Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Tunaweza Kumjua Mungu?

Je, Kweli Tunaweza Kumjua Mungu?

“Mungu hajulikani.” —Philo wa Aleksandria, mwanafalsafa wa karne ya kwanza.

“[Mungu] hayuko mbali nasi.” —Sauli wa Tarso, alipowahutubia wanafalsafa wa jiji la Athene katika karne ya kwanza.

UNAKUBALIANA na sentensi ipi kati ya hizo mbili? Wengi wamefarijika na kuvutiwa na maneno ya Sauli wa Tarso, anayeitwa pia mtume Paulo. (Matendo 17:26, 27) Biblia inatupatia uhakikisho mwingi. Kwa mfano, Yesu alitoa sala iliyowahakikishia wafuasi wake kwamba wangeweza kumjua Mungu na kubarikiwa.—Yohana 17:3.

Hata hivyo, wanafalsafa kama Philo wana maoni tofauti. Wanadai kwamba hatuwezi kabisa kumjua Mungu kwa kuwa hajulikani. Ukweli wa mambo ni nini?

Biblia inasema wazi kwamba tukiwa wanadamu hatuwezi kuelewa mambo fulani kuhusu Mungu. Kwa mfano, muda ambao Muumba amekuwepo, uwezo wa akili yake, na hekima yake, haiwezi kupimwa, kuhesabiwa, au kuchunguzwa. Akili ya mwanadamu haiwezi kujua mambo hayo. Hata hivyo, uwezo huo wa Mungu hautuzuii kumjua. Zaidi ya hilo, kutafakari mambo hayo kunaweza kutusaidia ‘kumkaribia Mungu.’ (Yakobo 4:8) Acheni tuchunguze mifano michache ya mambo hayo yasiyoeleweka. Kisha, tutachunguza yale tunayoweza kujifunza kuhusu Mungu kutokana na mambo hayo.

Ni Mambo Gani Yasiyoeleweka?

UMILELE WA MUNGU: Biblia inafundisha kwamba Mungu amekuwapo “tangu wakati usio na kipimo mpaka wakati usio na kipimo.” (Zaburi 90:2) Kwa maneno mengine, Mungu hana mwanzo wala hatakuwa na mwisho. Kwa maoni ya mwanadamu, “hesabu ya miaka yake haichunguziki.”—Ayubu 36:26.

Jinsi unavyonufaika: Mungu anakuahidi uzima wa milele ukijitahidi kabisa kumjua. (Yohana 17:3) Je, ungeamini ahadi hiyo ikiwa Mungu mwenyewe hangeishi milele? Ni “Mfalme wa umilele” tu anayeweza kutimiza ahadi hiyo.—1 Timotheo 1:17.

AKILI YA MUNGU: Biblia inafundisha kwamba “haiwezekani kuchunguza kikamilifu uelewaji wake,” kwa kuwa mawazo yake yako juu sana kuliko yetu. (Isaya 40:28; 55:9) Hivyo, Biblia inauliza swali hili: “Ni nani ameijua akili ya Yehova, ndipo amfundishe?”—1 Wakorintho 2:16.

Jinsi unavyonufaika: Mungu anaweza kusikiliza sala zinazotolewa kwa wakati mmoja na mamilioni ya watu. (Zaburi 65:2) Hata anatambua kila shomoro anayeanguka chini. Je, kuna wakati ambapo Mungu atakuwa na mambo mengi sana ya kufikiria hivi kwamba ashindwe kusikiliza sala zako? Hapana, kwa kuwa akili yake haina mipaka. Zaidi ya yote, machoni pa Mungu, ‘wewe ni bora kuliko shomoro wengi.’—Mathayo 10:29, 31.

NJIA ZA MUNGU: Biblia inafundisha kwamba mwanadamu ‘hawezi kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.’ (Mhubiri 3:11) Kwa hiyo, hatutajua kila kitu kuhusu Mungu. Hekima ya njia za Mungu ‘haitafutiki.’ (Waroma 11:33) Hata hivyo, Mungu yuko tayari kufunua njia zake kwa wale wanaotaka kumpendeza.—Amosi 3:7.

Muda ambao Muumba amekuwepo, uwezo wa akili yake, na hekima yake, haiwezi kupimwa, kuhesabiwa, au kuchunguzwa

Jinsi unavyonufaika: Utaendelea kujifunza mambo mapya kuhusu Mungu na njia zake ikiwa utasoma na kujifunza Biblia. Jambo hilo linaonyesha kwamba tunaweza kumkaribia zaidi Baba yetu wa mbinguni kwa umilele wote.

