Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Jinsi ya Kuwasiliana na Kijana Wako

Jinsi ya Kuwasiliana na Kijana Wako

KIKWAZO

Alipokuwa mtoto, alizungumza nawe kuhusu kila jambo. Sasa amekuwa  tineja, hakuambii chochote. Unapojaribu kuzungumza naye, anazungumza akiwa amenuna au anaanza mabishano ambayo yanageuza nyumba yenu kuwa uwanja wa vita.

Unaweza kujifunza  kuzungumza na kijana wako. Kwanza fikiria mambo mawili yanayoweza kuwa kikwazo.

KWA NINI JAMBO HILI HUTUKIA

Tamaa ya kujitegemea. Ili kijana wako awe mtu mzima mwenye kutegemeka, kwa njia ya mfano, anapaswa kuacha hatua kwa hatua kuwa abiria anayeendeshwa na awe dereva anayeendesha maisha yake kwenye barabara yenye vikwazo vingi. Bila shaka, baadhi ya matineja hutaka uhuru zaidi kuliko wanavyostahili, na kwa upande mwingine, baadhi ya wazazi huwapa matineja wao uhuru kidogo kuliko wanavyopaswa kuwapa. Tatizo hilo la vuta-nikuvute linaweza kusababisha mvurugo mkubwa kati ya wazazi na matineja. “Wazazi wangu hujaribu kudhibiti kila sehemu ya maisha yangu,” alalamika Brad mwenye umri wa miaka 16. * “Kama hawatanipa uhuru zaidi nitakapofika umri wa miaka 18, nitaondoka nyumbani!”

Uwezo wa kuchanganua mambo. Watoto wadogo wana mwelekeo wa kuyaona mambo jinsi yalivyo tu, lakini matineja wengi wanaweza kuona mambo yasiyo wazi kabisa. Kufanya hivyo kunawasaidia kuchanganua mambo na hilo huwawezesha vijana kusitawisha uwezo wa kufanya maamuzi mazuri. Fikiria mfano huu: Kwa mtoto, usawa humaanisha: ‘Mama aligawa biskuti vipande viwili, akanipa nusu na ile nusu nyingine akampa ndugu yangu.’ Kwa maoni ya mtoto, kugawa vitu kwa usawa ndio kutenda kwa haki. Hata hivyo, matineja wanatambua kwamba kutenda kwa haki kunahusisha mengi zaidi ya hayo. Kwa kweli, si mara zote kutenda kwa haki kunamaanisha kuwatendea wote kwa usawa, na si mara zote kuwatendea wote kwa usawa kunamaanisha unatenda kwa haki. Uwezo wa kuchanganua mambo humwezesha kijana wako kukabiliana na masuala yaliyo tata. Kwa  upande mwingine uwezo huo unaweza kutokeza tatizo. Unaweza kumfanya kijana wako ashindane nawe.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Ikiwezekana, zungumza naye isivyo rasmi. Tumia vizuri pindi zisizo rasmi. Kwa mfano, wazazi fulani wamegundua kwamba inakuwa rahisi zaidi kwa matineja kujieleza wanapofanya kazi au wanaposafiri ndani ya gari, kwa kuwa wakati huo wanakuwa kando ya wazazi wao badala ya kutazamana uso kwa uso.—Kanuni ya Biblia: Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.

Fanya mazungumzo yawe mafupi. Hakuna haja ya kubishania kila jambo mpaka mwisho. Badala yake, toa hoja yako . . . kisha utulie. Kijana wako atauelewa vizuri ujumbe wako baadaye, wakati anapokuwa peke yake na kutafakari mambo uliyosema. Mpe nafasi ya kufanya hivyo.—Kanuni ya Biblia: Methali 1:1-4.

Sikiliza—na uwe mwenye kubadilikana. Sikiliza kwa makini—bila kukatiza—ili upate picha kamili ya tatizo. Unapojibu, uwe na usawaziko. Ikiwa unashikilia sheria kupita kiasi, kijana wako atatafuta njia za kutozitii bila kuadhibiwa. “Wakati huo ndipo watoto huishi maisha maradufu,” kinaonya kitabu Staying Connected to Your Teenager. “Pindi moja wanawaambia wazazi wao kile wazazi wanachotaka kusikia na pindi nyingine wanafanya mambo kama wapendavyo mara tu wanapokuwa mbali na wazazi wao.”—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 4:5.

Uwe mtulivu. “Tusipokubaliana kuhusu jambo fulani, mama yangu hukasirishwa na kila kitu ninachosema” anasema tineja anayeitwa Kari. “Hali hiyo hunikasirisha, na haraka mazungumzo yetu hugeuka kuwa mabishano.” Badala ya kukasirika kupita kiasi, sema jambo fulani linaloonyesha kwamba unaelewa jinsi kijana wako anavyohisi. Kwa mfano, badala ya kusema “Hilo ni jambo dogo tu!” sema, “Naona jambo hili linakuhangaisha sana.”—Kanuni ya Biblia: Methali 10:19.

Kwa kadiri inavyowezekana, mshauri kijana wako, usimfanyie maamuzi. Uwezo wa kuchanganua mambo wa kijana wako ni kama misuli inayohitaji kuzoezwa. Kwa hiyo, anapokabili tatizo, badala ya kumfanyia uamuzi, mwache yeye mwenyewe ajifanyie uamuzi. Mnapojadili jambo fulani, mpe nafasi ya kueleza njia ambazo angetumia kusuluhisha jambo hilo. Halafu, baada ya kuzungumzia njia mbalimbali, unaweza kusema: “Hizo ni baadhi ya njia unazoweza kutumia. Zifikirie kwa siku moja au mbili, kisha tukutane tena ili tuzungumzie ni suluhisho gani unalopendekeza na kwa nini.”— Kanuni ya Biblia: Waebrania 5:14.

^ fu. 7 Majina katika makala hii yamebadilishwa.