Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Mtu Unayempenda Anapokufa

Mtu Unayempenda Anapokufa

“Mwanangu,. . . usilie. Kazi ya Mungu haina makosa.”

Mwanamke anayeitwa Bebe aliambiwa maneno hayo, siku ya mazishi ya baba yake aliyekufa kutokana na aksidenti ya gari.

Bebe alimpenda sana baba yake. Maneno hayo aliyoambiwa na rafiki wa familia mwenye nia nzuri, yalimuumiza sana badala ya kumfariji. Bebe aliendelea kujiambia, “baba hakupaswa kufa.” Kuonyesha kwamba bado alikuwa na huzuni, miaka mingi baadaye Bebe alisimulia tukio hilo katika kitabu chake.

Sawa na Bebe, wengi wanakubali kwamba huzuni ya kufiwa haiishi haraka, hasa ikiwa aliyekufa alikuwa mtu wa karibu sana. Biblia inasema kifo ni “adui wa mwisho.” (1 Wakorintho 15:26) Kifo huharibu maisha yetu na hakizuiliki. Hakuna yeyote kati yenu anayeweza kuepuka madhara ya kifo. Hivyo, haishangazi kwamba tunapopatwa na msiba mara nyingi tunashindwa kukabiliana na hali hiyo.

Huenda ukajiuliza: ‘Huzuni ya kufiwa huisha baada ya muda gani? Mtu anawezaje kukabiliana na huzuni hiyo? Ninaweza kuwafariji jinsi gani wale waliofiwa? Je, kuna tumaini lolote kwa wapendwa wetu waliokufa?