Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Shangilia Pamoja na Mke wa Ujana Wako’

‘Shangilia Pamoja na Mke wa Ujana Wako’

‘Shangilia Pamoja na Mke wa Ujana Wako’

“Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako . . . Mwanangu, kwa nini umfurahie mwanamke mgeni?”—METHALI 5:18, 20.

1, 2. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba upendo wa kimahaba kati ya mume na mke wake umebarikiwa?

BIBLIA inazungumza waziwazi kuhusu mambo ya ngono. Tunasoma hivi kwenye Methali 5:18, 19: “Chemchemi yako ya maji na ibarikiwe, na ushangilie pamoja na mke wa ujana wako, paa mwenye kupendeka na mbuzi wa milimani mwenye kuvutia. Na maziwa yake yakuleweshe nyakati zote. Upendo wake na ukufurahishe sikuzote.”

2 Katika andiko hilo neno “chemchemi” linamaanisha kile kinachompa mtu uradhi katika ngono. Chemchemi hiyo imebarikiwa katika maana ya kwamba upendo wa kimahaba na furaha ambayo wenzi wa ndoa wanapata ni zawadi kutoka kwa Mungu. Hata hivyo, uhusiano huo wa karibu unapaswa kufurahiwa tu katika ndoa. Hivyo, Mfalme Sulemani wa Israeli la kale ambaye ni mwandikaji wa Methali anauliza hivi: “Mwanangu, kwa nini umfurahie mwanamke mgeni au kukumbatia kifua cha mwanamke wa kigeni?”—Methali 5:20.

3. (a) Ndoa nyingi zimekumbwa na hali gani yenye kusikitisha? (b) Mungu anaonaje uzinzi?

3 Katika siku yao ya arusi, mwanamume na mwanamke huweka nadhiri nzito kwamba watapendana na kuendelea kuwa waaminifu katika ndoa. Hata hivyo, ndoa nyingi zinavunjika kwa sababu ya uzinzi. Baada ya kuchanganua matokeo 25 ya uchunguzi, mtafiti mmoja alikata kauli kwamba “asilimia 25 ya wake na asilimia 44 ya waume wamewahi kufanya ngono nje ya ndoa.” Mtume Paulo alisema hivi: “Msipotoshwe. Wala waasherati, wala waabudu-sanamu, wala wazinzi, wala wanaume wanaowekwa kwa ajili ya makusudi yasiyo ya asili, wala wanaume wanaolala na wanaume, . . . hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 6:9, 10) Hakuna shaka kuhusu jambo hilo. Uzinzi ni dhambi nzito machoni pa Mungu, na ni lazima waabudu wa kweli wajihadhari wasifanye ngono nje ya ndoa. Ni nini kitakachotusaidia ‘kuheshimu ndoa na kuweka kitanda cha ndoa kuwa bila unajisi’?—Waebrania 13:4.

Jihadhari na Moyo Wenye Hila

4. Ni katika njia gani Mkristo aliyefunga ndoa anaweza kuingia katika uhusiano wa kimahaba bila kujua?

4 Katika ulimwengu wa leo wenye maadili yaliyopotoka, watu wengi “wana macho yenye kujaa uzinzi na yasiyoweza kuachana na dhambi.” (2 Petro 2:14) Wao huanzisha uhusiano wa kimahaba nje ya ndoa kimakusudi. Katika nchi fulani wanawake wengi wameajiriwa, na kwa sababu wanafanya kazi pamoja na wanaume, hilo limechangia sana kusitawi kwa mahusiano yasiyofaa ya kimahaba katika mahali pa kazi. Pia, vituo vya mawasiliano kwenye Intaneti vimefanya iwe rahisi hata kwa watu waoga sana kuanzisha urafiki wa karibu kwenye mtandao. Watu wengi waliofunga ndoa huangukia mitego hiyo bila kujua kwamba wanaathiriwa.

5, 6. Mwanamke mmoja Mkristo aliingiaje katika hali hatari, nasi tunajifunza nini kutokana na hilo?

