Kitabu cha Kwanza cha Wafalme 8:1-66

  • Sanduku la agano laletwa hekaluni (1-13)

  • Sulemani awahutubia watu (14-21)

  • Sala ya Sulemani ya kuweka wakfu hekalu (22-53)

  • Sulemani awabariki watu (54-61)

  • Dhabihu na sherehe ya wakfu (62-66)

8  Wakati huo Sulemani aliwakusanya+ wazee wa Israeli—viongozi wote wa makabila, wakuu wa koo* za Israeli.+ Wakaja kwa Mfalme Sulemani huko Yerusalemu ili kuliondoa sanduku la agano la Yehova katika Jiji la Daudi,+ yaani, Sayuni.+  Wanaume wote wa Israeli wakakusanyika mbele ya Mfalme Sulemani wakati wa sherehe* katika mwezi wa Ethanimu,* yaani, mwezi wa saba.+  Basi wazee wote wa Israeli wakaja, na makuhani wakalibeba Sanduku.+  Wakalipandisha kutoka huko Sanduku la Yehova, hema la mkutano,+ na vyombo vyote vitakatifu vilivyokuwa katika hema hilo. Makuhani na Walawi wakavipandisha vitu hivyo.  Mfalme Sulemani na Waisraeli wote waliokusanywa ili wakutane naye, walikuwa mbele ya Sanduku. Kondoo na ng’ombe wengi sana wasiohesabika au kujulikana idadi walikuwa wakitolewa dhabihu.+  Kisha makuhani wakalileta sanduku la agano la Yehova mahali pake,+ katika chumba cha ndani zaidi cha nyumba, yaani, Patakatifu Zaidi, chini ya mabawa ya makerubi.+  Kwa hiyo mabawa ya makerubi yalikuwa yamenyooshwa juu ya mahali ambapo Sanduku liliwekwa, hivi kwamba makerubi hao walilifunika Sanduku na fito zake.+  Fito hizo+ zilikuwa ndefu sana hivi kwamba ncha zake zilionekana kutoka Patakatifu mbele ya chumba cha ndani zaidi, lakini hazikuonekana kutoka upande wa nje. Nazo ziko huko mpaka leo hii.  Hakukuwa na kitu kingine ndani ya Sanduku hilo isipokuwa yale mabamba mawili ya mawe+ ambayo Musa aliyaweka humo+ kule Horebu, Yehova alipofanya agano+ na Waisraeli walipokuwa wakitoka nchini Misri.+ 10  Makuhani walipotoka mahali patakatifu, wingu+ lilijaa katika nyumba ya Yehova.+ 11  Makuhani hawakuweza kusimama ili kuhudumu kwa sababu ya wingu hilo, kwa maana utukufu wa Yehova ulijaa katika nyumba ya Yehova.+ 12  Wakati huo Sulemani akasema: “Yehova alisema kwamba atakaa katika giza zito.+ 13  Nimefanikiwa kukujengea nyumba iliyokwezwa, mahali palipofanywa imara ili ukae humo milele.”+ 14  Kisha mfalme akageuka na kuanza kulibariki kutaniko lote la Waisraeli huku kutaniko lote la Waisraeli likiwa limesimama.+ 15  Akasema: “Na asifiwe Yehova Mungu wa Israeli, ambaye kwa kinywa chake mwenyewe alimwahidi baba yangu Daudi, na kwa mkono wake mwenyewe ametimiza, akisema, 16  ‘Kuanzia siku niliyowatoa watu wangu Waisraeli nchini Misri, sijachagua jiji katika makabila yote ya Israeli na kujenga humo nyumba ili jina langu likae humo,+ lakini nimemchagua Daudi awatawale watu wangu Waisraeli.’ 17  Moyo wa baba yangu Daudi ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli.+ 18  Lakini Yehova akamwambia Daudi baba yangu, ‘Moyo wako ulitamani kujenga nyumba kwa ajili ya jina langu, na ulifanya vizuri kutamani jambo hilo moyoni mwako. 19  Hata hivyo, hutajenga nyumba hiyo, lakini mwana wako mwenyewe utakayemzaa* ndiye atakayeijenga nyumba hiyo kwa ajili ya jina langu.’