Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Jinsi ya Kuepuka Kushinikizwa na Marafiki

Jinsi ya Kuepuka Kushinikizwa na Marafiki

KIKWAZO

“Nilipokuwa shuleni sikupendwa na watoto wengine, na hilo liliniumiza. Hivyo nilipoingia shule ya sekondari, nilibadili mtindo wangu wa mavazi na mtazamo wangu—na sikufanya hivyo kwa nia nzuri. Nilitamani sana kupata marafiki hivi kwamba nilikubali kushinikizwa ili tu wanafunzi wenzangu wanipende.”—Jennifer, miaka 16. *

Je, unashinikizwa na marafiki? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kukabiliana na hali hiyo.

Unapokubali kushinikizwa na marafiki, unakuwa kama roboti isiyo na akili kwa sababu unawaruhusu wengine wakuongoze. Hupaswi kuwaruhusu wafanye hivyo.—Waroma 6:16.

JAMBO UNALOPASWA KUJUA

Kushinikizwa na marafiki kunaweza kufanya watu wazuri wafanye mambo mabaya.

“Mashirika mabaya huharibu tabia nzuri.”—1 Wakorintho 15:33.

“Tunajua tabia fulani ni mbaya, lakini tunapokabiliwa na hali hiyo, tunashindwa na hisia zetu na kutaka kuwafurahisha wengine!”—Dana.

Tunaweza kujishinikiza sisi wenyewe.

“Ninapotaka kufanya yaliyo sawa, yaliyo mabaya yapo pamoja nami.”—Waroma 7:21.

“Mimi ndiye ninayejishinikiza; kwa kweli, ninatamani kufanya mambo ambayo marafiki wangu wanazungumzia na kuyafanya yaonekane kuwa yenye kusisimua.”—Diana.

Kushinda shinikizo la marafiki ni jambo la kujivunia.

“Iweni na dhamiri njema.”—1 Petro 3:16.

“Pindi fulani ilikuwa vigumu sana kwangu kukataa kushinikizwa na marafiki, lakini sasa siogopi kuwa tofauti na ninafanya maamuzi thabiti. Hakuna jambo linalofurahisha kama kulala nikiwa na dhamiri safi.”—Carla.

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Ukishinikizwa kufanya mambo mabaya, jaribu mambo yafuatayo:

Fikiria matokeo. Jiulize hivi, ‘Namna gani nikikubali kushinikizwa kisha jambo hilo lijulikane? Wazazi wangu watanionaje? Nitajionaje?’—Kanuni ya Biblia: Wagalatia 6:7.

“Wazazi wangu huniuliza maswali kama vile, ‘Ukikubali kushinikizwa ni nini kinachoweza kukupata?’ Wao hunisaidia kuona jinsi kushinikizwa kunavyoweza kuathiri wakati wangu ujao.”—Olivia.

Imarisha msimamo wako. Jiulize, ‘Kwa nini ninaamini kwamba jambo hili linaweza kunidhuru mimi au wengine?’—Kanuni ya Biblia: Waebrania 5:14.

“Nilipokuwa mchanga, ningekataa au kutoa jibu fupi, lakini sasa ninaweza kueleza kwa nini nitafanya au sitafanya jambo fulani. Nina msimamo thabiti kuhusu mambo ninayoamini kuwa mema au mabaya. Ninajibu kulingana na usadikisho wangu, si wa mtu mwingine.”—Anita.

Fikiria sifa yako. Jiulize, ‘Ninataka kuwa mtu wa aina gani?’ Kisha fikiria shinikizo unalokabili na ujiulize, ‘Mtu wa aina hiyo angefanya nini katika hali hii?’—Kanuni ya Biblia: 2 Wakorintho 13:5.

“Nimeridhika na jinsi nilivyo, na hivyo sihangaikii jinsi wengine wanavyoniona. Isitoshe, watu wengi hunipenda jinsi nilivyo.”—Alicia.

Fikiria wakati ujao. Ikiwa uko shuleni, baada ya miaka au hata miezi michache, watu unaojaribu kuwafurahisha hawatakuwa pamoja nawe.

“Niliangalia picha niliyopigwa pamoja na wanafunzi wenzangu na hata sikukumbuka baadhi ya majina yao. Lakini nilipokuwa shuleni, maoni yao yalikuwa muhimu sana kwangu kuliko mambo niliyoamini. Huo ulikuwa upumbavu kama nini!”—Dawn, sasa ana miaka 22.

Jitayarishe. Biblia inasema: “Mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.”—Wakolosai 4:6.

“Wazazi wetu hutusaidia mimi na dada yangu kufikiria hali mbalimbali zinazoweza kutokea, kisha tunaziigiza ili tujue jinsi ya kukabiliana nazo.”—Christine.

^ fu. 4 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.