Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, UNGEPENDA KUJIFUNZA BIBLIA?

Kwa Nini Ujifunze Biblia?

Kwa Nini Ujifunze Biblia?
  • Ni nini kusudi la maisha?

  • Kwa nini wanadamu wanateseka na kufa?

  • Ni nini kitakachotokea wakati ujao?

  • Je, Mungu ananijali?

Je, umewahi kujiuliza maswali kama hayo? Ikiwa ndivyo, hauko peke yako. Ulimwenguni pote watu wanajiuliza maswali muhimu kuhusu maisha. Je, unaweza kupata majibu?

Huenda mamilioni ya watu wakajibu, “Ndiyo!” Kwa nini? Kwa sababu wamepata majibu yenye kuridhisha ya maswali yao katika Biblia. Je, ungependa kujua kile ambacho Biblia inasema? Basi, utanufaika zaidi kwa kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova bila malipo. *

Ni kweli kwamba inapohusu kujifunza Biblia, baadhi ya watu husema: “Nina shughuli nyingi.” “Biblia haieleweki.” “Ninaogopa kuahidi kwamba nitapatikana ili kujifunza.” Hata hivyo, wengine wana maoni tofauti. Wanakubali kujifunza kile ambacho Biblia inafundisha. Fikiria mifano michache:

  • “Nilishirikiana na makanisa ya Kikatoliki na Kiprotestanti, hekalu la Kalasinga, makao ya watawa Wabudha, na nilisomea theolojia katika chuo kikuu. Hata hivyo, maswali yangu mengi kuhusu Mungu hayakujibiwa. Kisha, Shahidi wa Yehova alinitembelea nyumbani. Nilikubali kujifunza Biblia baada ya dada huyo kujibu maswali yangu kwa kutumia Biblia.”—Gill, Uingereza.

  • “Nilikuwa na maswali mengi kuhusu maisha, lakini majibu ya mchungaji wangu hayakuniridhisha. Hata hivyo, Shahidi wa Yehova alijibu maswali yangu kwa kutumia Biblia tu. Aliponiuliza ikiwa ningependa kujifunza mengi zaidi, nilikubali mara moja.”—Koffi, Benin.

  • “Nilitaka sana kujua kinachopata watu wanapokufa. Niliamini kwamba wafu wanaweza kudhuru walio hai, lakini nilitaka kujua kile ambacho Biblia inasema. Hivyo, rafiki yangu ambaye ni Shahidi alianza kunifundisha Biblia.”—José, Brazili.

  • “Nilijaribu kuisoma Biblia lakini sikuielewa. Kisha, Mashahidi wa Yehova walinitembelea na kunifafanulia vizuri unabii unaopatikana katika Biblia. Baada ya hapo, nilitaka kujifunza mengi zaidi.”—Dennize, Mexico.

  • “Nilifikiria sana ikiwa kwa kweli Mungu ananijali. Hivyo, nikaamua kusali kwa Mungu anayetajwa katika Biblia. Siku iliyofuata, Mashahidi walinitembelea nyumbani kwangu, nami nikakubali funzo la Biblia.”—Anju, Nepal.

Masimulizi hayo yanatukumbusha maneno haya ya Yesu: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” (Mathayo 5:3) Naam, kiasili wanadamu wana uhitaji wa kumjua Mungu. Ni Mungu tu anayeweza kutimiza uhitaji huo, na anafanya hivyo kupitia Neno lake, Biblia.

Hata hivyo, funzo la Biblia linahusisha nini? Litakunufaishaje? Maswali hayo yatajibiwa katika makala inayofuata.

^ fu. 8 Biblia inasema kwamba jina la Mungu ni Yehova.