Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Ni kalamu na wino wa aina gani uliotumiwa nyakati za Biblia?

Kalamu zilizotengenezwa kwa mafunjo kutoka misri, yapata karne ya kwanza W.K.

Katika umalizio wa barua ya mwisho kati ya barua zake tatu zilizo katika Biblia, mtume Yohana alisema hivi: “Nilikuwa na mambo mengi ya kukuandikia, lakini sitaki kuendelea kukuandikia kwa wino na kalamu.” Tafsiri ya neno kwa neno ya Kigiriki cha kale ambacho Yohana alitumia inaonyesha kwamba hakutaka kuendelea kuandika kwa kutumia “[wino] mweusi na utete.”—3 Yohana 13, The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures.

Kalamu ya waandishi ilitengenezwa kwa utete mrefu na mgumu. Ulikatwa kutoka pembe moja hadi nyingine na ncha yake ilichongwa vizuri. Mwandishi angechonga tena ncha hiyo kwa kutumia jiwe la kukwaruzia. Utete huo ulifanana na kutumiwa kama kalamu za kisasa za wino zenye ncha ya chuma.

Aina nyingi za wino, au “mweusi,” zilikuwa mchanganyiko wa masizi ya jiko au taa na mpira wenye kunata, ambao ulitumiwa kama gundi. Wino huo uliuzwa ukiwa mkavu na kabla ya kutumiwa ulipaswa kuchanganywa na kiwango maalumu cha maji. Wino huo ulipotumiwa, ungeonekana tu juu mafunjo au ngozi na haukupenya upande wa pili. Hivyo, mwandishi angeweza kufuta kwa urahisi kosa lolote kwa kutumia sifongo yenye unyevunyevu, ambayo ilikuwa mojawapo ya vifaa muhimu vya mwandishi. Habari hizo kuhusu wino uliotumiwa zamani, zinaonyesha kile ambacho waandikaji wa Biblia walikuwa wakifikiria walipoandika kuhusu kuondolewa au kufutwa kwa majina kutoka katika kitabu cha kumbukumbu cha Mungu.—Kutoka 32:32, 33; Ufunuo 3:5, Kingdom Interlinear.

Mtume Paulo alitengeneza mahema ya aina gani?

Vifaa vya kushona vya karne ya kwanza au ya pili W.K.

Andiko la Matendo 18:3, linasema kwamba mtume Paulo alikuwa fundi wa kutengeneza mahema. Katika nyakati za Biblia, watu waliotengeneza mahema walifuma manyoya ya ngamia au ya mbuzi ili kutokeza vipande vya nguo. Kisha, wangeunganisha vipande hivyo ili kufanyiza mahema kwa ajili ya wasafiri. Hata hivyo, mahema mengi ya nyakati hizo, yalifanyizwa kutokana na ngozi. Mengine yalifanyizwa kutokana na kitambaa cha kitani, kilichotengenezwa Tarso, mji wa nyumbani wa Paulo. Huenda Paulo aliwahi kutumia mojawapo ya vitu hivyo au vyote. Hata hivyo, Paulo alipofanya kazi na Akila, huenda alitengeneza miavuli ya jua ambayo ilitumiwa kufunika sehemu ya katikati ya nyumba za kibinafsi.

Yaelekea Paulo alijifunza kazi hiyo alipokuwa mvulana. Uthibitisho kutoka katika vitabu vya kukunjwa vya Misri unaonyesha kwamba wakati wa utawala wa Waroma, wanafunzi huko Misri walianza kujifunza kazi za ufundi wakiwa na umri wa miaka 13 hivi. Ikiwa Paulo alijifunza ufundi akiwa na umri huo, basi kufikia umri wa miaka 15 au 16, huenda alijua vizuri kukata vitambaa kwa kipimo na umbo linalofaa, kisha kuvishona kwa ufundi akitumia aina mbalimbali za sindano. “Mwishoni mwa masomo yake huenda Paulo alikuwa na vifaa vyote kwa ajili ya ufundi,” kinasema kitabu The Social Context of Paul’s Ministry. “Visu alivyohitaji na sindano,” kinaendelea kusema kitabu hicho, “zilifanya kazi hiyo iwe rahisi kubeba na kuifanya mahali popote,” kazi iliyomtegemeza Paulo akiwa mmishonari anayesafiri.