5 Fikiria jinsi Mkristo tutakayemwita Mary alivyojipata katika hali ambayo karibu sana imwongoze kwenye ukosefu wa adili katika ngono. Mume wake, ambaye si Shahidi wa Yehova, hakuonyesha kwamba anaipenda sana familia yake. Mary anakumbuka wakati fulani miaka iliyopita alipokutana na mtu aliyefanya kazi na mume wake. Mtu huyo alikuwa mwenye adabu, na hata baadaye alionyesha kuwa anapendezwa na mambo ambayo Mary anaamini. Mary anasema hivi: “Mtu huyo alikuwa mzuri sana, tofauti sana na mume wangu.” Muda si muda, Mary na mtu huyo wakawa na uhusiano wa kimahaba. Mary aliwaza hivi: “Sijafanya uzinzi, na mtu huyo anapendezwa na Biblia. Labda ninaweza kumsaidia.”

6 Kabla uhusiano wake wa kimahaba haujamwongoza kwenye uzinzi, Mary alirudiwa na fahamu zake. (Wagalatia 5:19-21; Waefeso 4:19) Dhamiri yake ilianza kufanya kazi, naye akarekebisha hali hiyo. Kisa cha Mary kinaonyesha kwamba “moyo ni wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yeremia 17:9) Biblia inatushauri hivi: “Linda moyo wako kuliko vitu vingine vyote vinavyopaswa kulindwa.” (Methali 4:23) Tunaweza kufanyaje hivyo?

‘Mtu Mwerevu Hujificha’

7. Unapomsaidia mtu mwenye matatizo ya ndoa, ni mashauri gani ya Maandiko yanayoweza kukulinda?

7 Mtume Paulo aliandika hivi: “Yeye anayefikiri kuwa amesimama na ajihadhari kwamba asianguke.” (1 Wakorintho 10:12) Na andiko la Methali 22:3 linasema hivi: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.” Badala ya kujiamini kupita kiasi na kufikiri, ‘Siwezi kuumia,’ ni jambo la hekima kuona kimbele hali ambazo zinaweza kusababisha matatizo. Kwa mfano, usikubali mtu wa jinsia tofauti anayekabili matatizo makubwa katika ndoa awe akikufunulia matatizo hayo wewe peke yako. (Methali 11:14) Mwambie mtu huyo kwamba anafaa kuzungumzia matatizo ya ndoa pamoja na mwenzi wake, pamoja na Mkristo mkomavu wa jinsia yake ambaye anataka ndoa hiyo ifanikiwe, au pamoja na wazee. (Tito 2:3, 4) Wazee katika makutaniko ya Mashahidi wa Yehova huweka kielelezo kizuri kuhusu jambo hilo. Mzee anapohitaji kuzungumza faraghani pamoja na dada Mkristo, yeye hufanya hivyo mahali penye watu, kama vile kwenye Jumba la Ufalme.

8. Unapaswa kujihadhari na mambo gani kazini?

8 Unapokuwa kazini na kwingineko, jihadhari na hali zinazoweza kufanya uwe na uhusiano wa karibu pamoja na mtu wa jinsia tofauti. Kwa mfano, kufanya kazi kwa ukaribu pamoja na mtu wa jinsia tofauti baada ya saa za kazi kunaweza kutokeza kishawishi. Ikiwa wewe ni mwanamume au mwanamke aliyefunga ndoa, unapaswa kuonyesha waziwazi kwa maneno na matendo kwamba hutaki kuwa na uhusiano wa kimahaba isipokuwa na mwenzi wako. Kwa kuwa unafuatia ujitoaji-kimungu, bila shaka hungependa kuwavutia watu kwa kucheza-cheza nao kimapenzi au kwa kuvalia na kujipamba kwa njia isiyofaa. (1 Timotheo 4:8; 6:11; 1 Petro 3:3, 4) Kuweka picha za mwenzi wako wa ndoa na za watoto wako mahali pa kazi kutakukumbusha na kuwakumbusha wengine kwamba unaipenda familia yako. Azimia kutochochea wala kuruhusu vishawishi vya uhusiano wa kimahaba.—Ayubu 31:1.

