Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri Ya Furaha Ya Familia

Kukabiliana na Madeni

Kukabiliana na Madeni

Giannis: * “Biashara yangu iliporomoka wakati wa matatizo ya kiuchumi yaliyoikumba nchi ya Ugiriki, na hivyo hatungeweza kuendelea kulipa mkopo wa nyumba na malipo ya kadi ya mkopo. Sikuweza kulala kwa sababu ya mkazo huo.”

Katerina: “Tulikuwa tumejenga nyumba yetu tuliyoipenda sana, na sikuwazia kwamba tunaweza kuipoteza. Mimi na Giannis tuligombana mara nyingi kuhusu jinsi ambavyo tungekabiliana na madeni yetu.”

MADENI yanaweza kuvunja familia au hata kuifanya iwe na mkazo. Kwa mfano, mtafiti Jeffrey Dew aligundua kwamba wenzi wa ndoa wenye madeni hutumia wakati mchache wakiwa pamoja, wanagombana mara nyingi na hawana furaha. Kwa kulinganishwa na mazungumzo mengine, mabishano yanayohusu madeni na pesa huwa marefu, hutokeza kelele na kupigana, na inaelekea yanasababisha mabishano kuhusu mambo mengine. Hivyo, haishangazi kwamba chanzo kikuu cha talaka nchini Marekani ni mizozo kuhusu pesa.

Kuwa na madeni mengi kunaweza pia kusababisha matatizo ya kiafya, kama vile kukosa usingizi, kuumwa na kichwa, mshtuko wa moyo, na mfadhaiko. Mke anayeitwa Marta anasema: “Mume wangu, Luís, alifadhaika sana kuhusu madeni yetu hivi kwamba alilala karibu siku nzima. Mwanamume ambaye sikuzote nilikuwa namtegemea alikuwa hana uwezo.” Wengine hulemewa na mkazo huo. Kwa mfano, kituo cha habari cha BBC kiliripoti kwamba mke fulani kusini mashariki mwa India alikuwa amejiua baada ya kushindwa kulipa mikopo ambayo kwa ujumla ilikuwa dola 840 za Marekani. Alikuwa amekopa pesa hizo ili alipie gharama za matibabu ya watoto wake.

Namna gani ikiwa familia yako ina mkazo kwa sababu ya madeni? Acheni tuchunguze matatizo fulani ambayo wenzi wa ndoa hukabili wanapolipa madeni na tuone kanuni za Biblia zinazoweza kuwasaidia.

TATIZO LA 1: Tunalaumiana.

Lukasz anasema: “Nilimlaumu mke wangu kwa sababu ya kutumia pesa vibaya, naye alilalamika kwamba tungekuwa na pesa za kutosha ikiwa ningekuwa na kazi ambayo ingenipa mshahara kwa mwaka mzima.” Wenzi wa ndoa wanaweza kufanya nini ili madeni yasiharibu uhusiano wao?

Siri ya kufanikiwa: Shirikianeni mnapokabiliana na deni.

Hakuna haja ya kumkasirikia mwenzi wako, hata kama hukushiriki kukopa deni hilo. Sasa, kuliko wakati mwingine wowote, shauri la Biblia lililo kwenye Waefeso 4:31 linaweza kutumika: “Uchungu wote wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote.”

Kabilianeni na deni bali sio kupigana. Mume anayeitwa Stephanos anaeleza jinsi alivyoshirikiana na mke wake: “Tuliona deni letu kama adui yetu.” Ushirikiano kama huo unapatana na andiko la Methali 13:10, linalosema: “Kwa sababu ya kimbelembele mtu husababisha tu pambano, lakini wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” Badala ya kujaribu kwa kimbelembele kusuluhisha mambo peke yako, zungumzeni waziwazi kuhusu matatizo ya pesa kisha mshirikiane.

Watoto wenu wanaweza kuwasaidia pia. Baba anayeitwa Edgardo, kutoka Argentina, anaeleza kuhusu familia yake: “Mwanangu mdogo alitaka baiskeli mpya, lakini tulimweleza kwa nini hatungeweza kumnunulia. Badala yake, tulimpa baiskeli iliyokuwa ya babu yake, na akafurahia sana kuiendesha. Nilijifunza umuhimu wa kushirikiana pamoja kama familia.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Pangeni wakati wa kuzungumza waziwazi na kwa utulivu kuhusu deni lenu. Tambueni makosa yoyote ambayo huenda mlifanya. Badala ya kukazia fikira mambo yaliyopita, jaribuni kukubaliana kuhusu kanuni ambazo mtafuata mnapopanga matumizi yenu ya pesa ya wakati ujao.—Zaburi 37:21; Luka 12:15.

