Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Lazima Tuwe na Siku Moja Takatifu Kila Juma?

Je, Lazima Tuwe na Siku Moja Takatifu Kila Juma?

Maoni ya Biblia

Je, Lazima Tuwe na Siku Moja Takatifu Kila Juma?

ULIMWENGUNI pote, mamilioni ya Waislamu, Wayahudi, na wale wanaodai kuwa Wakristo wametenga siku moja kila juma kwa ajili ya utendaji wa pekee wa kidini. Kwa nini? Kwa mfano, Ibrahim, mwanamume anayeshikilia sana imani ya Uislamu ambaye huenda kwenye msikiti kila Ijumaa (Siku ya 5) ili kusali na kusikiliza mafundisho anasema hivi: “Ninataka nijihisi kwamba niko karibu na Mungu na kupata amani ya akili.”

Je, Biblia inafundisha kwamba Mungu anataka tutenge siku moja kila juma kuwa takatifu? Je, kuabudu katika siku fulani hususa ndiyo siri ya kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu?

Mpango wa Muda Tu

Zaidi ya miaka 3,500 iliyopita, Mungu alimpa nabii Musa orodha ya sheria za pekee. Sheria hiyo ilitia ndani siku fulani za mapumziko, au Sabato, ambazo zilitengwa kwa ajili ya ibada. Siku ya mapumziko iliyoshikiliwa sana ilikuwa Sabato ya kila juma. Ilianza baada ya jua kushuka siku ya Ijumaa na kuendelea hadi jua kushuka siku ya Jumamosi (Siku ya Posho).—Kutoka 20:8-10.

Je, watu wa mataifa yote walipaswa kutenga siku hiyo iwe ya mapumziko kila juma? La. Sheria ya Musa ilitolewa hasa kwa ajili ya Waisraeli na watu waliogeuzwa imani. Mungu alimwambia hivi Musa: “Wana wa Israeli lazima waishike sabato . . . Kati yangu na wana wa Israeli ni ishara mpaka wakati usio na kipimo.” *Kutoka 31:16, 17.

Biblia inasema kwamba Sheria ya Musa ilikuwa “kivuli cha mambo yanayokuja.” (Wakolosai 2:17) Kwa hiyo, Sabato ilikuwa sehemu ya mpango wa ibada wa muda tu ambao ulitangulia kuonyesha mpango bora zaidi wa wakati ujao. (Waebrania 10:1) Biblia inaonyesha kwamba kwa maoni ya Mungu, Sheria waliyopewa Waisraeli, kutia ndani takwa la kushika Sabato ya kila juma, ilifikia kikomo Yesu alipokufa. (Waroma 10:4) Ni nini kilichochukua mahali pake?

Njia Mpya ya Kuabudu

Biblia inaonyesha waziwazi njia ya ibada ambayo ilikubaliwa na Mungu baada ya Sheria ya Musa kutimiza kusudi lake. Je, inatia ndani kutenga siku fulani hususa kila juma kwa ajili ya ibada?

Maandiko yanaonyesha kwamba amri fulani walizopewa Waisraeli ziliwahusu pia wale waliokuwa katika kutaniko la Kikristo. Amri hizo zilitia ndani kujiepusha na ibada ya sanamu, uasherati, na kula damu. (Matendo 15:28, 29) Amri kuhusu Sabato ya kila juma hazikutiwa ndani ya amri ambazo Wakristo walipaswa kutii.—Waroma 14:5.

Biblia inatuambia jambo gani lingine kuhusu jinsi Wakristo wa karne ya kwanza walivyoabudu? Walikutana kwa ukawaida ili kusali, kusoma maandiko, kusikiliza hotuba, na kumwimbia Mungu nyimbo za sifa. (Matendo 12:12; Wakolosai 3:16) Kwenye mikutano hiyo, Wakristo walifundishwa, imani yao iliimarishwa, na walitiana moyo.—Waebrania 10:24, 25.

Biblia haitaji popote kwamba mikutano ya Kikristo ilipaswa kufanywa siku ya Jumapili (Siku ya Yenga) au siku nyingine hususa katika juma. Kwa hiyo basi, kwa nini watu wengi wanaodai kuwa Wakristo huona Jumapili kuwa ndiyo siku takatifu? Desturi ya kufanya ibada siku ya Jumapili ilianza baada ya Biblia kukamilishwa na imani na desturi nyingi zisizo za Kimaandiko zilikuwa zimeanza kufuatwa.

Je, baadaye Mungu alianzisha tena mpango wa kuwa na siku moja katika juma ya watu kukutana pamoja ili kuabudu? La. Mpango wote wa ibada ya kweli umeandikwa waziwazi katika Biblia. Hakuna maandishi mengine yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo yameongezwa katika Maandiko Matakatifu. Mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika hivi: “Hata ikiwa sisi au malaika kutoka mbinguni tungewatangazia ninyi kuwa habari njema jambo fulani kupita lile tulilowatangazia ninyi kuwa habari njema, mtu huyo na alaaniwe.”—Wagalatia 1:8.

Ibada Yenye Kuburudisha Inayompendeza Mungu

Ingawa viongozi wa kidini katika siku za Yesu walifuata sana desturi ya kutenga siku takatifu kila juma, ibada yao haikukubaliwa na Mungu kwa sababu walikuwa waovu moyoni. Walipenda pesa na waliwadharau watu wa kawaida waliokuwa maskini. Walitaka umashuhuri, walikuwa wafisadi, na walijihusisha sana katika mizozo ya kisiasa ya wakati huo. (Mathayo 23:6, 7, 29-33; Luka 16:14; Yohana 11:46-48) Walidai kuwa wanamwakilisha Mungu. Lakini waligeuza Sabato, ambayo Mungu alikusudia iwe yenye kuburudisha, na kuifanya iwe na sheria za wanadamu zenye kukandamiza.—Mathayo 12:9-14.

Ni wazi kwamba ibada haimpendezi Mungu eti tu kwa sababu mtu ametenga siku moja iwe takatifu. Ni nini kinachofanya ibada impendeze? Yesu alitoa mwaliko huu wenye kuvutia: “Njooni kwangu, nyote mnaotaabika na kulemewa na mizigo, nami nitawaburudisha ninyi.” (Mathayo 11:28) Ibada ambayo inategemea kabisa mafundisho ya Yesu inaburudisha kwelikweli. Haina unafiki wala desturi zenye kulemea.

Ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova hufuata kwa ukaribu kielelezo cha ibada kilichofuatwa na wafuasi wa Yesu wa karne ya kwanza. Mashahidi huwa na programu ya kila juma ya kujifunza Biblia. Siku za kufanya mikutano hiyo huchaguliwa kulingana na hali za kila eneo na si kwa kufuata desturi zisizo za Kimaandiko. Tunakualika uhudhurie mkutano kama huo katika eneo lenu na ujionee mwenyewe ibada yenye kuburudisha.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Maneno “wakati usio na kipimo” yanayopatikana katika Biblia hayamaanishi milele kila wakati. Yanaweza pia kumaanisha kipindi kirefu cha wakati ambacho si hususa.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Je, ni lazima umwabudu Mungu siku fulani hususa katika juma?—Waroma 10:4; 14:5.

● Kwa nini tunapaswa kukutana pamoja ili kuabudu?—Waebrania 10:24, 25.

● Ni nini siri ya ibada ambayo inaridhisha?—Mathayo 11:28.

[Chati/​Picha katika ukurasa wa 10, 11]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

JUMANNE

JUMATANO

1 ALHAMISI

2 IJUMAA

3 JUMAMOSI

4 JUMAPILI