Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | MALAIKA​—JE, WANAHUSIKA KATIKA MAISHA YAKO?

Je, Kuna Malaika Waovu?

Je, Kuna Malaika Waovu?

Ndiyo, wapo malaika waovu. Walitoka wapi? Kumbuka kwamba Mungu aliwaumba malaika wakiwa na zawadi ya uhuru wa kuchagua. Muda mfupi baada ya mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa, kuumbwa, kiumbe mkamilifu wa roho alitumia vibaya zawadi yake ya uhuru wa kuchagua na kuanzisha uasi duniani. Alifanikiwa kuwashawishi Adamu na Hawa wamwasi Mungu. (Mwanzo 3:1-7; Ufunuo 12:9) Biblia haitaji malaika huyo aliitwa nani au alikuwa na cheo gani mbinguni kabla ya kuasi. Lakini baada ya kuasi, kwa kufaa Biblia inamwita Shetani, jina linalomaanisha “Mpinzani,” na Ibilisi, linalomaanisha “Mchongezi.”—Mathayo 4:8-11.

Kwa kusikitisha, uasi huo dhidi ya Mungu haukuishia hapo. Katika siku za Noa, malaika fulani ambao idadi yao haitajwi, “hawakubaki mahali pao pa kwanza” katika familia ya Mungu mbinguni. Walikuja dunia na kujivika miili ya kibinadamu ili kufuatilia ukosefu wa maadili, kinyume cha kusudi la Mungu la kuwaumba.—Yuda 6; Mwanzo 6:1-4; 1 Petro 3:19, 20.

Ni nini kilichowapata malaika hao waovu? Mungu alipoleta gharika ili kuisafisha dunia yote, malaika hao walibadili miili yao na kurudi katika makao ya roho. Hata hivyo, Mungu hakuwaruhusu waasi hao warudi “mahali pao pa kwanza.” Badala yake, aliwaweka katika hali ya “giza zito” la kiroho, inayoitwa Tartaro. (Yuda 6; 2 Petro 2:4) Roho hao waovu wamejitiisha kwa Shetani Ibilisi, “mtawala wa roho waovu,” ambaye “huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.”—Mathayo 12:24; 2 Wakorintho 11:14.

Biblia inafundisha kwamba Ufalme wa Mungu wa Kimasihi, serikali ya mbinguni, ulisimamishwa mwaka wa 1914. * Kufuatia tukio hilo muhimu, Shetani na malaika zake walifukuzwa mbinguni na kutupwa duniani, wakiwa wamenyimwa uwezo wa kufanya baadhi ya mambo. Uovu mwingi na upotovu wa maadili katika ngono uliopo duniani ni uthibitisho wa hasira na uvutano wao mbaya.—Ufunuo 12:9-12.

Hata hivyo, kuongezeka kwa upotovu wa maadili na uovu wenye kushtua ni uthibitisho wa kwamba mwisho wa utawala wao mwovu uko karibu. Hivi karibuni, viumbe hao waovu wataondolewa. Baada ya Ufalme wa Mungu kuitawala dunia itakayokuwa paradiso kwa miaka 1,000, viumbe hao waovu watakuwa na muda mfupi wa kuwajaribu wanadamu kwa mara ya mwisho. Kisha, wataharibiwa milele.—Mathayo 25:41; Ufunuo 20:1-3, 7-10.

^ fu. 6 Ili upate habari zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu, soma sura ya 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia, kinapatikana kwenye www.dan124.com/sw.