Hamia kwenye habari

VIJANA HUULIZA

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kileo?

Ninapaswa Kujua Nini Kuhusu Kileo?

 Biblia haikatazi kunywa kileo kwa kiasi ikiwa sheria ya nchi inakuruhusu kufanya hivyo. Hata hivyo, inakataza ulevi.​—Zaburi 104:15; 1 Wakorintho 6:​10.

 Lakini utafanyaje ukilazimishwa kunywa kileo wakati sheria ya nchi au wazazi wako hawakuruhusu kufanya hivyo?

 Fikiria mambo yatakayotokea baada ya kunywa

 Baadhi ya vijana wenzako huenda wanahisi kwamba kunywa kileo ni muhimu ili kufurahia maisha. Hata hivyo ni mambo gani yanayoweza kutokea baada ya kunywa kileo?

  •  Matatizo ya kisheria. Ikitegemea mahali unapoishi, ikiwa unakunywa kileo wakati sheria ya nchi unayoishi hairuhusu kufanya hivyo, unaweza kutozwa faini, kufunguliwa mashtaka ya uhalifu, kupoteza leseni yako ya udereva, kutakiwa kufanya utumishi fulani wa kijamii, au kufungwa gerezani.​—Waroma 13:3.

  •  Itaharibu sifa zako nzuri. Kileo kinapunguza uwezo wa kujizuia. Ukilewa unaweza kusema au kufanya mambo ambayo utajutia baadaye. (Methali 23:31-​33) Katika kipindi hiki ambacho mitandao ya kijamii inatumiwa sana, matendo yako yanaweza kuchafua sifa zako nzuri kwa muda mrefu.

  •  Inadhoofisha ulinzi. Kileo kinaweza kufanya iwe rahisi kushambuliwa kimwili au kingono. Pia, unaweza kuongozwa kwa urahisi na ushawishi wa wengine, jambo linaloweza kufanya ujihatarishe zaidi au utende kinyume cha sheria.

  •  Uraibu. Utafiti fulani unaonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa wa kuwa mraibu ikiwa ulianza kunywa kileo ukiwa na umri mdogo sana. Kunywa kileo ili kukabiliana na mikazo, upweke, au usumbufu kunaweza kufanya iwe vigumu sana kuacha zoea hilo.

  •  Kifo. Katika miaka ya karibuni, mtu mmoja hufa nchini Marekani kila baada ya dakika 52 kwa sababu ya dereva kuendesha gari akiwa amelewa. Katika kipindi cha miaka mitano, zaidi ya watu 1,500 walio chini ya umri wa miaka 21 walikufa kila mwaka kwa sababu ya aksidenti zilizosababishwa na ulevi. Hata ikiwa wewe hujanywa kileo, unajiweka katika mazingira hatari kama utakubali kuingia katika gari linaloendeshwa na mtu ambaye amelewa.

 Weka azimio

 Unaweza kuepuka hali ya hatari na gharama zinazotokana na kunywa kileo kupita kiasi ikiwa utaamua mapema mambo utakayofanya.

 Kanuni ya Biblia: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” (Methali 22:3) Si jambo la hekima kunywa kileo kabla ya kuendesha gari au kufanya kazi yoyote inayohitaji uwe mwangalifu sana.

 Azimio: ‘Ikiwa nitachagua kunywa kileo, nitafanya hivyo wakati sheria ya nchi na hali zinaniruhusu.’

 Kanuni ya Biblia: “Ninyi ni watumwa wake kwa sababu mnamtii yeye.” (Waroma 6:​16) Ikiwa unakunywa kileo kwa sababu rafiki zako wanakunywa, unawaruhusu wengine wakutawale. Ikiwa unakunywa ili kuepusha usumbufu au kukabiliana na mikazo, utashindwa kusitawisha ustadi wa kushughulikia matatizo yako.

 Azimio: ‘Sitawaruhusu rafiki zangu wanilazimishe kunywa kileo.’

 Kanuni ya Biblia: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno.” (Methali 23:20) Ukishirikiana na watu wabaya, watadhoofisha azimio lako. Unajiweka kwenye hatari ikiwa unakuwa pamoja na watu wanaokunywa kileo kupita kiasi.

 Azimio: ‘Sitashirikiana na watu wanaokunywa kileo kupita kiasi.’