Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

MWANAMKE kijana ambaye hakupendezwa na Mungu na ambaye alifurahia kazi yenye mshahara mnono alipataje kusudi la kweli maishani? Kijana Mkatoliki alijifunza nini kuhusu kifo na hivyo kubadili maisha yake? Na kijana ambaye alikuwa amekata tamaa maishani alijifunza nini kumhusu Mungu ambacho kilimchochea awe mhudumu Mkristo? Soma yale ambayo watu hao wanasema.

“Kwa miaka mingi nilijiuliza, ‘Kwa nini tuko hai?’”​—ROSALIND JOHN

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1963

  • NCHI: UINGEREZA

  • HISTORIA: ALIFURAHIA KAZI YENYE MSHAHARA MNONO

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa huko Croydon, Kusini mwa London, nikiwa mtoto wa sita katika familia ya watu tisa. Wazazi wangu wana asili ya kisiwa cha St. Vincent kilicho huko Karibea. Mama alikuwa mshiriki wa kanisa la Methodisti. Sikupenda kujifunza kumhusu Mungu, ingawa nilikuwa na tamaa kubwa ya kupata ujuzi. Mara nyingi, wakati wa likizo za shule nilikaa kando ya ziwa la eneo letu, nikisoma vitabu mbalimbali nilivyoazima kutoka kwenye maktaba.

Miaka kadhaa baada ya kumaliza masomo, nilitambua kwamba nilitaka kusaidia watu wasio na uwezo. Nilianza kufanya kazi ya kuwasaidia watu wasio na makazi, walemavu, na wenye matatizo ya kujifunza. Kisha, nikajiunga na chuo kikuu ili kusomea sayansi ya afya. Baada ya kuhitimu, nilifurahia kufanya kazi mbalimbali zenye mshahara mnono, na maisha yangu yakawa ya starehe zaidi. Nikiwa mshauri wa mambo ya usimamizi na mtafiti wa mambo ya kijamii aliyejiajiri, nilihitaji tu kuwa na kompyuta inayobebwa mkobani na kuwa mahali penye Intaneti. Ningesafiri kwa ndege kwa majuma kadhaa, na kuishi kwenye hoteli niliyopenda, nikifurahia mazingira mazuri, na kutumia huduma zao za kuoga kwa maji yenye madini na kutumia chumba cha mazoezi. Kwa kweli, nilifikiri ninafurahia maisha. Lakini sikuacha kuwahangaikia watu wanaoteseka.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Kwa miaka mingi nilijiuliza, ‘Kwa nini tuko hai, na kusudi la maisha ni nini?’ Lakini sikuwahi kamwe kujaribu kutafuta majibu katika Biblia. Siku moja mwaka wa 1999, dada yangu mdogo Margaret, ambaye alikuwa amejifunza na kuwa Shahidi wa Yehova, alinitembelea akiwa na rafiki yake ambaye alikuwa Shahidi, na rafiki huyo alipendezwa nami kibinafsi. Nilishangaa nilipokubali kujifunza Biblia pamoja na rafiki ya dada yangu, lakini nilifanya maendeleo polepole, kwa sababu nilitumia muda mwingi kufanya kazi na kujifurahisha.

Katika majira ya joto ya mwaka wa 2002, nilihamia kusini-magharibi mwa Uingereza. Nikiwa huko nilisomea digrii ya pili ya utafiti wa mambo ya kijamii katika chuo kikuu nikiwa na lengo la kupata shahada ya juu. Mimi na mwanangu tulianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida kwenye Jumba la Ufalme la eneo letu. Ingawa nilikuwa na elimu ya juu, kujifunza Biblia kulinisaidia kuelewa kwa undani zaidi matatizo ya maisha na jinsi yatakavyosuluhishwa. Nilielewa ukweli wa andiko la Mathayo 6:24, linalosema kwamba haiwezekani kuwatumikia mabwana wawili. Nilihitaji kuamua kumtumikia Mungu au utajiri. Nilijua kwamba nilipaswa kufanya uamuzi kuhusu mambo niliyotanguliza maishani.

Mwaka uliotangulia, nilikuwa nimehudhuria mara kadhaa kikundi cha funzo la Biblia la nyumbani ambapo Mashahidi walijifunza kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? * Nilisadikishwa kwamba ni Muumba wetu tu, Yehova, aliye na suluhisho la matatizo yanayowakumba wanadamu. Wakati huo, chuoni tulikuwa tukifundishwa kwamba kusudi la maisha halihusishi kuamini kuna Muumba. Nilikasirika sana. Baada ya miezi miwili, niliacha masomo ya chuo kikuu na nikaamua kutumia muda mwingi kufanya mambo ya kiroho.

