mahangaiko hayakusaidii kupata suluhisho, yatakuongezea matatizo​—au yawe ndilo tatizo.

  •   Usihangaikie matatizo ya kesho. “Fikiria kwa makini. Je, jambo linalokuhangaisha leo, litakuhangaisha kesho? mwezi ujao? mwaka ujao? miaka mitano ijayo?”​—Anthony.

     Biblia inasema hivi: “Msihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.”​—Mathayo 6:34.”

     Maana yake: Haipatani na akili kujaribu kutatua matatizo ya kesho​—ambayo huenda yasitokee.

  •   Jifunze kuishi na hali ambazo huwezi kubadili. “Unaweza kujitayarisha kwa ajili ya hali fulani kwa kadiri fulani tu, lakini kubali kwamba hali nyingine haziwezi kubadilika.”​—Robert.

     Biblia inasema hivi: “Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio, . . . wala wenye ujuzi wanaopata kibali; kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.”​—Mhubiri 9:11.

     Maana yake: Nyakati nyingine huwezi kubadili hali fulani, lakini unaweza kubadili maoni yako kuielekea.

  •   Uwe na mtazamo uliosawazika kuelekea hali yako. “Mimi hujitahidi kushughulikia jambo kuu wala si kuhangaikia mambo madogo madogo kulihusu. Ninatanguliza mambo ya maana na hivyo kutumia nguvu zangu kusuluhisha matatizo ya lazima.”​—Alexis.

     Biblia inasema hivi: “Mhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.”​—Wafilipi 1:​10.

     Maana yake: Watu wanaoona mahangaiko yao kwa njia yenye usawaziko, hawatalemewa nayo.

  •   Zungumza na mtu. “Nilipokuwa darasa la sita, ningerudi nyumbani kutoka shuleni nikiwa na mahangaiko mengi, nikiogopa mambo yatakayotukia siku itakayofuata. Mama na baba wangenisikiliza tu nilipojieleza. Hilo lilinisaidia. Niliwatumaini na kuzungumza nao kwa uhuru. Kufanya hivyo kulinitayarisha kwa ajili ya mambo ambayo ningekabili siku iliyofuata.”​—Marilyn.

     Biblia inasema hivi: “Hangaiko katika moyo wa mtu huufanya uiname, lakini neno jema huufanya ushangilie.”​—Methali 12:25.

     Maana yake: Mzazi au rafiki anaweza kukupa madokezo unayoweza kutumia ili kupunguza mahangaiko yako.

  •   Sali. “Kusali, hasa kwa sauti hunisaidia. Hilo hunifanya niseme mambo yanayonifanya nihangaike badala ya kuyawaza akilini tu. Hunisaidia pia kutambua kwamba Yehova ni mkuu kuliko mahangaiko yangu.”​—Laura.

     Biblia inasema hivi: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali nyinyi.’​—1 Petro 5:7.

     Maana yake: Sala si jambo la kupumbaza akili. Ni mawasiliano halisi pamoja na Yehova Mungu, anayeahidi hivi: “Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli.”​—Isaya 41:10.