Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uumbaji Unamfunua Mungu Aliye Hai

Uumbaji Unamfunua Mungu Aliye Hai

“Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu . . . kwa sababu uliumba vitu vyote.”UFU. 4:11.

1. Ni lazima tufanye nini ili kuhakikisha kwamba imani yetu inaendelea kuwa yenye nguvu?

WATU wengi husema kwamba wanaamini tu vitu wanavyoona. Tunawezaje kuwasaidia wajenge imani katika Yehova? Kwa kweli, Biblia inasema kwamba “hakuna mwanadamu ambaye amemwona Mungu wakati wowote.” (Yoh. 1:18) Kwa hiyo, tunawezaje kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwa na imani yenye nguvu kumwelekea “Mungu asiyeonekana,” Yehova? (Kol. 1:15) Hatua ya kwanza ni kutambua mafundisho yanayoficha ukweli kumhusu Yehova. Kisha, ni lazima tutumie Biblia kwa ustadi ili kupindua mawazo yoyote ‘yaliyoinuliwa kinyume cha ujuzi wa Mungu.’2 Kor. 10:4, 5.

2, 3. Ni mafundisho gani mawili ya uwongo yanayowapofusha watu na kuwazuia wasijue ukweli kumhusu Mungu?

2 Fundisho la mageuzi ni fundisho la uwongo lililoenea sana na linalopofusha na kuzuia watu kujua ukweli kumhusu Mungu. Fundisho hilo la wanadamu halipatani kamwe na Biblia, nalo huwafanya watu wakose tumaini. Kimsingi, fundisho la mageuzi hudai kwamba uhai ulijitokeza wenyewe; na hilo linamaanisha kwamba uhai wa wanadamu hauna kusudi.

3 Kwa upande mwingine, Wakristo wenye imani kali hufundisha kwamba ulimwengu mzima, pamoja na dunia na viumbe vyote vilivyomo, vimekuwapo kwa maelfu kadhaa tu ya miaka. Huenda wale wanaofundisha fundisho hilo wanaiheshimu Biblia, lakini wanadai kwamba Mungu aliumba kila kitu maelfu kadhaa ya miaka iliyopita katika kipindi cha siku sita tu, kila siku ikiwa na saa 24. Wanakataa uthibitisho wa kisayansi ulio wazi unaopinga maoni yao. Kwa kweli, fundisho hilo linawafanya watu waitilie shaka Biblia. Linaifanya ionekane isiyo sahihi na isiyoeleweka. Wale wanaounga mkono maoni hayo ni kama watu fulani katika karne ya kwanza waliokuwa na bidii kwa ajili ya Mungu “lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” (Rom. 10:2) Tunaweza kulitumiaje Neno la Mungu kupindua  “ngome zenye nguvu” za mafundisho hayo ya uwongo kuhusu uumbaji na mageuzi? * Tunaweza tu kufanya hivyo ikiwa tunajitahidi kabisa kupata ujuzi sahihi wa mafundisho ya Biblia.

IMANI HUTEGEMEA UTHIBITISHO NA SABABU ZINAZOSADIKISHA

4. Imani yetu inapaswa kutegemea nini?

4 Biblia inatufundisha tuweke hazina ya ujuzi. (Met. 10:14) Yehova anataka tujenge imani inayotegemea uthibitisho na sababu zinazosadikisha, badala ya mapokeo ya kidini au falsafa za wanadamu. (Soma Waebrania 11:1.) Ili kujenga imani yenye nguvu kumwelekea Yehova, ni lazima kwanza tusadiki kwamba yeye yupo. (Soma Waebrania 11:6.) Tunafikia mkataa huo kwa kuchunguza mambo ya hakika na kutumia ‘nguvu zetu za kufikiri’ badala ya kufuata tu mawazo yetu.Rom. 12:1.

5. Taja sababu moja inayotusadikishia kwamba Mungu yupo.

5 Mtume Paulo anataja sababu moja inayotusadikishia kwamba Mungu yupo, hata ingawa hatumwoni. Paulo aliandika hivi kumhusu Yehova: “Sifa zake ambazo hazionekani, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kwa vitu vilivyofanywa, yaani, nguvu zake za milele na Uungu.” (Rom. 1:20) Utamsaidiaje mtu anayetilia shaka kuwapo kwa Mungu aone ukweli wa maneno ya Paulo yaliyoongozwa na roho? Chunguza uthibitisho ufuatao wa uumbaji unaofunua nguvu na hekima ya Muumba wetu.