TATIZO LA 2: Inaonekana hamwezi kuishi bila madeni.

Enrique anakumbuka hivi: “Kwa sababu ya biashara yangu, nilikuwa na deni kubwa na hali ikawa mbaya zaidi kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi yaliyoikumba nchi ya Argentina. Na wakati huo, mke wangu alihitaji kufanyiwa upasuaji. Nilihisi siwezi kuishi bila madeni, kana kwamba nilikuwa nimenaswa kwenye mtego.” Mwanamume anayeitwa Roberto kutoka Brazili, alipoteza pesa zote alizoweka akiba baada ya biashara kuporomoka na alikuwa na madeni katika benki 12. Anasema: “Niliaibika sana kukutana uso kwa uso na marafiki wangu. Nilijihisi sifai.”

Unaweza kufanya nini ikiwa unajihisi umevunjika moyo, mwenye hatia, au kuaibika kwa sababu ya madeni?

Siri ya kufanikiwa: Pangia matumizi ya pesa zako. *

 

1. Tambua matumizi yako ya sasa ya pesa. Andika rekodi ya matumizi yote ya pesa unazopokea na unazotumia katika nyumba yako kwa majuma mawili au mwezi mmoja, ikitegemea hali. Andika kwenye rekodi yako gharama za matumizi kama vile kulipa kodi, bima, au mavazi, ambazo huenda zisitokee mara kwa mara, na uandike wastani wa pesa unazotumia kwa gharama hizo kwa mwezi.

2. Ongeza mapato yako. Unaweza kufanya kazi ya ziada mahali ulipoajiriwa, kufanya kazi za majira, kumfundisha mwanafunzi wa shule masomo ya ziada, kurekebisha vitu vilivyotumika, au kubadili jambo unalopenda kufanya unapostarehe liwe biashara. Tahadhari: Uwe mwangalifu ili usiruhusu kazi ivuruge shughuli muhimu zaidi, kama vile mazoea yako ya kiroho.

Tafuteni njia nzuri za kukabiliana na madeni mkiwa familia

3. Punguza matumizi yako. Nunua vitu unavyohitaji, bali si kwa sababu vinauzwa kwa bei ya chini. (Methali 21:5) Enrique aliyetajwa mapema anasema: “Ni vizuri kusubiri kabla ya kununua kwa kuwa unapata wakati wa kuamua ikiwa kwa kweli unahitaji kitu fulani au unatamani tu kuwa nacho.” Ona madokezo zaidi.

  • Nyumba: Ikiwezekana hamieni kwenye nyumba yenye kodi ya chini zaidi kila mwezi. Punguza gharama za matumizi kwa kudhibiti matumizi ya umeme na maji.

  • Chakula: Beba chakula chepesi cha mchana badala ya kuzoea kula kwenye mkahawa. Nunua vitu vinavyouzwa kwa bei iliyopunguzwa. Joelma, kutoka Brazili anasema: “Ninahifadhi pesa kwa kununua mboga na matunda barabarani kabla tu biashara hazijafungwa.”

  • Usafiri: Uza magari usiyohitaji, na udumishe gari ulilo nalo badala ya kuliuza haraka na kununua gari jipya la kisasa. Tumia usafiri wa umma au utembee inapowezekana.

Baada ya kupunguza matumizi yako, utakuwa tayari kutumia vizuri pesa zinazobaki.

4. Chunguza madeni yako na uchukue hatua. Kwanza, chunguza kiasi cha riba cha kila deni, malipo mengine, pesa unazotozwa kwa kulipa ukiwa umechelewa au unapokosa kulipa, na uwezekano wa kwamba deni limechelewa kulipwa. Soma kwa makini maandishi yanayohusiana na mkopo huo, kwa kuwa huenda wakopeshaji wakawa wadanganyifu. Kwa mfano, shirika moja la kutoa mkopo wa muda mfupi nchini Marekani lilisema kwamba kiasi cha riba kilikuwa asilimia 24, ingawa kwa kweli kilikuwa zaidi ya asilimia 400.

Kisha, amua njia ambayo utatumia kulipa madeni yako. Kwanza, unaweza kulipa deni lililo na kiwango cha juu zaidi cha riba. Njia nyingine ni kulipa madeni madogo kwanza, kwa kuwa huenda kupokea taarifa chache za matumizi kila mwezi kutakuchochea ujitahidi kulipa madeni. Ikiwa una mikopo yenye riba ya juu, huenda ukafaidika kwa kuchukua mkopo mwingine wenye riba ndogo ili kulipia ile mikopo mingine.