Andiko lililonichochea kubadili maisha yangu ni Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Kujifunza kumhusu Mungu wetu mwenye upendo kuliniletea baraka nyingi kuliko utajiri wowote wa kimwili na cheo ambacho shahada ya juu ingenipa. Kadiri nilivyozidi kujifunza kuhusu kusudi la Yehova kwa dunia na daraka ambalo Yesu alitimiza katika kudhabihu uhai wake kwa ajili yetu, ndivyo nilivyotamani kutoa maisha yangu kwa Muumba wetu. Nilibatizwa Aprili 2003. Baada ya hapo, nilirahisisha maisha yangu pole kwa pole.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Urafiki wangu pamoja na Yehova ni wenye thamani kubwa. Nimepata amani ya moyoni na shangwe kwa kumjua. Pia, ninapata furaha nyingi kwa kushirikiana na waabudu wengine wa kweli wa Mungu.

Tamaa yangu ya kupata ujuzi inaendelea kutoshelezwa kwa wingi kupitia mambo ninayojifunza katika Biblia na kwenye mikutano ya Kikristo. Ninafurahia kuwahubiria wengine kuhusu imani yangu. Sasa hiyo ndiyo kazi yangu, ambayo kwa kweli inaweza kuwasaidia watu wawe na maisha bora sasa na pia kuwa na tumaini zuri ajabu la kuishi katika ulimwengu mpya. Tangu Juni 2008, nimekuwa mhudumu wa wakati wote, na nina furaha zaidi na kuridhika kuliko wakati mwingine wowote. Nimepata kusudi la kweli maishani na hivyo ninamshukuru sana Yehova.

“Kifo cha rafiki yangu kilinishtua sana.”​—ROMAN IRNESBERGER

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1973

  • NCHI: AUSTRIA

  • HISTORIA: MCHEZA KAMARI

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nililelewa katika mji mdogo wa Braunau, Austria. Eneo hilo lilikuwa la matajiri na halikuwa na uhalifu mwingi. Familia yetu ilikuwa ya Kikatoliki na nililelewa katika dini hiyo.

Tukio fulani katika maisha yangu ya utotoni lilinishtua sana. Mwaka wa 1984, nilipokuwa na umri wa miaka 11 hivi, ninakumbuka nilipokuwa nikicheza mpira wa miguu pamoja na rafiki yangu wa karibu. Siku hiyo alasiri, alikufa kwenye aksidenti ya gari. Kifo cha rafiki yangu kilinishtua sana. Kwa miaka mingi baada ya aksidenti hiyo, nilijiuliza ni nini kinachotupata tunapokufa.

Nilipomaliza masomo, nilifanya kazi ya fundi-umeme. Ingawa nilikuwa na mazoea ya kucheza kamari na kutumia kiasi kikubwa cha pesa, sikuwa na matatizo ya kifedha. Pia, nilitumia muda mwingi katika michezo na nikapenda muziki wenye mdundo mzito. Maisha yangu yalihusisha kwenda disko na kujifurahisha kila wakati. Nilikuwa nikiishi maisha ya kufuatia anasa, yaliyo mapotovu kiadili lakini sikuridhika.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mwaka wa 1995, Shahidi fulani mwenye umri mkubwa alibisha mlango wangu na kunipa kitabu ambacho kilizungumzia jibu la Biblia la swali, Ni nini hutupata tunapokufa? Bado nilisumbuliwa na kifo cha mvulana aliyekuwa rafiki yangu, hivyo nikachukua kitabu hicho. Sikusoma sura hiyo tu bali nilisoma kitabu hicho chote!

Mambo niliyosoma yalijibu maswali yangu kuhusu kifo. Lakini nilijifunza mengi zaidi. Kwa kuwa nililelewa nikiwa Mkatoliki, sehemu kubwa ya imani yangu ilikuwa kumwamini Yesu. Hata hivyo, kuchunguza Biblia kwa makini kulinisaidia kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na Baba ya Yesu, Yehova Mungu. Nilifurahi kujifunza kwamba Yehova anajifunua na angependa tuwe rafiki zake na anawasaidia watu wanaomtafuta wamjue vizuri. (Mathayo 7:7-11) Nilijifunza kwamba Yehova ana hisia. Pia, nilijifunza kuwa sikuzote yeye hutimiza ahadi zake. Hilo lilinifanya nipendezwe sana na unabii wa Biblia na kuchunguza jinsi ulivyotimizwa. Mambo niliyojifunza yaliimarisha imani yangu katika Mungu.

