Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mwandikie Anton Barua!”

“Mwandikie Anton Barua!”

“Mwandikie Anton Barua!”

● Kijana mmoja anayeitwa Anton ambaye ni Shahidi wa Yehova alikuwa akiishi katika kijiji cha mbali cha Schelkan huko Stavropol’ Kray, Urusi. Alipokuwa mtoto, iligunduliwa kuwa ana ugonjwa wa Duchenne muscular dystrophy ambao hauna tiba na hufanya misuli idhoofike haraka na kusababisha kifo kabla mtu hajafikia umri wa miaka 20. Alipofikia umri wa miaka tisa, Anton hangeweza kutembea au kuinuka.

Walipotembelea kutaniko moja la Mashahidi, Yevgeny, na mke wake Diana, walikutana na Anton. Diana alieleza hivi: “Anton alionekana dhaifu sana kimwili, lakini alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu. Kwa kuwa kaka yake alikuwa amekufa kutokana na ugonjwa huo alipokuwa na umri wa miaka 19, Anton alijua kwamba yeye pia angekufa karibuni. Lakini bado alikuwa na furaha na mtazamo mzuri.”

Diana na mume wake walimtia moyo Anton apanue huduma yake kwa kuwaandikia barua watu walioishi katika vijiji vingine vilivyokuwa mbali. Katika mwaka wa 2005, Anton aliandika barua 500 hivi na kuzituma kwa watu waliokuwa katika vijiji vya karibu. Hata hivyo, alivunjika moyo kwa kuwa hakupata jibu lolote. Ingawa alivunjika moyo, Anton aliendelea kuwaandikia watu barua, na alisali kwa bidii apate mwelekezo wa jinsi ya kuwa mhudumu mwenye matokeo licha ya hali zake.

Siku moja, Anton alipokuwa akisoma gazeti fulani, aliona barua kutoka kwa mwanamke mgonjwa aliyehitaji faraja. Anton alimwandikia barua, na sehemu ya barua hiyo ilichapishwa katika gazeti hilo. Ilisema hivi: “Ingawa nina ugonjwa usioweza kupona, kusoma Biblia hunisaidia niwe na tumaini la wakati ujao. Mimi hupenda sana kupokea barua na huzisubiri kwa hamu.”

Mwanamke huyo aliguswa sana na barua hiyo, kwa hiyo akaandika barua katika gazeti hilo. Barua hiyo ilichapishwa katika makala iliyokuwa na kichwa “Mwandikie Anton Barua!” Mwanamke huyo alimshukuru Anton kwa maneno yake yenye kutia moyo kuhusu kusoma Biblia, kisha akaandika: “Tumsaidie Anton! Acheni tumwandikie barua. Kijana huyu anahitaji sana maneno yenye fadhili!” Alionyesha anwani ya Anton kwenye makala hiyo.

Anton alianza kupokea barua kupitia ofisi ndogo ya posta katika kijiji chao—nyakati nyingine alipokea barua 30 hivi kwa siku! Barua hizo zilitoka kotekote Urusi, kutia ndani nchi za Baltiki, Ujerumani, na hata Ufaransa. Alipokea mamia ya barua kutoka kwa wasomaji wa gazeti hilo. Diana anasema hivi: “Anton alijawa na shangwe! Sasa angeweza kuwaandikia mamia ya watu na kuwaambia kuhusu imani yake inayotegemea Biblia.”

Kwa zaidi ya mwaka mmoja, Anton aliwasiliana kupitia barua na wale waliokuwa wamemwandikia na kuwaambia kweli za Biblia. Pole kwa pole, mikono yake ilipoanza kudhoofika, Anton alimwomba mtu fulani amwandikie barua hizo. Mnamo Septemba (Mwezi wa 9) 2008, Anton alikufa akiwa na umri wa miaka 20. Ingawa alikuwa dhaifu sana kimwili, imani yake na upendo wake wa kuhubiri ulimpa nafasi ya kuzungumzia mambo yaliyogusa maisha ya watu wengi.