“Furahia Maisha Pamoja na Mke Unayempenda”

9. Ni matukio gani yenye kufuatana ambayo yanaweza kumfanya mtu avutiwe na uhusiano mpya wa kimahaba?

9 Kulinda moyo kunatia ndani mengi zaidi ya kuepuka hali hatari. Kupendezwa kimahaba na mtu nje ya ndoa kunaweza kuonyesha kwamba mume au mke anapuuza mahitaji ya mwenzi wake. Huenda ikawa mke anapuuzwa tena na tena au mume anachambuliwa kila wakati. Kwa ghafula, mtu mwingine, iwe kazini au hata katika kutaniko la Kikristo, anaonekana kuwa na sifa zilezile ambazo mwenzi wa ndoa amekosa. Muda si muda, wanakuwa marafiki wa karibu, na uhusiano huo mpya unavutia sana. Matukio hayo yanayofuatana na yanayotokea bila mtu kutambua yanaonyesha ukweli wa maneno haya ya Biblia: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe.”—Yakobo 1:14.

10. Waume na wake wanaweza kuimarishaje uhusiano wao?

10 Badala ya kwenda nje ya ndoa ili kutosheleza tamaa zao, ziwe za kupendwa, za urafiki, au za kutegemezwa wakati wa hali ngumu, waume na wake wanapaswa kujitahidi kuimarisha uhusiano wao wenye upendo pamoja na wenzi wao. Basi, tumieni wakati pamoja, na mfanye uhusiano wenu uwe wa karibu zaidi na zaidi. Fikirieni kilichowafanya mpendane. Jaribu kuwa na shauku uliyokuwa nayo hapo kwanza kumwelekea mwenzi wako. Fikiria nyakati nzuri ambazo mmefurahia pamoja. Sali kwa Mungu kuhusu jambo hilo. Mtunga-zaburi Daudi alimsihi Yehova hivi: “Uumbe moyo safi ndani yangu, Ee Mungu, na kuweka ndani yangu roho mpya, iliyo imara.” (Zaburi 51:10) Azimia ‘kufurahia maisha pamoja na mke unayempenda siku zote za maisha yako ambayo umepewa na Mungu chini ya jua.’—Mhubiri 9:9.

11. Ujuzi, hekima, na utambuzi huimarishaje uhusiano wa ndoa?

11 Ujuzi, hekima, na utambuzi ni sifa ambazo hazipaswi kupuuzwa wakati watu wanapoimarisha uhusiano wa ndoa. Andiko la Methali 24:3, 4 linasema hivi: “Nyumba hujengwa kwa hekima, na kwa utambuzi itasimamishwa imara. Na kwa ujuzi vyumba vya ndani vitajazwa vitu vyote vyenye thamani na vyenye kupendeza.” Upendo, ushikamanifu, kumwogopa Mungu, na imani ni baadhi ya vitu vyenye thamani vinavyoijaza nyumba yenye furaha. Mtu anahitaji kumjua Mungu ili awe na sifa hizo. Basi, wenzi wa ndoa wanapaswa kujifunza Biblia kwa bidii. Na hekima na utambuzi ni muhimu kadiri gani? Kukabiliana na matatizo ya kila siku kunahitaji hekima, yaani, uwezo wa kutumia ujuzi wa Maandiko. Mtu mwenye utambuzi anaweza kuelewa mawazo na hisia za mwenzi wake. (Methali 20:5) Kupitia Sulemani, Yehova anasema hivi: “Mwanangu, sikiliza hekima yangu. Tega sikio usikie utambuzi wangu.”—Methali 5:1.

