Yeremia 38:1-28

  • Yeremia atupwa ndani ya tangi (1-6)

  • Ebed-meleki amwokoa Yeremia (7-13)

  • Yeremia amsihi Sedekia ajisalimishe (14-28)

38  Sasa Shefatia mwana wa Matani, Gedalia mwana wa Pashuri, Yukali+ mwana wa Shelemia, na Pashuri+ mwana wa Malkiya wakasikia maneno ambayo Yeremia alikuwa akiwaambia watu wote, akisema:  “Yehova anasema hivi: ‘Yule atakayebaki katika jiji hili atakufa kwa upanga, kwa njaa kali, na kwa ugonjwa hatari.+ Lakini yule atakayejisalimisha* kwa Wakaldayo ataendelea kuishi naye atapata uhai wake* kama nyara* na kuendelea kuishi.’+  Yehova anasema hivi: ‘Kwa kweli jiji hili litatiwa mikononi mwa jeshi la mfalme wa Babiloni, naye ataliteka.’”+  Wakuu wakamwambia mfalme: “Tafadhali agiza mtu huyu auawe,+ kwa maana hivyo ndivyo anavyoidhoofisha mioyo* ya wanajeshi waliobaki jijini, na pia ya watu wote, kwa kuwaambia maneno hayo. Kwa maana mtu huyu hawatakii amani watu hawa, bali msiba.”  Mfalme Sedekia akajibu: “Tazama! Yuko mikononi mwenu, kwa maana mfalme hawezi kufanya jambo lolote ili kuwazuia.”  Basi wakamchukua Yeremia na kumtupa ndani ya tangi la maji la Malkiya mwana wa mfalme, lililokuwa katika Ua wa Walinzi.+ Wakamshusha Yeremia ndani kwa kamba. Basi hapakuwa na maji ndani ya tangi hilo, ila matope tu, naye Yeremia akaanza kuzama ndani ya matope.  Ebed-meleki+ Mwethiopia, towashi* aliyekuwa katika nyumba ya* mfalme, akasikia kwamba wamemtia Yeremia ndani ya tangi. Sasa mfalme alikuwa ameketi katika Lango la Benjamini,+  basi Ebed-meleki akatoka katika nyumba ya* mfalme na kuzungumza na mfalme, akisema:  “Ee bwana wangu mfalme, watu hawa wamemtendea Yeremia uovu! Wamemtupa ndani ya tangi, naye atafia humo kwa sababu ya njaa kali, kwa maana hakuna mkate uliobaki jijini.”+ 10  Ndipo mfalme akamwamuru hivi Ebed-meleki Mwethiopia: “Chukua watu 30 kutoka mahali hapa, nawe umvute nabii Yeremia kutoka katika tangi hilo kabla hajafa.” 11  Basi Ebed-meleki akawachukua wale watu na kwenda kwenye nyumba ya* mfalme sehemu iliyokuwa chini ya hazina,+ naye akachukua kutoka sehemu hiyo matambara yaliyochakaa na vipande vya nguo vilivyochakaa na kumshushia Yeremia ndani ya tangi hilo kwa kamba. 12  Ndipo Ebed-meleki Mwethiopia akamwambia Yeremia: “Tafadhali weka matambara na vipande hivyo vya nguo kati ya makwapa yako na kamba.” Yeremia akafanya hivyo, 13  nao wakamvuta Yeremia nje kwa zile kamba na kumtoa ndani ya tangi hilo. Na Yeremia akaendelea kukaa katika Ua wa Walinzi.+ 14  Mfalme Sedekia akaagiza Yeremia aletwe kwake kwenye mlango wa tatu, ulio katika nyumba ya Yehova, naye mfalme akamwambia Yeremia: “Ningependa kukuuliza jambo fulani. Usinifiche jambo lolote.” 15  Ndipo Yeremia akamwambia Sedekia: “Nikikuambia, kwa kweli utaniua. Nami nikikushauri, hutanisikiliza.” 16  Basi Mfalme Sedekia akamwapia Yeremia kisiri, akisema: “Kwa hakika kama Yehova anavyoishi, ambaye ametupatia uhai huu, sitakuua, nami sitakutia mikononi mwa watu hawa wanaotaka kukuua.”* 17  Kisha Yeremia akamwambia Sedekia: “Yehova, Mungu wa majeshi, Mungu wa Israeli, anasema hivi: ‘Ukijisalimisha* kwa wakuu wa mfalme wa Babiloni, uhai wako utaokoka,* na jiji hili halitateketezwa kwa moto, na wewe na watu wa nyumba yako mtaokoka.+ 18  Lakini usipojisalimisha* kwa wakuu wa mfalme wa Babiloni, jiji hili litatiwa mikononi mwa Wakaldayo, nao wataliteketeza kwa moto,+ nawe hutaponyoka mikononi mwao.’”+ 19  Kisha Mfalme Sedekia akamwambia Yeremia: “Ninawaogopa Wayahudi ambao wamekimbia kwenda kwa Wakaldayo, kwa maana nikitiwa mikononi mwao watanitendea ukatili.” 20  Lakini Yeremia akasema: “Hutatiwa mikononi mwao. Tafadhali, itii sauti ya Yehova kuhusiana na yale ninayokuambia, na mambo yatakuendea vema, nawe utaendelea kuishi. 21  Lakini ukikataa kujisalimisha,* Yehova amenifunulia jambo hili: 22  Tazama! Wanawake wote waliobaki katika nyumba ya* mfalme wa Yuda wanatolewa nje kwa wakuu wa mfalme wa Babiloni,+ nao wanasema,‘Watu uliowatumaini* wamekudanganya na kukushinda.+ Wamefanya mguu wako uzame kwenye matope. Sasa wamegeuka na kurudi nyuma.’ 23  Nao wanawatoa nje wake zako wote na wanao wote na kuwapeleka kwa Wakaldayo, nawe hutaponyoka mikononi mwao, lakini utakamatwa na mfalme wa Babiloni,+ na kwa sababu yako, jiji hili litateketezwa kwa moto.”+ 24  Kisha Sedekia akamwambia Yeremia: “Usimwambie mtu yeyote mambo haya, ili usife. 25  Na wakuu wakisikia kwamba nimezungumza nawe nao waje na kukuambia, ‘Tafadhali, tuambie ulichomwambia mfalme. Usitufiche jambo lolote, nasi hatutakuua.+ Mfalme alikuambia nini?’ 26  utawajibu hivi: ‘Nilikuwa nikimwomba mfalme asinirudishe katika nyumba ya Yehonathani ili nisifie humo.’”+ 27  Baadaye wakuu wote wakamjia Yeremia na kumuuliza maswali. Akawaambia mambo yote ambayo mfalme alimwamuru aseme. Basi hawakumwambia jambo lolote zaidi, kwa maana hakuna mtu aliyesikia mazungumzo hayo. 28  Mpaka siku ambayo Yerusalemu lilitekwa, Yeremia alikaa katika Ua wa Walinzi;+ bado alikuwa humo Yerusalemu lilipotekwa.+

Maelezo ya Chini

Tnn., “atakayeenda.”
Au “nafsi yake.”
Au “ataponyoka na uhai wake.”
Tnn., “mikono.”
Au “ofisa wa makao ya mfalme.”
Au “jumba la.”
Au “jumba la.”
Au “jumba la.”
Au “wanaotafuta nafsi yako.”
Tnn., “ukienda nje.”
Au “nafsi yako itaendelea kuishi.”
Tnn., “usipoenda nje.”
Tnn., “kwenda nje.”
Tnn., “Watu wa amani yako.”
Au “jumba la.”