Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kuwa Mtu Mwema Kutakuhakikishia Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Je, Kuwa Mtu Mwema Kutakuhakikishia Maisha Bora ya Wakati Ujao?

Kwa karne nyingi, watu wengi wamehisi kwamba wakiwa watu wema na wenye maadili mazuri watakuwa na maisha bora ya wakati ujao. Kwa mfano, watu wa Mashariki waliheshimu sana maneno haya ambayo mwanafalsafa na mwalimu aliyeitwa Confucius (551-479 K.W.K.) alisema: “Jambo ambalo hutaki wengine wakutendee, usiwatendee.” *

NJIA INAYOFUATWA NA WATU WENGI

Bado watu wengi waamini kwamba kuwa na tabia njema ndiyo siri ya kupata mafanikio ya wakati ujao. Wanajitahidi kuwa na heshima, tabia nzuri, kutambua wajibu wao katika jamii, na kudumisha dhamiri njema. Linh, mwanamke anayeishi Vietnam anasema: “Sikuzote niliamini kwamba ikiwa ningekuwa msema kweli na mnyoofu, ningepata baraka.”

Baadhi ya watu wanajitahidi kufanya mema kwa sababu ya imani zao za kidini. Mwanamume anayeitwa Hsu-Yun, anayeishi Taiwan, anasema, “Nilifundishwa kwamba matendo ya mtu anapokuwa hai yanaamua ikiwa atapata raha milele au atateseka motoni milele atakapokufa.”

MATOKEO NI NINI?

Ni kweli kwamba tunapata faida nyingi kwa kuwatendea wengine mema. Hata hivyo, watu wengi ambao kwa unyoofu wanajitahidi kuwatendea wengine mema, wanatambua kwamba mara nyingi hawapati matokeo waliyotarajia. Shiu Ping, mwanamke anayeishi Hong Kong anasema: “Nimejionea mwenyewe kwamba si wakati wote wale wanaowatendea wengine mema wanapata maisha bora kama walivyotarajia. Nilijitahidi sana kuitunza familia yangu na kufanya mambo mazuri. Lakini, ndoa yangu ilivunjika na mume wangu alitutelekeza mimi na mtoto wangu.”

Watu wengi wamejionea kwamba, si kila mara dini zinawasaidia watu kuwa wema. Etsuko, mwanamke kutoka Japani anasema hivi; “Nilijiunga na shirika fulani la dini, na kisha nikawa msimamizi wa shughuli za vijana. Nilishangazwa kuona washiriki wa dini yangu wakiwa na maadili mabaya, wakigombania vyeo, na kutumia vibaya pesa za kanisa.”

“Nilijitahidi sana kuitunza familia yangu na kufanya mambo mazuri. Lakini ndoa yangu ilivunjika na mume wangu alitutelekeza mimi na mtoto wangu.”​—SHIU PING, HONG KONG

Baadhi ya watu wamevunjika moyo kwa sababu wamepatwa na mambo mabaya licha ya kushika dini na kutenda mema. Hivyo ndivyo Van, mwanamke kutoka Vietnam, alivyohisi. Anasema hivi; “Kila siku nilinunua matunda, maua, na chakula na kuvitoa sadaka kwa mababu waliokufa nikitumaini kwamba nitapata baraka. Licha ya kufanya mema na kufuata desturi za kidini kwa miaka mingi, mume wangu alipatwa na ugonjwa mbaya sana. Kisha binti yangu aliyekuwa akisoma nje ya nchi akafa akiwa na umri wa miaka 20 tu.”

Ikiwa kuwa mtu mwema hakutuhakikishii maisha bora ya wakati ujao, ni nini kinachoweza kutupatia uhakika huo? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji mwongozo wenye kutegemeka kabisa—chanzo cha habari kinachoweza kutupa majibu ya maswali yetu na kutuelekeza kwenye maisha bora ya wakati ujao. Tunaweza kupata wapi mwongozo huo?

^ fu. 2 Kwa maelezo zaidi kuhusu mambo ambayo Confucius alifundisha, tazama sura ya 7, fungu la 31-35, la kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova na ambacho kinapatikana mtandaoni kwenye www.dan124.com/sw.