Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kuvuta Sigara na Kutumia Sigara za Kielektroni?

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kuvuta Sigara na Kutumia Sigara za Kielektroni?

 “Ni vigumu kukutana na mtu katika eneo letu ambaye ana umri wa chini ya miaka 25 ambaye hajawahi kuvuta sigara au kutumia sigara za kielektroni.”​—Julia.

Katika makala hii

 Unachopaswa kujua

  •   Sigara ni hatari. Nikotini—sehemu kuu katika tumbaku—ni sumu ambayo ina nguvu nyingi sana za kumfanya mtu kuwa mraibu sugu. Kulingana na Vituo vya Kudhibiti Magonjwa ya Kuambukiza vya Marekani, “matumizi ya tumbaku ni kisababishi kimoja kikuu cha vifo vinavyoweza kuzuiwa na pia cha magonjwa ulimwenguni pote.”

     “Ninafanya kazi ya kuchunguza picha za “ultrasound,” na nimejionea picha zinazoonyesha jinsi kuvuta sigara kunavyoathiri sana mwili wa mtu. Inashtua sana kuona kiasi cha ukoga ndani ya mishipa ya watu waliokuwa wakivuta sigara hapo awali. Ninaheshimu mwili wangu sana hivi kwamba siwezi kujaribu kuvuta sigara.”​—Theresa.

     Je wajua? Sigara zina kemikali 7,000 hivi, na nyingi kati ya hizo zina sumu. Kila mwaka, mamilioni ya watu hufa kutokana na magonjwa yanayosababishwa na tumbaku.

  •   Watu wanaovuta sigara za kielektroni wanaingiza kemikali zenye sumu mwilini. Wataalamu wanasema watu wanaotumia sigara za kielektroni au kalamu za sigara, wamepata madhara makubwa katika mapafu yao na wengine wamekufa. Pia, kama tu sigara za kawaida, sigara za kielektroni zina nikotini. Kwa sababu nikotini inawafanya watu wawe waraibu sugu, jarida moja kuhusu sigara za kielektroni linasema zinaweza “kuwaongoza vijana wawe waraibu wa dawa nyingine za kulevya.”

     “Sigara za kielektroni zilizo na majina kama vile “cotton candy” na “cherry bomb” zina ladha tamu, nazo zimekusudiwa hasa kuwavutia watoto na matineja. Ladha yake huwafanya wapuuze hatari.”​—Miranda.

     Je wajua? Mvuke unaotokezwa na sigara za kielektroni si maji tu. Una kemikali zenye sumu kutia ndani madini hatari, ambayo huingia katika mapafu yako.

 Hatari zinazohusianishwa na kuvuta sigara na kutumia sigara za kielektroni

  1.  (1) Kupungua kwa uwezo wa akili kutia ndani matatizo ya kukaza fikira na ya kihisia, hasa kwa ubongo unaoendelea kukua

  2.  (2) Kuvimba kwa fizi na mashimo katika meno

  3.  (3) Kuvimba vibaya sana kwa mapafu na ugonjwa wa moyo

     Pumu mbaya

     Matatizo ya tumbo na kichefuchefu

 Unachoweza kufanya

  •   Jifunze habari kamili. Usikubali kila kitu unachosikia, kwa mfano, watu fulani husema hakuna madhara yoyote ya kutumia sigara za kielektroni au kwamba kufanya hivyo ni njia nzuri ya kupunguza mkazo. Fanya utafiti, na ujifanyie uamuzi unaofaa.

     Kanuni ya Biblia: “Mjinga huamini kila neno, lakini mwerevu hutafakari kila hatua.”​—Methali 14:15.

     “Unapofikiria kuhusu madhara ya kuvuta sigara na sigara za kielektroni, unatambua kwamba mengi zaidi yanahusika kuliko burudani ambayo watu mashuhuri na vijana wenzako wanaonekana kuwa wanafurahia.”​—Evan.

     Jambo la kufikiria: Je, kweli vijana wanaovuta sigara au kutumia sigara za kielektroni wana furaha zaidi? Je, wanajiandaa vizuri zaidi kukabiliana na mkazo wa maisha unaowapata sasa na utakaowapata wakati ujao? Au je, wanapanda mbegu za kujiletea matatizo zaidi?

  •    Tafuta njia bora za kukabiliana na mahangaiko. Njia nzuri za kupunguza mahangaiko zinatia ndani kufanya utendaji unaoboresha afya yako, kama vile kufanya mazoezi, kusoma, au kufurahia tafrija ukiwa na marafiki wanaokujenga. Unapokuwa na mambo mengi mazuri ya kukazia fikira, hutahisi unahitaji kuvuta sigara.