Unachoweza Kujua

Kutoelewa vizuri habari fulani kuhusu Mungu hakumaanishi kwamba hatuwezi kumjua kabisa. Biblia ina habari nyingi zinazotusaidia kumjua vizuri Mungu. Fikiria mifano ifuatayo:

JINA LA MUNGU: Biblia inatufundisha kwamba Mungu amejipa jina. Anasema hivi: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” Jina la Mungu linapatikana mara 7,000 hivi katika Biblia, mara nyingi zaidi ya jina lingine lolote.—Isaya 42:8.

Jinsi unavyonufaika: Yesu alisema hivi katika sala yake ya mfano: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kwa nini usitumie jina la Mungu katika sala zako? Yehova yuko tayari kumwokoa kila mtu anayeliheshimu jina lake.—Waroma 10:13.

MAKAO YA MUNGU: Biblia inafundisha kwamba kuna “makao” ya aina mbili—makao ya kiroho ambamo viumbe wa roho walio na miili ya kiroho wanaishi na makao halisi yanayotia ndani dunia na sayari. (Yohana 8:23; 1 Wakorintho 15:44) Katika Biblia, mara nyingi neno “mbingu” hurejelea makao ya kiroho. “Makao” ya Muumba yako “mbinguni.” —1 Wafalme 8:43.

Jinsi unavyonufaika: Inakusaidia kumwelewa vizuri Mungu. Muumba si nguvu isiyoeleweka inayopatikana kila mahali na katika kila kitu. Yehova ni Mtu halisi anayeishi katika eneo halisi. Pamoja na hayo, “hakuna kiumbe kisichokuwa wazi machoni pake.”—Waebrania 4:13.

UTU WA MUNGU: Biblia inafundisha kwamba Yehova ana sifa zenye kuvutia. “Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Hasemi uwongo. (Tito 1:2) Hana ubaguzi, ni mwenye rehema, neema, na si mwepesi wa hasira. (Kutoka 34:6; Matendo 10:34) Pia, Muumba anatamani kuwa na “urafiki wa karibu” na wale wanaomheshimu; jambo ambalo huenda likawashangaza watu wengi.—Zaburi 25:14.

Jinsi unavyonufaika: Unaweza kuwa rafiki ya Yehova. (Yakobo 2:23) Kadiri utakavyozidi kujua utu wa Yehova ndivyo utakavyoelewa vizuri zaidi masimulizi ya Biblia.

“MTAFUTE”

Biblia inamfafanua vizuri Yehova Mungu. Muumba anataka umjue kwa kuwa inawezekana kufanya hivyo. Neno lake Biblia linaahidi hivi: “Ukimtafuta, ataacha umpate.” (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Kwa nini usianze kumjua Mungu kwa kusoma na kutafakari masimulizi ya Biblia? Ukifanya hivyo, Biblia inaahidi kwamba Mungu ‘atakukaribia.’—Yakobo 4:8.

Utaendelea kujifunza mambo mapya kuhusu Mungu na njia zake ikiwa utasoma na kujifunza Biblia

Huenda ukawaza hivi, ‘Ninawezaje kuwa rafiki ya Muumba ikiwa siwezi kujua mambo yote kumhusu?’ Fikiria jambo hili: Je, ni lazima rafiki wa karibu wa daktari mpasuaji awe na shahada ya upasuaji? La hasha! Huenda rafiki ya daktari huyo akawa na kazi tofauti. Hata hivyo, wanaweza kuwa marafiki wa karibu. Jambo la muhimu ni kwamba rafiki ya daktari anajua utu, mambo anayopenda na asiyopenda. Vivyo hivyo, unaweza kujifunza kuhusu utu wa Yehova katika Biblia—jambo unalohitaji kujua ili uwe rafiki yake.

Biblia haielezi tu kwa ufupi kuhusu Muumba. Ina habari muhimu tunazohitaji ili kumjua Mungu. Je, ungependa kujifunza mengi zaidi kumhusu Yehova Mungu? Mashahidi wa Yehova hufundisha watu Biblia bila malipo. Unaweza kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova katika eneo lako au kutembelea tovuti yetu ya www.dan124.com/sw.