+ 20  Yehova ametimiza ahadi hiyo aliyoitoa, kwa maana nimechukua mahali pa baba yangu Daudi na kuketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli, kama Yehova alivyoahidi. Pia nimejenga nyumba kwa ajili ya jina la Yehova Mungu wa Israeli,+ 21  nami nimetenga mahali humo kwa ajili ya lile Sanduku lenye agano+ ambalo Yehova alifanya na mababu zetu alipokuwa akiwatoa nchini Misri.” 22  Kisha Sulemani akasimama mbele ya madhabahu ya Yehova mbele ya kutaniko lote la Waisraeli, akanyoosha mikono yake kuelekea mbinguni,+ 23  akasema: “Ee Yehova Mungu wa Israeli, hakuna Mungu kama wewe+ juu mbinguni wala chini duniani, unayeshika agano na kuwatendea kwa upendo mshikamanifu+ watumishi wako wanaotembea mbele zako kwa moyo wao wote.+ 24  Umetimiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu. Ulitoa ahadi hiyo kwa kinywa chako mwenyewe, na siku ya leo umeitimiza kwa mkono wako mwenyewe.+ 25  Na sasa, Ee Yehova Mungu wa Israeli, timiza ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ulipomwambia, ‘Hutakosa kamwe mwanamume wa uzao wako atakayeketi kwenye kiti cha ufalme cha Israeli mbele zangu, ikiwa tu wana wako watakazia uangalifu njia yao kwa kutembea mbele zangu, kama ulivyotembea mbele zangu.’+ 26  Na sasa, Ee Mungu wa Israeli, tafadhali acha ahadi uliyomwahidi mtumishi wako Daudi baba yangu ithibitike kuwa ya kweli. 27  “Lakini Ee Mungu, je, kweli utakaa duniani?+ Tazama! Mbingu, naam, mbingu za mbingu, haziwezi kukutosha;+ sembuse nyumba hii niliyoijenga!+ 28  Sasa sikiliza sala yangu mimi mtumishi wako na ombi langu la kutaka kibali, Ee Yehova Mungu wangu, sikiliza kilio changu cha kuomba msaada na sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali leo mbele zako. 29  Macho yako na yatazame nyumba hii usiku na mchana, yatazame mahali ambapo ulisema hivi kupahusu: ‘Jina langu litakuwa hapo,’+ ili usikilize sala ambayo mimi mtumishi wako ninasali kuelekea mahali hapa.+ 30  Nawe usikilize ombi langu mimi mtumishi wako la kutaka kibali na pia ombi ambalo watu wako Waisraeli wanaomba kuelekea mahali hapa, nawe usikilize katika makao yako mbinguni;+ naam, usikilize na kusamehe.+ 31  “Mwanadamu akimtendea dhambi mwanadamu mwenzake, naye aapishwe* na kuwekwa chini ya wajibu wa kiapo hicho,* naye akiwa chini ya kiapo* aje mbele ya madhabahu yako katika nyumba hii,+ 32  basi usikie kutoka mbinguni na kuchukua hatua na kuwahukumu watumishi wako kwa kumtangaza yule mwovu kuwa na hatia na kumwadhibu kwa sababu ya jambo alilotenda,* na kumtangaza mwadilifu kuwa asiye na hatia* na kumthawabisha kulingana na uadilifu wake mwenyewe.+ 33  “Watu wako Waisraeli wakishindwa na maadui kwa sababu ya kuzidi kukutendea dhambi,+ nao warudi kwako na kulitukuza jina lako+ na kusali na kukusihi wapate kibali katika nyumba hii,+ 34  basi usikie kutoka mbinguni na kuwasamehe watu wako Waisraeli dhambi yao na kuwarudisha katika nchi uliyowapa mababu zao.+ 35  “Mbingu zikifungwa kusiwe na mvua+ kwa sababu wamezidi kukutendea dhambi,+ nao wasali kuelekea mahali hapa na kulitukuza jina lako na kuacha dhambi yao kwa sababu umewanyenyekeza,*+ 36  basi usikie kutoka mbinguni na kuwasamehe watumishi wako dhambi yao, dhambi ya watu wako Waisraeli, kwa sababu utawafundisha+ njia nzuri wanayopaswa kufuata; na ulete mvua katika nchi yako+ ambayo uliwapa watu wako kuwa urithi. 