Baada ya muda nilitambua kwamba Mashahidi wa Yehova ndio tu wanaopendezwa kikweli kuwasaidia watu kuielewa Biblia. Niliandika maandiko yanayotajwa katika machapisho ya Mashahidi na nikayasoma kwenye nakala yangu ya tafsiri ya Catholic Bible. Kadiri nilivyoendelea kufanya utafiti, ndivyo nilivyotambua kwamba nilikuwa nimepata ukweli.

Kwa kujifunza Biblia nilitambua kwamba Yehova alitazamia niishi kulingana na viwango vyake. Baada ya kusoma andiko la Waefeso 4:22-24, niliona kuwa nilipaswa kuvua “utu wa zamani,” ambao ulifanyizwa na ‘mwenendo wangu wa kwanza’ na kwamba nilipaswa “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu.” Hivyo, nikaacha maisha yangu mapotovu kiadili. Vilevile, nilitambua nilihitaji kuacha kucheza kamari, kwa kuwa tabia hiyo inachochea tamaa ya kupata mali na kuwa na pupa. (1 Wakorintho 6:9, 10) Nilijua kwamba ili nifanye mabadiliko hayo, nilipaswa kuacha kushirikiana na marafiki wangu wa zamani na kutafuta marafiki wapya ambao walifuata viwango kama vyangu.

Haikuwa rahisi kufanya mabadiliko hayo. Lakini nilianza kuhudhuria mikutano pamoja na Mashahidi kwenye Jumba la Ufalme na nikaanza kupata marafiki wapya katika kutaniko letu. Pia, niliendelea kujifunza Biblia kwa makini nikiwa peke yangu. Hatua hizo zilinisaidia kubadili muziki niliopenda, miradi yangu maishani, na kuwa nadhifu. Mwaka wa 1995, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Sasa nina mtazamo unaofaa kuhusu pesa na mali. Nilikuwa na hasira kali, lakini sasa nimepunguza hasira yangu. Pia, sihangaikii tena wakati ujao kupita kiasi.

Ninafurahi kuwa sehemu ya kikundi cha kimataifa cha watu wanaomtumikia Yehova. Miongoni mwao ninaona watu wanaojitahidi kukabiliana na matatizo lakini bado wanamtumikia Mungu kwa uaminifu. Ninashukuru kwamba sasa ninatumia wakati na nguvu zangu zote kumwabudu Yehova na kuwatendea watu wengine mambo mema bali si kutosheleza tamaa zangu mwenyewe.

“Hatimaye, maisha yangu yana kusudi.”​—IAN KING

  • MWAKA WA KUZALIWA: 1963

  • NCHI: UINGEREZA

  • HISTORIA: ALIKUWA AMEKATA TAMAA

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nilizaliwa Uingereza, na nilipokuwa na umri wa miaka saba hivi, familia yetu ilihamia Australia. Tuliishi katika eneo la Gold Coast, ambalo ni kivutio cha watalii katika jimbo la Queensland, Australia. Ingawa hatukuwa matajiri, sikuzote familia yetu haikukosa mahitaji ya lazima.

Ingawa nililelewa katika hali nzuri, sikuwahi kamwe kuwa na furaha. Nilikatishwa tamaa sana maishani. Baba yangu alikuwa mlevi kupindukia. Sikuwa na uhusiano wa karibu naye, hasa kwa sababu ya tabia yake ya kulewa na jinsi alivyomtendea mama. Baadaye, nilianza kuelewa kwa nini alitenda hivyo nilipotambua mambo aliyopitia alipokuwa mwanajeshi huko Malaya.

Nilianza kunywa pombe kupindukia nilipokuwa kwenye shule ya sekondari. Nilipokuwa na umri wa miaka 16, niliacha shule na kujiunga na jeshi la wanamaji. Nilianza kutumia dawa za kulevya na nikawa mraibu wa sigara. Pia, niliendelea kunywa pombe kupita kiasi. Nilianza kunywa kupindukia kila mwisho juma, kisha nikaanza kunywa kila siku.

Nilipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, nilianza kujiuliza, ‘Je, Mungu yupo.’ Nilijiambia, ‘Ikiwa kweli Mungu yuko, kwa nini anaruhusu watu wateseke na kufa?’ Hata niliandika mashairi ya kumlaumu Mungu kwa sababu ya uovu wote ulio duniani.