UUMBAJI UNAONYESHA NGUVU ZA MUNGU

6, 7. Ngao mbili zinazotulinda zinafunuaje nguvu za Yehova?

6 Ngao mbili zinazotulinda, yaani, angahewa na nguvu za sumaku za dunia, zinafunua nguvu za Yehova. Kwa mfano, angahewa halitokezi tu hewa tunayopumua, linatulinda pia dhidi ya mawe yanayoanguka kwa kasi kutoka angani. Kwa kawaida, mawe yanayoweza kusababisha uharibifu huteketea yanapoingia kwenye angahewa la dunia na kutokeza nuru nyangavu inayovutia wakati wa usiku.

7 Nguvu za sumaku za dunia zinatulinda pia. Ngao hiyo inaanzia katika kiini cha dunia. Kiini hicho kina chuma kilichoyeyuka, kinachotokeza nguvu nyingi za sumaku zinazozingira dunia yetu na kufika angani. Nguvu hizo hutulinda dhidi ya miale ya jua na milipuko inayotoka kwenye jua. Nguvu hizo za sumaku hufyonza miale hiyo na hivyo kulinda viumbe duniani ili visiteketezwe na miale hiyo. Nguvu za sumaku za dunia husababisha mwangaza maridadi wa rangi mbalimbali unaoonekana angani karibu na ncha ya Kaskazini na ya Kusini. Bila shaka, Yehova ni “hodari katika nguvu.”Soma Isaya 40:26.

VITU VYA ASILI VINAFUNUA HEKIMA YA MUNGU

8, 9. Mizunguko inayotegemeza uhai inafunuaje hekima ya Yehova?

8 Tunaweza kuona hekima ya Yehova tunapochunguza mizunguko inayotegemeza uhai duniani. Kwa mfano: Wazia kwamba unaishi katika jiji lenye watu wengi lililozungukwa na ukuta. Jiji hilo lina kiasi kidogo cha maji safi, na takataka haziwezi kuondolewa jijini. Baada ya muda, jiji hilo litakuwa na uchafu mwingi sana. Kwa njia fulani, dunia yetu ni kama jiji hilo lililozungukwa na ukuta. Ina maji safi lakini yanaweza kwisha na takataka haziwezi kutolewa nje ya dunia. Hata hivyo, “jiji hilo lililozungukwa na ukuta” linategemeza mabilioni ya viumbe, kizazi baada ya kizazi. Kwa nini? Kwa sababu ya mizunguko  yake muhimu yenye kustaajabisha inayotegemeza uhai na kudumisha usafi.

9 Fikiria mzunguko wa oksijeni. Mabilioni ya viumbe huvuta oksijeni na kutoa kaboni dioksidi. Hata hivyo, angahewa letu haliishiwi kamwe na oksijeni na kujaa hewa “chafu” ya kaboni dioksidi. Kwa nini? Kwa sababu ya utaratibu wa pekee unaoitwa usanidi-mwanga. Kupitia utaratibu huo, mimea ya kijani kibichi hutumia hewa ya kaboni dioksidi, maji, nuru ya jua, na madini ili kutokeza kabohidrati na oksijeni. Tunapovuta hewa ya oksijeni, tunakamilisha mzunguko huo. Yehova anatumia kihalisi mimea aliyoumba ili kuwapa “watu wote uhai na pumzi.” (Mdo. 17:25) Kwa kweli, ana hekima ya pekee!

10, 11. Kipepeo anayeitwa monarch na mdudu anayeitwa kereng’ende wanafunuaje hekima ya Yehova?

10 Viumbe vingi sana vinavyoishi katika sayari yetu ya pekee vinafunua hekima ya Yehova. Inakadiriwa kwamba duniani kuna aina milioni 2 hadi milioni 100 hivi za viumbe. (Soma Zaburi 104:24.) Chunguza baadhi ya viumbe hivyo uone jinsi vilivyoumbwa kwa hekima.

