Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Kristo Ni Nani?

Yesu Kristo Ni Nani?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Yesu Kristo Ni Nani?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Yesu Kristo ni nani?

Tofauti na mwanadamu mwingine yeyote, Yesu aliishi mbinguni akiwa kiumbe wa roho kabla ya kuzaliwa hapa duniani. (Yohana 8:23) Yeye ndiye aliyeumbwa kwanza na Mungu na alisaidia katika kuumba vitu vingine vyote. Ni yeye tu aliyeumbwa moja kwa moja na Yehova na hivyo anaitwa Mwana “mzaliwa-pekee” wa Mungu. Yesu pia anaitwa “Neno” kwa kuwa alikuwa msemaji wa Mungu.—Yohana 1:1-3, 14; soma Methali 8:22, 23, 30; Wakolosai 1:15, 16.

2. Kwa nini Yesu alikuja duniani?

Mungu alimtuma Mwana wake duniani kwa kuhamisha uhai wake kutoka mbinguni na kuuweka katika tumbo la uzazi la bikira Myahudi aliyeitwa Maria. Kwa hiyo Yesu hakuwa na baba wa kibinadamu. (Luka 1:30-35) Yesu alikuja duniani (1) kufundisha ukweli kumhusu Mungu, (2) kuweka mfano katika kufanya mapenzi ya Mungu, na (3) kutoa uhai wake mkamilifu uwe “fidia,” au dhabihu ya ukombozi.—Soma Mathayo 20:28; Yohana 18:37.

3. Kwa nini tunahitaji fidia?

Fidia ni kitu kinachotolewa kama malipo ili kumkomboa mtu kutoka utumwani. Mwanzoni Mungu hakukusudia wanadamu wazeeke na kufa. Tunajuaje jambo hilo? Mungu alimwambia mwanadamu wa kwanza, Adamu, kuwa iwapo angefanya kile ambacho Biblia hukiita dhambi, angekufa. Kama Adamu hangefanya dhambi, hangekufa. Ingawa Adamu alikufa karne kadhaa baadaye, alianza kufa ile siku ambayo alikosa kumtii Mungu. (Mwanzo 2:16, 17; 5:5) Watoto wote wa Adamu walirithi dhambi na adhabu yake ambayo ni kifo. Hivyo, kifo ‘kikaingia’ katika ulimwengu wa binadamu kupitia Adamu. Hiyo ndiyo sababu tunahitaji fidia.—Soma Waroma 5:12; 6:23.

4. Kwa nini Yesu alikufa?

Ni nani ambaye angeweza kulipa fidia ili kutukomboa kutoka katika kifo? Tunapokufa, tunalipia adhabu ya dhambi zetu tu. Mwanadamu ambaye si mkamilifu hawezi kulipia dhambi za wengine.—Soma Zaburi 49:7-9.

Kwa kuwa Yesu hakurithi hali ya kutokamilika kutoka kwa baba wa kibinadamu, alikufa, si kwa sababu ya dhambi zake mwenyewe, bali kwa sababu ya dhambi za wengine. Mungu alimtuma Mwana wake afe kwa ajili yetu ili kuonyesha upendo Wake mkubwa kwa wanadamu. Yesu pia alituonyesha upendo kwa kumtii Baba yake na kutoa uhai wake kwa ajili ya dhambi zetu.—Soma Yohana 3:16; Waroma 5:18, 19.

5. Yesu anafanya nini sasa?

Kwa kuwaponya wagonjwa, kuwafufua wafu, na kuwakomboa watu kutoka katika dhambi na kifo, Yesu alionyesha mambo ambayo hatimaye angewafanyia wanadamu wote watiifu. (Luka 18:35-42; Yohana 5:28, 29) Baada ya Yesu kufa, Mungu alimfufua akiwa kiumbe wa roho. (1 Petro 3:18) Kisha, Yesu akangoja akiwa kwenye mkono wa kuume wa Mungu mpaka alipopewa mamlaka ya kutawala akiwa Mfalme wa dunia yote. (Waebrania 10:12, 13) Sasa Yesu anatawala akiwa Mfalme mbinguni, na wafuasi wake duniani wanatangaza habari hizo njema duniani kote.—Soma Danieli 7:13, 14; Mathayo 24:14.

Karibuni, Yesu atatumia mamlaka yake akiwa Mfalme kukomesha mateso yote na wale wanaoyasababisha. Mamilioni ya watu wanaomwamini Yesu na kumtii watafurahia uhai katika dunia paradiso.—Soma Zaburi 37:9-11.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 4 ya kitabu hiki Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 17]

Mamilioni ya watu wanaomwamini na kumtii Yesu watafurahia uhai katika dunia paradiso