37  “Njaa kali ikitokea nchini,+ au ugonjwa hatari, upepo unaochoma, kuvu,+ makundi ya nzige, au parare* wanaokula sana; au maadui wao wakiwazingira katika jiji lolote nchini* au pigo au ugonjwa wa aina yoyote ukitokea,+ 38  sala yoyote, ombi lolote la kutaka kibali+ ambalo huenda likatolewa na mtu yeyote au na watu wako wote Waisraeli (kwa sababu kila mmoja anajua mateso yaliyo katika moyo wake mwenyewe)+ wakinyoosha mikono yao kuelekea nyumba hii, 39  basi usikie kutoka mbinguni, makao yako,+ nawe usamehe+ na kuchukua hatua; na umthawabishe kila mmoja kulingana na njia zake zote,+ kwa sababu unajua moyo wake (ni wewe peke yako unayejua vizuri moyo wa kila mwanadamu),+ 40  ili wakuogope sikuzote watakazoishi katika nchi uliyowapa mababu zetu. 41  “Pia mgeni ambaye si sehemu ya watu wako Waisraeli na ambaye anatoka katika nchi ya mbali kwa sababu ya jina lako*+ 42  (kwa maana watasikia kuhusu jina lako kuu+ na mkono wako wenye nguvu na mkono wako ulionyooshwa), akija na kusali kuelekea nyumba hii, 43  basi usikilize kutoka mbinguni, makao yako,+ nawe ufanye mambo yote ambayo mgeni huyo anakuomba ufanye, ili watu wote duniani wajue jina lako na kukuogopa,+ kama watu wako Waisraeli wanavyokuogopa, na ili wajue kwamba nyumba hii niliyojenga imeitwa kwa jina lako. 44  “Watu wako wakienda vitani kupigana na maadui wao mahali utakapowaelekeza,+ nao wasali+ kwako wewe, Yehova, kuelekea jiji ambalo umechagua+ na kuelekea nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako,+ 45  basi usikie kutoka mbinguni sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao. 46  “Wakikutendea dhambi (kwa sababu hakuna mwanadamu asiyetenda dhambi),+ nawe uwakasirikie vikali na kuwaacha mikononi mwa maadui, na waliowateka wawapeleke katika nchi ya maadui, mbali au karibu;+ 47  nao warudiwe na ufahamu wakiwa katika nchi ya watu waliowachukua mateka,+ na kukurudia+ na kuomba kibali chako wakisema, ‘Tumetenda dhambi na kukosea; tumetenda uovu,’+ 48  nao wakurudie kwa moyo wao wote+ na kwa nafsi* yao yote katika nchi ya maadui wao waliowachukua mateka, nao wasali kwako kuelekea nchi yao ambayo uliwapa mababu zao na kuelekea jiji ambalo umelichagua na nyumba ambayo nimejenga kwa ajili ya jina lako,+ 49  basi usikie kutoka mbinguni, makao yako,+ sala yao na ombi lao la kutaka kibali, nawe utekeleze hukumu kwa ajili yao 50  na uwasamehe watu wako ambao wamekutendea dhambi, na kusamehe makosa yote waliyokukosea. Utafanya waliowateka wawahurumie,* nao watawahurumia+ 51  (kwa maana wao ni watu wako na urithi wako,+ uliowatoa Misri,+ kutoka ndani ya tanuru la kuyeyushia chuma).+ 52  Macho yako yatazame ombi langu mimi mtumishi wako la kutaka kibali+ na ombi la kutaka kibali la watu wako Waisraeli kwa kuwasikiliza wakati wowote wanapokulilia.*+ 53  Kwa maana uliwatenga wawe urithi wako kutoka kati ya mataifa yote ya dunia,+ kama ulivyotangaza kupitia mtumishi wako Musa ulipokuwa ukiwatoa mababu zetu Misri, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.” 