Kunapokuwa na “Dhiki”

12. Kwa nini haishangazi kwamba wenzi wa ndoa hupatwa na matatizo?

12 Hakuna ndoa kamilifu. Hata Biblia inasema kwamba waume na wake watakuwa na “dhiki katika mwili wao.” (1 Wakorintho 7:28) Mahangaiko, magonjwa, mateso, na mambo mengine yanaweza kusababisha mkazo katika ndoa. Hata hivyo, matatizo yanapotokea mnahitaji kutafuta masuluhisho pamoja mkiwa wenzi wa ndoa washikamanifu wanaojitahidi kumpendeza Yehova.

13. Mume na mke wanaweza kujichunguza kuhusiana na mambo gani?

13 Namna gani ndoa ikikabiliwa na mkazo kwa sababu ya vile wenzi wanavyotendeana? Jitihada zinahitajiwa ili kupata suluhisho. Tuseme wenzi wa ndoa walianza kuzungumziana kwa maneno yasiyo ya fadhili, na sasa wamezoea kufanya hivyo. (Methali 12:18) Kama ilivyozungumziwa katika makala iliyotangulia, hilo linaweza kuwa na matokeo mabaya. Methali moja ya Biblia inasema hivi: “Ni afadhali kukaa nyikani kuliko kukaa pamoja na mke mgomvi pamoja na uchokozi.” (Methali 21:19) Ikiwa wewe ni mke katika ndoa ya aina hiyo, jiulize hivi: ‘Je, mtazamo wangu unafanya iwe vigumu kwa mume wangu kuwa pamoja nami?’ Biblia inawaambia waume hivi: “Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Wakolosai 3:19) Ikiwa wewe ni mume, jiulize hivi: ‘Je, nimekosa huruma na hivyo kumshawishi mke wangu kutafuta faraja mahali pengine?’ Bila shaka, hakuna kisingizio cha kufanya uzinzi. Hata hivyo, kwa kuwa msiba huo unaweza kutokea, hiyo ni sababu nzuri ya kuzungumzia matatizo waziwazi.

14, 15. Kwa nini kwenda nje ya ndoa hakusuluhishi matatizo ya ndoa?

14 Kutafuta faraja katika uhusiano wa kimahaba nje ya ndoa hakusuluhishi matatizo ya ndoa. Uhusiano kama huo unaweza kuwa na matokeo gani? Je, utatokeza ndoa mpya na iliyo bora zaidi? Huenda wengine wakafikiri hivyo. Huenda wakasema, ‘Mtu huyu ana sifa zilezile ambazo ningependa mwenzi wangu wa ndoa awe nazo.’ Lakini huko ni kujidanganya, kwa kuwa mtu yeyote ambaye anaweza kumwacha mwenzi wake, au kukuhimiza umwache mwenzi wako, anadharau sana utakatifu wa ndoa. Ni jambo lisilo la akili kutarajia uhusiano huo utokeze ndoa bora zaidi.

15 Mary, aliyetajwa mapema, alifikiria kwa uzito matokeo ya mwenendo wake, kutia ndani uwezekano wa yeye au mtu mwingine kupoteza kibali cha Mungu. (Wagalatia 6:7) Anasema hivi: “Nilipoanza kuchunguza jinsi nilivyohisi kuhusu mtu huyo aliyefanya kazi pamoja na mume wangu, nilitambua kwamba huenda mwenendo wangu ungemzuia mtu huyo asijifunze ukweli siku moja. Kutenda dhambi kungemwathiri kila mtu aliyehusika na kuwakwaza wengine!”—2 Wakorintho 6:3.

Kichocheo Kikubwa Zaidi

16. Taja baadhi ya matokeo ya ukosefu wa adili.

16 Biblia inaonya hivi: “Midomo ya mwanamke mgeni hudondoka-dondoka kama sega la asali, nalo kaakaa lake ni laini kuliko mafuta. Lakini matokeo yake ni machungu kama pakanga; ni makali kama upanga wenye makali kuwili.” (Methali 5:3, 4) Matokeo ya ukosefu wa adili ni machungu na yanaweza kuwa hatari sana. Yanatia ndani kusumbuliwa na dhamiri, magonjwa ya zinaa, na kumuumiza kihisia mwenzi wa ndoa wa mtu asiye mwaminifu. Bila shaka, hiyo ni sababu ya kutoanza jambo lolote ambalo linaweza kumfanya mtu asiwe mwaminifu kwa mwenzi wake.

