Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | KULEA WATOTO

Binti Yako Anapokuwa na Mkazo

Binti Yako Anapokuwa na Mkazo

KIKWAZO

Binti yako anasema ana mkazo. Unajiuliza hivi kwa mshangao: ‘Mtoto wa umri wa miaka 13 anawezaje kuwa na mkazo? Sidhani anajua mkazo ni nini!’ Kabla hujamwambia binti yako hivyo, hebu fikiria kwa nini anaweza kuhisi kwamba analemewa na maisha.

KWA NINI HILI HUTUKIA

Mabadiliko ya kimwili. Kukua kwa haraka kunakotokea wakati wa kubalehe kunaweza kumfanya msichana awe na mkazo sana, hasa ikiwa amechelewa kukua au amewatangulia wasichana wenzake. Anna, * ambaye sasa ana umri wa miaka 20 anasema hivi: “Nilikuwa kati ya wasichana wa kwanza kuvaa sidiria, na niliona haya sana. Nilipojilinganisha na wasichana wengine, nilijiona kana kwamba nina kasoro fulani.”

Mabadiliko ya kihisia. Karen, ambaye sasa ana umri wa miaka 17, anakumbuka hivi: “Nilichanganyikiwa, sikuelewa kwa nini nilikuwa na furaha mchana na usiku ulipofika nililia sana. Sikujua nilikuwa na tatizo gani. Nilishindwa kabisa kudhibiti hisia zangu.”

Kuanza kupata hedhi. Msichana anayeitwa Kathleen anasema: “Nilipopata hedhi kwa mara ya kwanza nilishtuka sana ingawa mama yangu alikuwa ameniambia mengi kuhusu kipindi hicho. Nilioga mara nyingi kwa siku kwa sababu nilijihisi mchafu wakati wote. Na pia, kaka zangu watatu walinitania sana bila huruma. Walidhani kwamba kupata hedhi ni jambo la kuchekesha.”

Kushinikizwa na marafiki. Maria, ambaye sasa ana umri wa miaka 18, anakumbuka hivi: “Nilipokuwa na umri wa kati ya miaka 12 na 14, marafiki wangu walinishinikiza sana. Wanafunzi wenzangu walimchokoza yeyote aliyekuwa tofauti nao.” Anita mwenye umri wa miaka 14 anasema:  “Vijana wengi hutaka sana kukubaliwa na marafiki wao, na inaumiza sana unapotengwa.”

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Mtie moyo binti yako azungumzie mkazo anaokabili. Mwanzoni, anaweza kusita kuzungumzia jambo hilo. Lakini uwe mvumilivu na ufuate ushauri huu wa Biblia: Uwe “mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema.”—Yakobo 1:19.

Usipuuze mkazo anaopata binti yako. Kumbuka, hana uzoefu kama wewe kwa kuwa hajapitia mikazo maishani, hivyo hana ujuzi wa kumwezesha kushughulika nayo.—Kanuni ya Biblia: Waroma 15:1.

Usimpangie binti yako mambo mengi ya kufanya. Kulingana na kitabu kimoja kuhusu watoto, (Teach Your Children Well) vijana ambao wana mambo mengi sana ya kufanya “mara nyingi huonyesha dalili za mkazo, kama vile maumivu ya kichwa na tumbo.”—Kanuni ya Biblia: Wafilipi 1:9, 10.

Hakikisha binti yako anapumzika vya kutosha. Mara nyingi vijana hawalali vya kutosha. Binti yako asipolala vya kutosha, uwezo wake wa kufikiri utapungua na hivyo hataweza kukabiliana na mikazo.—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 4:6.

Msaidie binti yako ajue jinsi ya kukabiliana na mkazo. Kwa wasichana wengi, mazoezi hupunguza mkazo. Biblia inasema kwamba “mazoezi ya kimwili ni yenye faida.” (1 Timotheo 4:8) Wasichana wengine huona kwamba wanapoandika hisia zao kwenye kitabu, hilo huwasaidia kukabiliana na mkazo. Brittany ambaye sasa ana umri wa miaka 22 anasema hivi: “Nilipokuwa mdogo niliandika matatizo ambayo yalinilemea. Hilo lilinisaidia kuwa na mtazamo unaofaa na lilifanya iwe rahisi kuyasuluhisha au kutoyakazia fikira.”

Mwekee mfano. Wewe hukabilianaje na mkazo? Je, wewe hufanya mambo mengi kuliko uwezo wako kisha unapatwa na wasiwasi usipofaulu? Je, wewe hufanya kazi kupita kiasi hivi kwamba unakosa nafasi ya kufanya mambo yaliyo muhimu zaidi? “Usawaziko wenu na ujulikane kwa watu wote,” inasema Wafilipi 4:5. Kumbuka binti yako atajifunza kutokana na mfano unaomwekea iwe ni mzuri au mbaya. [Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Majina katika makala hii yamebadilishwa.