54  Mara tu Sulemani alipomaliza kumtolea Yehova sala hiyo yote na kuomba kibali chake, aliinuka kutoka mbele ya madhabahu ya Yehova, mahali alipokuwa amepiga magoti akiwa amenyoosha mikono yake kuelekea mbinguni.+ 55  Kisha akasimama na kulibariki kwa sauti kubwa kutaniko lote la Waisraeli akisema: 56  “Na asifiwe Yehova, ambaye amewapa watu wake Waisraeli mahali pa kupumzikia, kama alivyoahidi.+ Hakuna ahadi yoyote kati ya ahadi zake zote nzuri ambazo aliahidi kupitia Musa mtumishi wake iliyokosa kutimia.+ 57  Yehova Mungu wetu na awe pamoja nasi kama tu alivyokuwa pamoja na mababu zetu.+ Naye asituache wala kututupa.+ 58  Na aivute mioyo yetu kwake+ ili tutembee katika njia zake zote na kushika amri zake, masharti yake, na sheria zake,* ambazo aliwaamuru mababu zetu washike. 59  Na maneno haya yangu ambayo nimesema ili kumwomba Yehova kibali na yawe karibu na Yehova Mungu wetu mchana na usiku, ili atekeleze hukumu kwa ajili yangu mimi mtumishi wake na kwa ajili ya watu wake Waisraeli kulingana na mahitaji ya kila siku, 60  ili mataifa yote duniani yajue kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.+ Hakuna mwingine!+ 61  Basi acheni mioyo yenu iwe kamili+ kwa* Yehova Mungu wetu kwa kufuata masharti yake na kushika amri zake kama ilivyo leo.” 62  Kisha mfalme na Waisraeli wote wakamtolea Yehova dhabihu kubwa.+ 63  Sulemani alimtolea Yehova dhabihu za ushirika:+ Alitoa ng’ombe 22,000 na kondoo 120,000. Basi mfalme na Waisraeli wote wakaizindua nyumba ya Yehova.+ 64  Siku hiyo ilimbidi mfalme atakase sehemu ya katikati ya ua ulio mbele ya nyumba ya Yehova, kwa sababu alipaswa kutolea mahali hapo dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na vipande vya mafuta vya dhabihu za ushirika, kwa sababu madhabahu ya shaba+ iliyo mbele za Yehova ilikuwa ndogo sana isiweze kutoshea dhabihu za kuteketezwa, matoleo ya nafaka, na vipande vya mafuta+ vya dhabihu za ushirika. 65  Wakati huo Sulemani alifanya sherehe hiyo+ pamoja na Waisraeli wote, kutaniko kubwa kuanzia Lebo-hamathi* na kushuka mpaka kwenye Korongo* la Misri,+ mbele za Yehova Mungu wetu kwa siku 7 na kisha siku nyingine 7, jumla ya siku 14. 66  Siku iliyofuata,* aliwaruhusu watu waondoke, nao wakambariki mfalme na kwenda nyumbani kwao wakishangilia na kufurahi moyoni kwa sababu ya wema wote+ ambao Yehova alikuwa amemtendea Daudi mtumishi wake na watu wake Waisraeli.

Maelezo ya Chini

Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, Sherehe ya Vibanda.
Tnn., “mwana wako, atakayetoka katika viuno vyako.”
Au “aliyetendewa dhambi akimweka chini ya laana.” Yaani, kiapo kinacholeta laana ikiwa mtu anaapa kwa uwongo au kukosa kutimiza kiapo hicho.
Tnn., “laana.”
Tnn., “laana.”
Tnn., “kuleta juu ya kichwa chake mwenyewe jambo alilotenda.”
Tnn., “kuwa mwadilifu.”
Au “umewatesa.”
Au “panzi.”
Tnn., “katika nchi ya malango yake.”
Au “sifa yako.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “Utawafanya wawe vitu vya kuhurumiwa mbele ya waliowateka.”
Au “kuwasikiliza wanapokuomba jambo lolote.”
Tnn., “maamuzi yake.”
Au “imtumikie kikamili.”
Au “njia ya kuingia Hamathi.”
Angalia Kamusi.
Tnn., “Siku ya nane,” yaani, siku iliyofuata kipindi cha pili cha siku saba.