Mwishowe, ikiwa hutaweza kulipa, unaweza kuzungumza na wakopeshaji wako ili wabadili jinsi unavyowalipa. Unaweza kuomba wakupe muda zaidi au wapunguze riba. Baadhi ya wakopeshaji huwa tayari kupokea kiwango kidogo cha pesa wanachokudai ikiwa utalipa mara moja. Uwe mnyoofu na mwenye adabu katika kueleza hali yako ya kifedha. (Wakolosai 4:6; Waebrania 13:18) Andika makubaliano yoyote mtakayoafikiana. Ikiwa mwanzoni hawatakubali, uwe tayari kuendelea kuomba mabadiliko inapohitajika.—Methali 6:1-5.

Bila shaka, unapopangia pesa zako utahitaji kuona mambo kihalisi. Hata mpango unaoonekana kuwa mzuri kabisa huenda usifanikiwe kwa sababu ya hali ambazo huwezi kuzidhibiti, kwa kuwa mara nyingi pesa “hujifanyia mabawa kama yale ya tai na kuruka kuelekea mbinguni.”—Methali 23:4, 5.

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Ukimaliza kutayarisha bajeti ya kwanza, zungumzieni jinsi kila mmoja anavyoweza kupunguza gharama au kuongeza mapato ya familia. Kuona jinsi kila mmoja anavyojitahidi kunaweza kuwaunganisha mnapokabiliana na madeni.

TATIZO LA 3: Mawazo yetu hulemewa na madeni.

Jitihada za kukabiliana na madeni zinaweza kufanya tusahau mambo mengine muhimu ya maisha. Mwanamume anayeitwa Georgios anasema kuwa “tatizo kubwa ni kwamba tulielekeza fikira zetu zote kwenye madeni. Tulipuuza mambo tuliyopaswa kutanguliza.”

Siri ya kufanikiwa: Uwe na maoni yanayofaa kuhusu pesa.

Licha ya jitihada zako, huenda ukalipa madeni yako kwa miaka mingi. Kwa sasa, unaweza kuamua maoni utakayokuwa nayo kuhusu hali yako. Badala ya kufikiria kuhusu pesa kila wakati, ni jambo la hekima kufuata ushauri huu wa Biblia: “Tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.”—1 Timotheo 6:8.

Kuridhika huleta shangwe ambayo haiwezi kuletwa na mali

Ukiridhika na hali yako ya kifedha utakuwa na nafasi ya ‘kuhakikisha mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10) Mambo hayo “yaliyo ya maana zaidi” yanatia ndani urafiki wako pamoja na Mungu na familia yako. Georgios, aliyetajwa mapema anasema: “Ingawa hatujamaliza kulipa madeni yetu, hatuyakazii tena fikira zetu zote. Sasa ndoa yetu ni yenye furaha zaidi kwa sababu tunatumia muda mwingi zaidi pamoja na watoto wetu, tukiwa wenzi wa ndoa, na katika kufanya mambo ya kiroho.”

JARIBUNI KUFANYA HIVI: Orodhesha mambo unayothamini sana na ambayo pesa haziwezi kununua. Kisha, amua jinsi utakavyoongeza wakati na nguvu unazotumia katika kila jambo uliloorodhesha.

Matatizo yanayosababishwa na madeni hutokeza mkazo, na unahitaji kujidhabihu ili ukabiliane nayo; hata hivyo, kuna faida ya kufanya hivyo. Mume anayeitwa Andrzej kutoka Poland anakubali hivi: “Nilipotambua kwamba mke wangu alikuwa mdhamini wa mfanyakazi mwenzake aliyechukua mkopo mkubwa na ambaye baadaye alitoroka bila kulipa, hali ilikuwa mbaya nyumbani.” Hata hivyo, anapofikiria jinsi yeye na mke wake walivyoshughulikia hali hiyo, anasema: “Uhusiano wetu ulikuwa wa karibu zaidi, si kwa sababu ya tatizo hilo, bali kwa sababu tulishirikiana kulitatua.”

^ fu. 3 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 17 Kwa mapendekezo zaidi, ona mfululizo wa makala za kwanza wenye kichwa “Jinsi ya Kupangia Matumizi ya Pesa” kwenye gazeti la Amkeni! la Septemba 2011 lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

JIULIZE . . .

  • Ninawezaje kuisaidia familia yangu kulipa madeni?

  • Tunaweza kufanya nini ili madeni yasiwe jambo kuu maishani au kuharibu uhusiano wetu?