Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Dini Nzuri Inawachochea Watu Kuliheshimu Neno la Mungu

Dini Nzuri Inawachochea Watu Kuliheshimu Neno la Mungu

YESU aliwachochea watu waliheshimu Neno la Mungu, Biblia. Jambo hilo linaonekana wazi kutokana na majibu yake alipojaribiwa na Ibilisi. (Mathayo 4:4-11) Kwa mfano, Yesu alitenda jinsi gani Shetani alipomshawishi ageuze mawe yawe mikate? Yesu alipinga kishawishi hicho kwa kunukuu maneno ya Musa ambayo yaliongozwa na roho ya Mungu, na unaweza kuyasoma kwenye Kumbukumbu la Torati 8:3. Na wakati Ibilisi alipomtolea Yesu utawala wa falme zote za ulimwengu kwa kubadilishana na tendo moja tu la ibada, Yesu alimjibu namna gani? Alikataa na kutaja kanuni ya Kimaandiko ambayo unaweza kuipata kwenye Kumbukumbu la Torati 6:13.

Fikiria jambo hili! Ingawa Yesu alikuwa Mwana wa Mungu, alitegemea kabisa Biblia alipokuwa akifundisha. Na bila shaka hakupuuza kamwe Neno la Mungu na kufuata mapokeo ya wanadamu. (Yohana 7:16-18) Hata hivyo, viongozi wengi wa kidini wa siku za Yesu hawakuliheshimu Neno la Mungu kama Yesu alivyoheshimu. Kwa nini? Waliyaona mapokeo ya wanadamu kuwa ya maana sana kuliko Maandiko Matakatifu. Yesu aliwaambia hivi waziwazi wanaume hao wa kidini: “Mkalitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu. Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao huniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”—Mathayo 15:6-9, Union Version.

Dini nyingi ulimwenguni, za Kikristo au zisizo za Kikristo, zinadai kwamba zinaiheshimu Biblia. Lakini unajua dini ngapi ambazo zinakataa mapokeo ya wanadamu wakati mapokeo hayo yanapopingana na mafundisho yaliyo wazi ya Neno la Mungu? Fikiria mifano miwili peke yake.

HABARI: Majina ya cheo ya kidini.

BIBLIA INAFUNDISHA HIVI: Yesu aliwashutumu viongozi wa kidini wa siku zake kwa sababu walipenda majina ya cheo na walitamani kuwa mashuhuri. Alisema kwamba wanaume hao walipenda “viti vya mbele katika karamu, na kuketi mbele katika masinagogi, na kusalimiwa masokoni, na kuitwa na watu, Rabi.” Kisha Yesu akawaambia hivi wanafunzi wake: “Ninyi msiitwe Rabi, maana mwalimu wenu ni mmoja, nanyi nyote ni ndugu. Wala msimwite mtu baba duniani; maana Baba yenu ni mmoja, aliye wa mbinguni.”—Mathayo 23:1-10, UV.

SWALI: Je, viongozi wa dini hiyo wanapenda kuitwa kwa majina ya cheo na kutaka kuwa mashuhuri katika jamii, au wanatii amri ya Yesu na kuepuka kufanya hivyo?

HABARI: Kutumia sanamu katika ibada.

BIBLIA INAFUNDISHA HIVI: “Usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu cho chote kilicho juu mbinguni, wala kilicho chini duniani, wala kilicho majini chini ya dunia. Usivisujudie wala kuvitumikia.”—Kutoka 20:4, 5, UV.

Mtume Yohana aliwaandikia hivi Wakristo: “Epukaneni na sanamu za miungu!”—1 Yohana 5:21, Biblia Habari Njema.

SWALI: Je, dini hiyo inatii amri ya Biblia iliyo wazi ya kuepuka kutumia mifano na sanamu katika kumwabudu Mungu?

Unaweza Kupata Njia Inayofaa

Ingawa leo kuna idadi kubwa yenye kutatanisha ya dini, unaweza kupata dini inayoongoza kwenye uzima. Kuna mambo mengi ambayo yanaweza kutusaidia kuitambua “dini iliyo safi na isiyo na hitilafu mbele ya Mungu.” (Yakobo 1:27, BHN) Maandiko yaliyotajwa katika habari hizi ni kama ishara za barabarani ambazo zinaweza kukuelekeza kwenye dini hiyo.

Tafadhali waombe Mashahidi wa Yehova wakufafanulie majibu ya maswali ambayo yameulizwa katika habari hizi. Unapochunguza majibu yao, iga mfano mzuri wa watu ambao waliishi katika karne ya kwanza katika jiji la Beroya. Baada ya kumsikia mtume Paulo akihubiri, “wakawa wanayachunguza Maandiko Matakatifu kila siku, ili kuona kama yale waliyosema Paulo na Sila yalikuwa kweli.” (Matendo 17:11, BHN) Ikiwa utaliheshimu Neno la Mungu na kujifunza kwa bidii kama Waberoya, utapata njia inayoongoza kwenye uzima. Ni juu yako kuamua ikiwa utaifuata njia hiyo.

Ni dini gani ambayo inawatia watu moyo wajifunze Maandiko ili waone ikiwa mambo wanayojifunza ni ya kweli?