Nilipokuwa na umri wa miaka 23, niliondoka jeshini. Nilifanya kazi mbalimbali na hata nikasafiri kwenda kwenye nchi nyingine kwa mwaka mmoja, lakini hilo halikunisaidia. Sikutamani kuwa na malengo au kutimiza jambo lolote. Hakuna kitu kilichonipendeza. Sikuona umuhimu wa kuwa na nyumba yangu mwenyewe, kazi nzuri, na kupandishwa cheo. Nilipata “faraja” kwa kunywa pombe na kusikiliza muziki tu.

Ninakukumbuka wakati hususa nilipotamani sana kujua kusudi la maisha. Nilikuwa huko Poland nikitembelea kambi ya mateso ya Auschwitz yenye sifa mbaya. Nilikuwa nimesoma kuhusu ukatili mbaya uliofanyika huko. Lakini niliposimama mahali hapo na kuona ukubwa wa kambi hiyo, niliguswa moyo sana. Sikuelewa kwa nini watu wanaweza kuwatendea wanadamu wenzao kwa ukatili hivyo. Ninakumbuka nikitembea huku na huku kambini nikitokwa na machozi na kujiuliza, ‘Kwa nini?’

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Mwaka wa 1993, baada ya kurudi nyumbani, nilianza kusoma Biblia ili kutafuta majibu. Muda mfupi baadaye, Mashahidi wawili wa Yehova walinitembelea nyumbani na kunialika kwenye kusanyiko ambalo lingefanywa kwenye uwanja uliokuwa karibu. Niliamua kuhudhuria.

Miezi michache mapema, nilikuwa kwenye uwanja huohuo ili kutazama mechi, lakini wakati wa kusanyiko kulikuwa na tofauti kubwa. Mashahidi walijiendesha kwa njia nzuri na walivalia nadhifu, na watoto wao walikuwa na adabu. Na nilishangazwa na kile nilichoona wakati wa chakula cha mchana. Mamia ya Mashahidi walikula chakula uwanjani, lakini waliporudi kwenye viti, sikuona takataka yoyote uwanjani! Zaidi ya yote, watu hao walionekana kuwa wenye kuridhika na wenye amani, mambo niliyotamani. Sikumbuki hotuba yoyote iliyotolewa siku hiyo, lakini siwezi kusahau mwenendo wa Mashahidi.

Jioni hiyo, nilimfikiria binamu yangu ambaye alisoma Biblia na kuchunguza dini mbalimbali. Miaka kadhaa iliyotangulia, aliniambia kwamba Yesu alisema watu wangetambua dini ya kweli kupitia matunda yake. (Mathayo 7:15-20) Nilihisi kwamba angalau nilipaswa kuchunguza kwa nini Mashahidi walikuwa tofauti. Kwa mara ya kwanza maishani, nilipata matumaini.

Juma lililofuata, wale Mashahidi wawili ambao walinialika kusanyikoni walirudi. Walijitolea kunifunza Biblia, nami nikakubali. Pia, nikaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo pamoja nao.

Nilipoendelea kujifunza Biblia, maoni yangu kumhusu Mungu yalibadilika kabisa. Nilijifunza kwamba hasababishi uovu na kuteseka na kwamba yeye mwenyewe anaumia watu wanapofanya mambo mabaya. (Mwanzo 6:6; Zaburi 78:40, 41) Niliazimia kwamba sitamuumiza Yehova kamwe. Nilitaka kuufurahisha moyo wake. (Methali 27:11) Niliacha kunywa pombe kupita kiasi na kuvuta sigara, na nikaacha mwenendo mpotovu. Mnamo Machi 1994, nilibatizwa na kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Sasa nimeridhika na nina furaha ya kweli. Sitegemei tena pombe ili kutatua matatizo yangu. Badala yake, nimejifunza kumtupia Yehova mizigo yangu.—Zaburi 55:22.

Kwa miaka kumi iliyopita, nimekuwa mume wa mke mrembo ambaye ni Shahidi anayeitwa Karen, na nina binti mzuri wa kambo anayeitwa Nella. Sote watatu, tunafurahia kutumia wakati mwingi katika huduma ya Kikristo, tukiwasaidia watu wajifunze ukweli kumhusu Mungu. Hatimaye, maisha yangu yana kusudi.

^ fu. 11 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.