Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

BIBLIA INABADILI MAISHA

Maswali Matatu Yalibadili Maisha Yangu

Maswali Matatu Yalibadili Maisha Yangu
  • ALIZALIWA: 1949

  • NCHI: MAREKANI

  • HISTORIA: ALITAFUTA KUSUDI LA MAISHA

MAISHA YANGU YA ZAMANI:

Nililelewa katika mji mdogo unaoitwa Ancram, kaskazini mwa jiji la New York, Marekani. Wenyeji wa mji huo walikuwa wafugaji wa ng’ombe wa maziwa. Mji huo ulikuwa na ng’ombe wengi kuliko watu.

Familia yetu ilihudhuria kanisa pekee lililokuwa katika mji huo. Jumapili asubuhi, Babu angeng’arisha viatu vyangu na kisha ningeenda kuhudhuria shule ya Biblia ya watoto iliyofanywa kila Jumapili, nikiwa na Biblia yangu ndogo yenye jalada jeupe niliyopewa na nyanya yangu. Mimi na ndugu zangu tulifundishwa kufanya kazi kwa bidii, kuheshimu na kusaidia majirani zetu, na kuwa wenye shukrani kwa baraka tulizonazo.

Nilipokuwa mtu mzima, nilihama nyumbani na kufanya kazi ya ualimu. Nilikuwa na maswali mengi kuhusu Mungu na maisha. Baadhi ya wanafunzi wangu walikuwa na vipaji. Wengine hawakuwa na vipaji lakini walikuwa na bidii. Wengine walikuwa walemavu huku wengine hawakuwa na ulemavu wowote. Niliiona hali hiyo kuwa ukosefu wa haki. Pindi fulani, wazazi wa wanafunzi ambao hawakuwa na vipaji walisema mambo kama vile, “Hivi ndivyo Mungu alivyotaka mtoto wangu awe.” Nilijiuliza ni kwa nini Mungu aliruhusu watoto wengine wazaliwe wakiwa na ulemavu. Nilihisi hivyo kwa sababu nilijua kwamba mtoto huzaliwa bila dhambi yoyote.

Nilijiuliza hivi pia: ‘Ni jambo gani la maana ninalopaswa kufanya maishani?’ Nilihisi kwamba umri wangu unasonga haraka. Nililelewa katika familia nzuri, nilisoma katika shule zilizotoa elimu bora, na nilikuwa nafanya kazi niliyoipenda. Hata hivyo, bado sikuwa na kusudi maishani. Nilitarajia kufunga ndoa, kuwa na nyumba nzuri na kuzaa watoto, kufanya kazi mpaka nitakapostaafu na hatimaye kuhamia katika nyumba ya kutunza wazee. Nilijiuliza ikiwa maisha yana kusudi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU:

Pindi moja katika majira ya kiangazi, mimi na walimu wenzangu tulitembelea Ulaya. Tulitembelea Westminster Abbey, Notre-Dame de Paris, Vatikani, na makanisa mengine mengi madogo. Kila kanisa nililotembelea, niliuliza maswali yaliyonisumbua. Baada ya kurudi nyumbani katika mji wa Sloatsburg, New York, niliendelea kutembelea makanisa kadhaa. Hata hivyo, sikupata majibu yenye kuridhisha.

Siku moja, mwanafunzi wangu mwenye umri wa miaka 12, alinifuata na kuniuliza maswali matatu. Aliniuliza kwanza ikiwa ninajua kwamba yeye ni Shahidi wa Yehova. Nikamjibu ndiyo. Kisha, akaniuliza ikiwa ningependa kujua mengi zaidi kuhusu Mashahidi wa Yehova. Nikasema ndiyo. Tatu, akataka kujua ninapoishi. Nilipomwambia ninapoishi, tuligundua kwamba nyumba yangu ilikuwa karibu tu na nyumba yao. Sikuwazia kwamba maswali hayo matatu niliyoulizwa na msichana huyo mdogo yangebadili maisha yangu milele.

Muda mfupi baadaye, alikuja kwa baiskeli nyumbani kwangu na kuanza kunifundisha Biblia. Nilimuuliza maswali niliyowauliza viongozi wengi wa dini. Tofauti na viongozi hao, msichana huyo alinionyesha majibu yaliyo wazi na yenye kuridhisha akitumia Biblia yangu mwenyewe. Hatimaye, nilipata majibu ya maswali yangu!