Macho ya kereng’ende yenye lenzi nyingi yanafunua hekima ya Mungu (Tazama fungu la 11)

11 Kipepeo anayeitwa monarch ana ubongo unaotoshana na ncha ya kalamu. Hata hivyo, kipepeo huyo ana ustadi na uwezo wa kusafiri umbali wa karibu kilomita 3,000 kuanzia Kanada hadi msitu fulani nchini Mexico. Anafanya hivyo kwa kufuata mwendo wa jua. Anasafiri jinsi gani jua linaposonga angani? Yehova aliumba ubongo wa kipepeo huyo ukiwa na uwezo wa kutambua mwendo wa jua na kubadili njia ili asipotee. Fikiria pia jicho la kereng’ende. Mdudu huyo ana macho mawili yenye lenzi nyingi. Kila jicho lina lenzi 30,000. Hata hivyo, ubongo mdogo wa kereng’ende humwezesha kutambua mawimbi kutoka lenzi hizo zote, na anaweza kutambua mtikisiko wowote katika mazingira yake.

12, 13. Ni nini kinachokuvutia kuhusu jinsi Yehova alivyoumba chembe za mwili wako?

12 Yehova aliumba chembe za mwili kwa njia ya ajabu hata zaidi. Kwa mfano, mwili wako una chembe trilioni 100 hivi. Kila chembe ina molekuli ndogo inayofanana na kamba. Molekuli hiyo inaitwa DNA (deoksiribonyukilia asidi). DNA ina habari nyingi zinazohitajiwa ili kujenga mwili wako.

13 Molekuli ya DNA ina kiasi gani cha habari? Linganisha kiasi cha habari zilizo katika gramu moja ya DNA na kiasi kinachoweza kuwekwa katika diski (CD). Diski inaweza kuhifadhi habari zote zilizo katika kamusi, na hilo linashangaza kwa kuwa diski ni plastiki nyembamba. Hata hivyo, habari zilizo katika gramu moja tu ya DNA zinaweza kutoshea katika diski trilioni moja! Hilo linamaanisha kwamba kiasi kilichokaushwa cha DNA kinachotoshea kwenye kijiko kimoja  cha chai kinaweza kubeba maagizo ya kutosha kutokeza wanadamu trilioni 2.5 hivi!

14. Mambo yaliyogunduliwa na wanasayansi yanakufanya uhisije kumhusu Yehova?

14 Mfalme Daudi alisema kwamba habari zinazohitajiwa ili kutokeza mwili wa mwanadamu zimeandikwa katika kitabu cha mfano. Alisema hivi kumhusu Yehova Mungu: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa, kuhusiana na siku ambazo zilifanyizwa na hakukuwako hata moja kati ya hizo.” (Zab. 139:16) Bila shaka, Daudi alichochewa kumsifu Yehova alipofikiria jinsi alivyoumbwa. Mambo ambayo wanasayansi wamegundua katika miaka ya karibuni yanatuchochea tumheshimu Yehova hata zaidi tunapofikiria jinsi alivyotuumba. Yanatufanya tukubaliane na mtunga-zaburi aliyeandika hivi kumhusu Yehova: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha. Kazi zako ni za ajabu, kama vile nafsi yangu inavyojua vema.” (Zab. 139:14) Kwa kweli, uumbaji unaonyesha wazi kabisa kwamba kuna Mungu aliye hai.

WASAIDIE WENGINE WAMTUKUZE MUNGU ALIYE HAI

15, 16. (a) Machapisho yetu yametuchocheaje kuthamini uwezo wa Yehova wa kuumba? (b) Ni makala gani iliyokuvutia katika sehemu yenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?”

15 Kwa miaka mingi, gazeti la Amkeni! limewasaidia mamilioni ya watu kuthamini sifa za Mungu wetu aliye hai zinazofunuliwa na uumbaji. Kwa mfano, toleo la Septemba 2006, lilikuwa na kichwa “Je, Kuna Muumba?” Lilikusudiwa hasa kufungua macho ya watu waliopofushwa na fundisho la mageuzi na mafundisho ya uwongo kuhusu uumbaji. Dada mmoja aliiandikia hivi ofisi ya tawi ya Marekani kuhusu toleo hilo la pekee: “Kampeni ya kusambaza toleo hilo la pekee ilifanikiwa sana. Mwanamke mmoja ambaye ni mwalimu wa biolojia aliomba nakala 20, ili ampe kila mwanafunzi nakala moja.” Ndugu mwingine aliandika hivi: “Nimekuwa nikihubiri tangu miaka ya 1940 na sasa ninakaribia umri wa miaka 75, hata hivyo sijawahi kamwe kufurahia utumishi wangu kama nilivyofurahia tulipokuwa tukitoa toleo hilo la pekee la Amkeni!

