Kumbukumbu la Torati 8:1-20

  • Baraka kutoka kwa Yehova zatajwa tena (1-9)

    • “Haishi kwa mkate tu” (3)

  • Msimsahau Yehova (10-20)

8  “Mnapaswa kuwa waangalifu kushika kila amri ninayowapa leo, ili mwendelee kuishi, mwongezeke,+ mwingie na kuimiliki nchi ambayo Yehova aliwaapia mababu zenu.+  Kumbukeni njia ndefu ambayo Yehova Mungu wenu alifanya mtembee nyikani kwa miaka hii 40,+ ili awanyenyekeze na kuwajaribu+ ili ajue yaliyokuwa mioyoni mwenu,+ aone kama mngezishika amri zake au la.  Kwa hiyo aliwanyenyekeza na kuwaacha mkae njaa,+ naye akawalisha mana,+ ambayo ninyi wala baba zenu hamkuwa mmeijua, ili awafundishe kwamba mwanadamu haishi kwa mkate tu bali huishi kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.+  Nguo mlizovaa hazikuchakaa, wala miguu yenu haikuvimba miaka hiyo 40.+  Mnajua vizuri mioyoni mwenu kwamba kama baba anavyomrekebisha mwana wake, ndivyo Yehova Mungu wenu alivyokuwa akiwarekebisha.+  “Basi ni lazima mshike amri za Yehova Mungu wenu kwa kutembea katika njia zake na kumwogopa yeye.  Kwa maana Yehova Mungu wenu anawaleta katika nchi nzuri,+ nchi yenye vijito vya maji, mabubujiko na chemchemi zinazotiririka* katika bonde tambarare na katika eneo lenye milima,  nchi yenye ngano na shayiri, na mizabibu, mitini, na mikomamanga,+ nchi yenye mafuta ya zeituni na asali,+  nchi ambayo haitakuwa na upungufu wa chakula na hamtakosa chochote, nchi yenye mawe yaliyo na chuma na katika milima yake mtachimba shaba. 10  “Baada ya kula na kushiba, mnapaswa kumsifu Yehova Mungu wenu kwa sababu ya nchi nzuri ambayo amewapa.+ 11  Jihadharini msimsahau Yehova Mungu wenu kwa kutoshika amri zake, maagizo yake, na sheria zake ambazo ninawaamuru leo. 12  Baada ya kula na kushiba na kujenga nyumba nzuri na kukaa humo,+ 13  ng’ombe wenu na kondoo wenu watakapokuwa wameongezeka na fedha yenu na dhahabu yenu itakapokuwa imeongezeka na mtakapokuwa na wingi wa vitu vyote, 14  msiache mioyo yenu iwe na kiburi+ na kuwafanya mumsahau Yehova Mungu wenu, aliyewatoa nchini Misri, kutoka katika nyumba ya utumwa,+ 15  aliyewafanya mtembee katika nyika kubwa na yenye kutisha,+ iliyo na nyoka wenye sumu na nge na ardhi iliyokauka isiyo na maji. Alifanya maji yatiririke kutoka katika mwamba mgumu+ 16  na kuwalisha mana+ nyikani, ambayo baba zenu hawakuwa wameijua, ili awanyenyekeze+ na kuwajaribu ili awanufaishe baadaye.+ 17  Mkijiambia mioyoni mwenu, ‘Nimepata utajiri huu kwa nguvu zangu mwenyewe na uwezo wa mkono wangu mwenyewe,’+ 18  kumbukeni kwamba Yehova Mungu wenu ndiye anayewapa nguvu za kupata utajiri,+ ili atimize agano lake ambalo aliwaapia mababu zenu, kama ilivyo leo.+ 19  “Ikiwa mtamsahau Yehova Mungu wenu na kufuata miungu mingine na kuiabudu na kuiinamia, nashuhudia dhidi yenu leo kwamba hakika mtaangamia.+ 20  Mtaangamia kama mataifa ambayo Yehova anayaangamiza mbele yenu, kwa sababu hamkuisikiliza sauti ya Yehova Mungu wenu.+

Maelezo ya Chini

Au “vyanzo vya maji vyenye kina kirefu.”