     Kanuni ya Biblia: “ Mahangaiko yaliyo moyoni mwa mtu huulemea moyo, lakini neno jema huuchangamsha.”​—Methali 12:25.

     “Watu hufikiri kuvuta sigara na kutumia sigara za kielektroni kutawasaidia kupunguza mkazo. Hata hivyo, vitu hivyo huandaa kitulizo cha muda tu na vinatokeza madhara ya kudumu. Kuna njia nzuri zaidi za kukabiliana na mkazo.”​—Angela.

     Jambo la kufikiria: Ni zipi baadhi ya njia ambazo wewe unaweza kukabiliana na mkazo kwa njia inayofaa? Ikiwa unahitaji msaada, ona makala ya “Vijana Huuliza” yenye kichwa “Ninawezaje Kukabiliana na Mahangaiko?

Kujaribu kukabiliana na mahangaiko kwa kutegemea vitu ambavyo vinaweza kukufanya uwe mraibu ni sawa na kujitupa ndani ya bahari ili kuepuka kunyeshewa na mvua; unajiongezea matatizo tu!

  •    Jitayarishe kukabiliana na shinikizo kutoka kwa wengine. Unaweza kushinikizwa na wanafunzi wenzako au hata kupitia burudani. Mara nyingi sinema, vipindi vya televisheni, na mitandao ya kijamii hufanya ionekane kwamba kuvuta sigara na kutumia sigara za kielektroni ni jambo lenye kupendeza na linalofurahisha.

     Kanuni ya Biblia: “Watu wakomavu . . . wamezoeza nguvu zao za utambuzi kwa kuzitumia ili kutofautisha mambo yaliyo sawa na mambo yasiyo sawa.”​—Waebrania 5:14.

     “Nilipokuwa shuleni, vijana wengi waliniheshimu kwa sababu sikuvuta sigara au kutumia sigara za kielektroni. Nilipoweka wazi msimamo wangu, walinitetea. Kwa hiyo, hata likionekana kuwa jambo la ajabu, kutangaza msimamo wako kunaweza kuwa ulinzi.”​—Anna.

     Jambo la kufikiria: Je, unaweza kusimama imara unaposhinikizwa na marafiki? Unaweza kutaja pindi ambazo umefanya hivyo? Ukihitaji msaada kufanya hivyo, ona ukurasa wa mazoezi wenye kichwa “Kukabiliana na Mkazo” katika sura ya 15 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2.

  •   Chagua marafiki wako kwa uangalifu. Huenda usishawishiwe sana kuvuta sigara au kutumia sigara za kielektroni ikiwa rafiki zako wana maoni kama yako kuhusu mazoea hayo.

     Kanuni ya Biblia: “Anayetembea na wenye hekima atakuwa na hekima, lakini anayeshirikiana na wapumbavu ataumia.”​—Methali 13:20.

     “Ni msaada mkubwa kuwa na marafiki ambao wana sifa kama vile kujidhibiti na utimilifu. Unapoona kwamba wana maisha mazuri unachochewa kuwa kama wao.”​—Calvin.

     Jambo la kufikiria: Je, rafiki zako wa karibu zaidi wanafanya iwe rahisi kwako kuishi maisha safi na yenye afya, au wanafanya iwe vigumu kwako kufanya hivyo?

 Vipi kuhusu kuvuta bangi?

 Watu wengi wanasema kwamba kuvuta bangi hakuna madhara. Lakini huo ni uwongo!

  •   Vijana wanaotumia bangi wanaweza kuwa waraibu. Uchunguzi unaonyesha kwamba bangi inaweza kusababisha madhara ya kudumu kwenye ubongo wako, madhara ambayo yanatia ndani kupunguza uwezo wako wa akili.

  •   Kulingana na Kituo cha Kuwahudumia Watumiaji wa Dawa za Kulevya na Afya ya Akili cha Marekani, “utafiti unaonyesha kwamba watu wanaotumia bangi wanakabili uwezekano mkubwa wa kuwa na matatizo katika mahusiano yao, kupata matokeo mbaya shuleni, kutofanikiwa sana kazini, na kutoridhika na maisha yao.”

     “Nilishawishika kutumia bangi hasa kwa sababu nilitaka kujiondolea mkazo wa mahangaiko. Lakini nilipofikiria jinsi ninavyoweza kuwa mraibu wake, pesa ambazo ningelazimika kutumia ili kuinunua, na madhara ya afya ambayo ningepata, nilitambua kwamba kuvuta bangi kungeniletea mahangaiko mengi zaidi.”​—Judah.