16 Katika miaka ya karibuni, matoleo mengi ya Amkeni! yamekuwa na sehemu yenye kichwa “Je, Ni Kazi ya Ubuni?” Makala hizo fupi zinafunua uhandisi wa kustaajabisha sana ulio katika uumbaji na kuonyesha jinsi ambavyo wanadamu wamejaribu kumwiga Muumba Mkuu. Katika mwaka wa 2010, tulipokea broshua yenye kichwa Uhai—Ulitokana na Muumba? Broshua hiyo inakusudiwa pia kutusaidia kumtukuza Mungu. Picha maridadi na michoro yenye kufundisha iliyo katika broshua hiyo inatuchochea kuthamini uwezo wa Yehova wa kuumba. Maswali yaliyo mwishoni mwa kila sehemu humsaidia msomaji kuchanganua habari aliyosoma. Je, umefurahia kutumia broshua hiyo unapohubiri nyumba kwa nyumba, hadharani, au isivyo rasmi?

17, 18. (a) Wazazi, mnawezaje kuwasaidia watoto wenu ili watetee imani yao kwa uhakika? (b) Mmetumiaje broshua za uumbaji kwenye ibada yenu ya familia?

17 Wazazi, je, mmejifunza na watoto wenu broshua hiyo maridadi katika ibada yenu ya familia? Mkifanya hivyo, mtawasaidia watoto wenu wamthamini Mungu wetu aliye hai. Huenda mna vijana wanaosoma shule ya sekondari. Vijana ni shabaha ya watu wanaofundisha fundisho la uwongo la mageuzi. Wanasayansi, walimu wa shule, vipindi vya televisheni vinavyohusu uumbaji, na sinema zinaeneza wazo la kwamba mageuzi ni fundisho la kweli.  Unaweza kuwasaidia vijana wako kupambana na propaganda hiyo kwa kutumia broshua nyingine yenye kichwa, Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai, iliyotolewa pia mwaka wa 2010. Sawa na broshua yenye kichwa Uhai—Ulitokana na Muumba?, broshua hii inawatia moyo watoto kusitawisha ‘uwezo wao wa kufikiri.’ (Met. 2:10, 11) Inawafundisha kuhakikisha kwamba yale wanayofundishwa shuleni ni mambo ya kweli.

Wazazi, wasaidieni watoto wenu wawe tayari kutetea imani yao (Tazama fungu la 17)

18 Broshua Chanzo cha Uhai imekusudiwa kuwasaidia wanafunzi kuchunguza ripoti zenye kusisimua za vyombo vya habari kuhusu kupatikana kwa mabaki “yaliyokosekana” ya vitu vya kale. Inawahimiza vijana wachunguze wenyewe ikiwa ripoti hizo zinathibitisha kwamba mwanadamu aligeuka kutokana na viumbe wa hali ya chini. Inawafundisha pia kukanusha madai ya kuwa wanasayansi wamethibitisha katika maabara kwamba uhai ulijitokeza wenyewe. Wazazi, mkitumia broshua hizo, mtawasaidia watoto wenu kuwajibu kwa uhakika wale wanaotaka kujua sababu inayowafanya wamwamini Muumba.Soma 1 Petro 3:15.

19. Sote tuna pendeleo gani?

19 Machapisho yaliyofanyiwa utafiti wa kina tunayopewa na tengenezo la Yehova, hutusaidia kutambua sifa zake zenye kuvutia zinazofunuliwa na uumbaji. Huo ni uthibitisho mzuri unaotufanya tububujike sifa kumwelekea Mungu. (Zab. 19:1, 2) Ni pendeleo kama nini kumpa Yehova, Muumba wa vitu vyote, heshima na utukufu anaostahili kabisa!1 Tim. 1:17.

^ fu. 3 Unaweza kuzungumza na wale wanaoamini fundisho hilo ukitumia habari zilizo kwenye ukurasa wa 24 hadi 28 wa broshua Uhai—Ulitokana na Muumba?