17. Taja sababu kubwa zaidi ya kuendelea kuwa waaminifu katika ndoa.

17 Sababu kuu inayofanya uzinzi uwe kosa ni kwamba unashutumiwa na Yehova, ambaye alianzisha mpango wa ndoa na kuwapa wanadamu uwezo wa kufanya ngono. Yehova anasema hivi kupitia nabii Malaki: “Nitawakaribia ninyi ili kuhukumu, nami nitakuwa shahidi wa haraka juu ya . . . wazinzi.” (Malaki 3:5) Andiko la Methali 5:21 linasema hivi kuhusu mambo ambayo Yehova anaona: “Njia za mwanadamu ziko mbele za macho ya Yehova, naye anayatafakari mapito yake yote.” Naam, “vitu vyote viko uchi navyo vimefunuliwa wazi machoni pake yeye ambaye tunatoa hesabu kwake.” (Waebrania 4:13) Basi, kichocheo kikubwa zaidi cha kuendelea kuwa waaminifu katika ndoa ni kutambua kwamba hata mtu akificha uzinzi kadiri gani na matokeo yake ya kimwili au ya kijamii yaonekane kuwa madogo kadiri gani, tendo lolote la uchafu wa kingono huharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova.

18, 19. Tunajifunza nini kutokana na kisa cha Yosefu na mke wa Potifa?

18 Kielelezo cha Yosefu, mwana wa yule mzee wa ukoo Yakobo, kinaonyesha kwamba tamaa ya kuwa na amani pamoja na Mungu ni kichocheo chenye nguvu. Baada ya kupata kibali machoni pa Potifa, ofisa wa makao ya Farao, Yosefu alipata cheo kikubwa katika nyumba ya Potifa. Pia, Yosefu alikuwa “mwenye umbo zuri na mwenye sura ya kupendeza,” na mke wa Potifa alivutiwa na mambo hayo. Kila siku, alijaribu kumshawishi Yosefu, lakini hakufanikiwa. Ni jambo gani lililomwezesha Yosefu kukataa vishawishi vyake vyote? Biblia inatuambia hivi: “Akawa akikataa, naye alikuwa akimwambia mke wa bwana wake: ‘Tazama bwana wangu . . . hakunizuilia chochote ila wewe, kwa sababu wewe ni mke wake. Basi ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?’”—Mwanzo 39:1-12.

19 Yosefu, aliyekuwa mseja, alidumisha usafi wa maadili kwa kukataa kufanya ngono pamoja na mke wa mtu mwingine. Andiko la Methali 5:15 linawaambia hivi wanaume waliooa: “Unywe maji ya birika lako mwenyewe, na maji yanayotiririka kutoka katikati ya kisima chako mwenyewe.” Jihadhari dhidi ya kusitawisha uhusiano wa kimahaba nje ya ndoa hata bila kujua. Jitahidi kuimarisha upendo katika ndoa yako na kusuluhisha matatizo yoyote ya ndoa ambayo huenda ukakabili. Naam, azimia ‘kushangilia pamoja na mke wa ujana wako.’—Methali 5:18.

Umejifunza Nini?

• Mkristo anaweza kuingiaje katika uhusiano wa kimahaba bila kujua?

• Ni tahadhari gani zinazoweza kumsaidia mtu asianzishe uhusiano wa kimahaba nje ya ndoa?

• Wenzi wa ndoa wanapaswa kufanya nini wanapokabili matatizo?

• Taja kichocheo kikubwa zaidi cha kudumisha uaminifu katika ndoa.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 26]

Inasikitisha kwamba mahali pa kazi panaweza kutokeza kishawishi cha kuwa na uhusiano usiofaa wa kimahaba

[Picha katika ukurasa wa 28]

‘Kwa ujuzi vyumba vya ndani vitajazwa vitu vyenye kupendeza’