Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kufanikisha Ndoa

Jinsi ya Kufanikisha Ndoa

Maoni ya Biblia

Jinsi ya Kufanikisha Ndoa

“Yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja’ . . . Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Yesu Kristo, kama ilivyoandikwa kwenye Mathayo 19:4-6.

KATIKA ulimwengu wa leo wenye viwango vinavyobadilika-badilika, ndoa haiheshimiwi tena. Watu wengi waliooana huishi pamoja hadi wanapoacha kuvutiwa kimapenzi na wenzi wao au matatizo yanatokea—nyakati nyingine si matatizo makubwa—kisha wanatengana au kutalikiana. Kwa kusikitisha, mara nyingi watoto wa wenzi hao ndio huathiriwa sana.

Watu wanaosoma Biblia hawashangazwi na hali hiyo. Kuhusu “siku za mwisho,” kipindi ambacho tunaishi, Biblia ilitabiri kwamba watu kwa ujumla hawatakuwa na sifa ambazo huunganisha familia pamoja—sifa kama ushikamanifu, upendo wa kweli, na upendo wa asili. (2 Timotheo 3:1-5) Je, kuzorota kwa maadili na madhara yake kwa maisha ya familia kunakuhangaisha? Je, wewe unaiheshimu ndoa?

Ikiwa unahangaishwa, unaweza kufarijiwa na Biblia, kwa kuwa mashauri yake ambayo yametumika kwa muda mrefu yameendelea kuwasaidia wenzi wengi. Kwa mfano, fikiria kanuni tano tu ambazo zimesaidia sana ndoa. *

Mambo Matano ya Kufanikisha Ndoa

(1) Ione ndoa kuwa muungano mtakatifu. Kama inavyoonyeshwa na maneno ya Yesu yaliyonukuliwa hapa kando, yeye na Muumba, Yehova Mungu, wanaiona ndoa kuwa muungano mtakatifu. Jambo hilo linakaziwa na shauri kali la Mungu kwa wanaume fulani wa kale ambao waliwataliki wake zao ili waoe wanawake wachanga. “Umeivunja ahadi yako kwa mke uliyeoa ulipokuwa kijana,” Mungu akasema. “Alikuwa mwenzi wako, na umeivunja ahadi yako kwake, ingawa uliahidi mbele za Mungu kwamba utakuwa mwaminifu kwake.” Kisha Yehova anasema maneno haya mazito: “Ninachukizwa mtu anapofanya ukatili huo kwa mke wake.” (Malaki 2:14-16, Today’s English Version) Ni wazi kwamba Mungu anaheshimu sana ndoa; anaona jinsi ambavyo waume na wake wanatendeana.

(2) Uwe mume anayetimiza wajibu wake. Kunapokuwa na mambo muhimu ya familia, mtu fulani lazima afanye uamuzi wa mwisho. Biblia inampa mume daraka hilo. “Mume ni kichwa cha mke wake,” inasema Waefeso 5:23. Lakini hapaswi kutumia ukichwa huo kwa ukatili. Mume anapaswa kukumbuka kwamba yeye na mke wake ni “mwili mmoja,” na anapaswa kumpa heshima na kushauriana naye kuhusu mambo ya familia. (1 Petro 3:7) Biblia inashauri kwamba “waume wanapaswa kuwa wakiwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.”—Waefeso 5:28.

(3) Uwe mke anayemuunga mkono mume wake. Biblia inamtaja mke kuwa “kikamilisho” cha mume wake. (Mwanzo 2:18) Kwa hiyo, yeye huchangia sifa muhimu katika ndoa. Akiwa kikamilisho cha mume wake, yeye hashindani naye, bali anamuunga mkono kwa upendo, na hivyo kufanya familia iwe na amani. “Wake na wajitiishe kwa waume zao kama kwa Bwana,” inasema Waefeso 5:22. Namna gani ikiwa hakubaliani na mume wake kuhusu jambo fulani? Ikiwa hivyo, anapaswa kuwa uhuru kueleza maoni yake kwa heshima kama vile tu angetaka mume wake azungumze naye.

(4) Ona mambo kihalisi, na utazamie matatizo. Ndoa inaweza kupata matatizo kwa sababu ya maneno yasiyo ya fadhili au yanayosemwa bila kufikiri, matatizo ya kifedha, ugonjwa mbaya, au mikazo ya kuwalea watoto. Hivyo, Biblia inasema wazi kwamba wale wanaofunga ndoa “watakuwa na dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Lakini dhiki, au majaribu, hayapaswi kudhoofisha ndoa. Kwa kweli, ikiwa watu wawili wanapendana na wana hekima ya kimungu, wanaweza kutatua masuala yanayoweza kusababisha mgawanyiko. Je, una hekima ya kutosha kutatua matatizo ambayo huenda yakatokea katika familia yako? Biblia inasema kwamba “ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu.”—Yakobo 1:5.

(5) Uwe mwaminifu kwa mwenzi wako. Uasherati, au ngono nje ya ndoa, ni mojawapo ya mambo yanayoharibu ndoa na ndio msingi pekee wa talaka inayokubaliwa na Mungu. (Mathayo 19:9) Biblia inasema: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi, kwa maana Mungu atawahukumu waasherati na wazinzi.” (Waebrania 13:4) Wenzi wa ndoa wanapaswa kufanya nini ili wasishawishiwe kutosheleza hamu ya ngono nje ya ndoa? Biblia inasema: “Mume na ampe mke wake haki yake; lakini mke pia na amfanyie vivyo hivyo mume wake.”—1 Wakorintho 7:3, 4.

Huenda wengine wakaona mambo hayo matano kuwa mazuri lakini waseme kuwa yamepitwa na wakati. Lakini matokeo ya kuyafuata yameonekana wazi. Kwa kweli, matokeo yake ni kama ya mtu anayetafuta mwongozo wa Mungu katika sehemu zote za maisha yake: “Hakika atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.” (Zaburi 1:2, 3) “Kila jambo” linatia ndani kufanikiwa katika ndoa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Kwa habari zaidi kuhusu ndoa, ona gazeti la Mnara wa Mlinzi la Februari 1, 2011.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Mungu ana maoni gani kuhusu talaka?—Malaki 2:14-16.

● Mume anapaswa kumtendea mke wake jinsi gani?—Waefeso 5:23, 28.

● Ni hekima ya nani inayofanikisha ndoa?—Zaburi 1:2, 3.