Yale niliyojifunza kutoka katika Biblia yalinipa shangwe nyingi na uradhi. Niliguswa sana moyoni niliposoma andiko la 1 Yohana 5:19, linalosema hivi: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Nilifarijika kujifunza kwamba si Mungu anayesababisha mateso tunayoona leo ulimwenguni bali ni Shetani. Na kwamba Mungu ataondoa hali hiyo. (Ufunuo 21:3, 4) Niligundua pia kwamba Biblia hueleweka vizuri ikifafanuliwa wazi. Ingawa Shahidi aliyenifundisha alikuwa na umri wa miaka 12 tu, nilitambua kwamba kweli itaendelea kuwa kweli bila kujali ni nani anayesema kuihusu.

Hata hivyo, nilitaka kuona ikiwa Mashahidi wanaishi kulingana na mafundisho yao. Kwa mfano, msichana huyo mdogo alinifundisha kwamba Wakristo wa kweli wanapaswa kuonyesha sifa kama vile ustahimilivu na fadhili. (Wagalatia 5:22, 23) Hivyo, niliamua kumjaribu ili nione ikiwa ana sifa hizo. Siku moja, nilichelewa kimakusudi kwa ajili ya funzo. Niliwaza hivi: ‘Ataningojea kweli? Na hata kama ataningoja, atakasirika kwa kuwa nimechelewa?’ Nilipokuwa naegesha gari langu, nilimwona akiwa ameketi katika ngazi za nyumba yangu akinisubiri. Akanifuata mara moja nikiwa bado ndani ya gari yangu na kusema: “Ilikuwa bado kidogo niende nyumbani kumwambia mama yangu tupige simu hospitali na polisi, ili kujua ikiwa uko salama kwa kuwa si kawaida yako kuchelewa kwa ajili ya funzo letu. Nilikuwa na wasiwasi sana!”

Katika pindi nyingine, nilimuuliza swali ambalo nilihisi kwamba haingekuwa rahisi kwa mtu mwenye umri wa miaka 12 kujibu. Nilitaka kuona ikiwa atabuni jibu. Nilipomuuliza swali hilo, alinitazama kwa makini na kusema: “Hilo ni swali gumu. Nitaliandika na kisha nitawauliza wazazi wangu.” Na kwa kweli, aliporudi pindi iliyofuata kwa ajili ya funzo, alileta gazeti la Mnara wa Mlinzi lililokuwa na jibu la swali nililouliza. Na hilo ndilo jambo lililonifanya nivutiwe na Mashahidi, yaani, machapisho yao yalirejelea Biblia ili kujibu maswali yangu yote. Msichana huyo mdogo aliendelea kunifundisha, na baada ya mwaka mmoja nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. *

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA:

Baada ya kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali yangu, nilitaka kuwaambia wengine. (Mathayo 12:35) Mwanzoni, familia yangu ilipinga imani yangu mpya. Hata hivyo, baada ya muda walibadili mtazamo wao. Mama yangu alianza kujifunza Biblia muda mfupi kabla ya kifo chake. Ingawa alikufa kabla ya kubatizwa, nina uhakika kwamba tayari alikuwa ameazimia kumtumikia Yehova.

Mwaka wa 1978, nilifunga ndoa na Shahidi mwenzangu, Elias Kazan. Katika mwaka wa 1981, mimi na Elias tulialikwa ili kutumika tukiwa Wanabetheli katika Betheli ya Marekani. * Nilisikitika sana Elias alipokufa baada ya kutumika naye Betheli kwa miaka minne tu. Ingawa nilikuwa mjane, niliendelea na mgawo wangu wa Betheli ulionisaidia kuwa na jambo la muhimu la kufanya na kunipatia faraja.

Mwaka wa 2006, nilifunga ndoa na Richard Eldred, ambaye ni Mwanabetheli pia. Mimi na Richard bado tunafurahia pendeleo la kutumika Betheli. Kujua kweli kuhusu Mungu kumenifanya nihisi kwamba nimepata si majibu tu ya maswali niliyokuwa nayo, bali pia kusudi halisi la maisha, yote hayo kwa sababu ya maswali matatu niliyoulizwa na msichana mdogo.

^ fu. 16 Kwa kuongezea, msichana huyo na ndugu zake walijifunza Biblia na walimu wao watano, nao wakaanza kumwabudu Yehova.

^ fu. 18 Neno “Betheli,” linamaanisha “Nyumba ya Mungu,” nalo hutumiwa na Mashahidi wa Yehova kumaanisha ofisi zao za tawi ulimwenguni pote. (Mwanzo 28:17, 19) Wanabetheli hufanya kazi mbalimbali zinazotegemeza kazi ya elimu ya Mashahidi wa Yehova.