Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhusu Wakati Ujao wa Wanadamu

Kuhusu Wakati Ujao wa Wanadamu

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Kuhusu Wakati Ujao wa Wanadamu

Je, Yesu aliwaahidi wanadamu uzima mbinguni?

Ndiyo, aliwaahidi! Yesu mwenyewe alifufuliwa, naye akapanda mbinguni ili awe pamoja na Baba yake. Lakini kabla ya kufa na kufufuliwa, aliwaambia hivi mitume wake 11 waaminifu: “Katika nyumba ya Baba yangu mna makao mengi. . . . Ninaenda kuwatayarishia ninyi mahali.” (Yohana 14:2) Hata hivyo, wale ambao wangeenda mbinguni wangekuwa wachache. Yesu alionyesha wazi ukweli huo alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Msiogope, kundi dogo, kwa sababu Baba yenu amekubali kuwapa ninyi ufalme.”—Luka 12:32.

Hilo “kundi dogo” litafanya nini mbinguni?

Baba anataka kikundi hicho kidogo kiwe sehemu ya serikali ya mbinguni pamoja na Yesu. Tunajua hivyo jinsi gani? Baada ya kufufuliwa, Yesu alimfunulia mtume Yohana kwamba watu fulani waaminifu “watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 1:1; 5:9, 10) Hiyo ni habari njema. Moja ya mambo ambayo wanadamu wanahitaji sana ni serikali nzuri. Serikali hiyo inayotawaliwa na Yesu itatimiza nini? Yesu alisema: “Katika uumbaji-mpya Mwana wa binadamu atakapoketi juu ya kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi ambao mmenifuata mtaketi pia juu ya viti vya ufalme kumi na viwili.” (Mathayo 19:28) Utawala wa Yesu na wafuasi wake utatokeza “uumbaji-mpya,” au kurudishwa upya kwa hali kamilifu ambazo wenzi wawili wa kwanza wanadamu walifurahia duniani kabla ya kutenda dhambi.

Yesu aliwapa wanadamu wengine tumaini gani?

Wanadamu waliumbwa waishi duniani, tofauti na Yesu, ambaye aliumbwa aishi mbinguni. (Zaburi 115:16) Hivyo, Yesu alisema hivi: “Ninyi mnatoka kwenye makao ya chini; mimi ninatoka kwenye makao ya juu.” (Yohana 8:23) Yesu alisema kwamba wanadamu watakuwa na wakati ujao mzuri ajabu duniani. Pindi moja alisema hivi: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mathayo 5:5) Alikuwa akifikiria zaburi iliyoongozwa na roho takatifu inayosema hivi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani. Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:11, 29.

Kwa hiyo, “kundi dogo,” ambao wanaenda mbinguni, si wao peke yao watakaopokea uzima wa milele. Yesu alizungumza pia kuhusu tumaini ambalo linatolewa kwa ulimwengu wote wa mamilioni ya wanadamu. Alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Mungu atakomesha jinsi gani mateso yanayowapata wanadamu?

Yesu alisema jinsi ambavyo vyanzo viwili vya mateso vitaondolewa: “Sasa ulimwengu huu unahukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” (Yohana 12:31) Kwanza, watu wasiomwogopa Mungu ambao wanasababisha mateso watahukumiwa na kuharibiwa. Pili, Shetani atatupwa nje na hatawapotosha tena wanadamu.

Namna gani wale ambao katika historia yote wameishi na kufa bila kupata nafasi ya kujifunza kumhusu Mungu na Kristo na kuonyesha kwamba wanawaamini? Yesu alimwambia hivi mtenda-maovu aliyekufa kando yake: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.” (Luka 23:43) Mtu huyo, pamoja na mamilioni ya watu wengine, atakuwa na nafasi ya kujifunza kumhusu Mungu wakati Yesu atakapomfufua kutoka kwa wafu katika paradiso duniani. Kisha atapata nafasi ya kuwa kati ya watu wapole na waadilifu ambao watapewa uzima wa milele duniani.—Matendo 24:15.

Kwa habari zaidi ona sura ya 3 na ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 13 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 23]

“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29