Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kilio cha Haki Kitasikika?

Je, Kilio cha Haki Kitasikika?

 Inaonekana ukosefu wa haki umeenea kila mahali. Fikiria mifano miwili ya watu waliohukumiwa isivyo haki:

  •   Mnamo Januari 2018, hakimu nchini Marekani aliamuru mwanamume fulani aliyefungwa miaka 38 hivi iliyopita awekwe huru. Ilionekana hakuwa na hatia kwa msingi wa uthibitisho wa chembe za urithi (DNA).

  •   Mnamo Septemba 1994, vijana watatu katika nchi moja ya Afrika walifungwa kwa sababu walikataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Kufikia Septemba 2020, walikuwa wamefungwa gerezani kwa miaka 26 bila hata kushtakiwa au kufikishwa mahakamani kwa uhalifu wanaodaiwa kuwa walifanya.

 Ikiwa umekabili ukosefu wa haki, huenda ukahisi kama Ayubu aliyeishi katika nyakati za Biblia aliyesema: “Naendelea kulilia msaada, lakini hakuna haki.” (Ayubu 19:7) Hata hivyo, ingawa huenda ikaonekana kwamba kupata haki ya kweli ni ndoto, Biblia inaahidi wakati ambapo kilio cha haki kitasikika. Isitoshe, hekima yake inaweza kukusaidia kukabiliana na ukosefu wa haki sasa hivi.

Ni nini husababisha ukosefu wa haki?

 Ukosefu wa haki husababishwa na wale wanaokataa mwongozo wa Mungu. Biblia inaonyesha kwamba haki ya kweli inatoka kwa Mungu. (Isaya 51:4) Katika Biblia, maneno yanayotafsiriwa “haki” na “uadilifu” yana uhusiano wa karibu. (Zaburi 33:5) Matendo ya uadilifu, au yaliyo mema na yanayofaa kulingana na viwango vya Mungu, hutokeza haki. Tofauti na hilo, ukosefu wa haki hutokana na dhambi, ambayo ni kuvunja viwango vya uadilifu vya Mungu. Fikiria mifano ifuatayo:

  •   Ubinafsi. Tamaa yenye ubinafsi na dhambi zina uhusiano wa karibu. (Yakobo 1:14, 15) Ili kupata wanachotaka, watu wengi huwatumia wengine vibaya kwa kuwatendea bila haki. Tofauti na hilo, Mungu anataka tutangulize faida za wengine.—1 Wakorintho 10:24.

  •   Kutojua. Huenda wengine wakawatendea wenzao kwa ukosefu wa haki bila kutambua, hata hivyo, kwa maoni ya Mungu matendo kama hayo ni dhambi. (Waroma 10:3) Kwa kweli, kutojua kuliongoza kwenye tendo la ukosefu mkubwa zaidi wa haki—kuuawa kwa Yesu Kristo.—Matendo 3:15, 17.

  •   Mifumo ya kibinadamu iliyoshindwa. Mifumo ya kisiasa, kiuchumi, na ya kidini ulimwenguni inadai kwamba hiyo inawachochea watu kutendeana kwa haki. Hata hivyo, ukweli ni kwamba mifumo hiyo ni chanzo cha makosa, ufisadi, ubaguzi, pupa, tofauti kubwa za kiuchumi, na kutovumiliana. Mambo yote hayo yanaweza kutokeza ukosefu wa haki. Baadhi ya mifumo hiyo imetokezwa na watu walio na nia nzuri. Lakini kimsingi, jitihada zote za wanadamu zinazopuuza mwongozo wa Mungu haziwezi kufanikiwa.—Mhubiri 8:9; Yeremia 10:23.

Je, Mungu anajali kuhusu ukosefu wa haki?

 Ndiyo, anachukia ukosefu wa haki na mitazamo na matendo yanayoutokeza. (Methali 6:16-18) Alimwongoza nabii Isaya kwa roho yake kuandika hivi: “Mimi, Yehova, a ninapenda haki; ninachukia unyang’anyi na ukosefu wa uadilifu.”—Isaya 61:8.

 Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli wa kale ilionyesha kwamba alitaka watu watende kwa haki. Aliwaamuru waamuzi wao wakatae rushwa na matendo mengine ambayo yangepotosha haki. (Kumbukumbu la Torati 16:18-20) Aliwashutumu Waisraeli kwa sababu walikosa kumtii na wakawadhulumu maskini na watu wa hali ya chini, naye aliwakataa kwa sababu walishindwa kushikamana na viwango vyake.—Isaya 10:1-3.

Je, Mungu atakomesha ukosefu wa haki?

 Ndiyo. Kupitia Yesu Kristo, Mungu ataondoa dhambi, chanzo cha ukosefu wa haki, na kuwafanya wanadamu kuwa wakamilifu. (Yohana 1:29; Waroma 6:23) Pia, ameusimamisha Ufalme ambao utaleta ulimwengu mpya wenye uadilifu na kufanya haki ya kweli ipatikane kwa kila mtu. (Isaya 32:1; 2 Petro 3:13) Ili kujifunza mengi zaidi kuhusu Ufalme huo wa mbinguni, tazama video yenye kichwa Ufalme wa Mungu Ni Nini?

Maisha yatakuwaje katika ulimwengu mpya wenye uadilifu?

 Haki itakapojaa duniani, matokeo yatakuwa amani na usalama kwa kila mtu. (Isaya 32:16-18) Mungu anauona uhai wote kuwa wenye thamani, kwa hiyo, wote watatendewa bila ubaguzi. Huzuni, kilio, na maumivu yanayotokana na ukosefu wa haki yataondolewa milele, na hata kumbukumbu zenye uchungu za kutendewa kwa njia isiyo ya haki zitapita hatimaye. (Isaya 65:17; Ufunuo 21:3, 4) Kwa habari zaidi, ona makala yenye kichwa “Ufalme wa Mungu Utatimiza Nini?

Je, unaweza kuamini ahadi ya Mungu ya kuishi katika ulimwengu usio na ukosefu wa haki?

 Ndiyo. Biblia imethibitika kuwa kitabu cha unabii wa kweli, usahihi wa kihistoria na wa kisayansi, na kinachopatana, na mambo hayo yanatuonyesha kwamba tunaweza kuamini ahadi zake. Makala zinazofuata zinaandaa habari zaidi:

Vipi kuhusu kupigana na ukosefu wa haki sasa?

 Watu katika nyakati za Biblia walipinga ukosefu wa haki. Kwa mfano, mtume Paulo alishtakiwa isivyo haki na kufunguliwa kesi ambayo ingemfanya auawe. Badala ya kukubali tu ukosefu huo wa haki, alitumia njia za kisheria zilizopatikana na kukata rufaa kwa Kaisari.—Matendo 25:8-12.

 Hata hivyo, jitihada za wanadamu kurekebisha ukosefu wote wa haki katika ulimwengu huu zitashindwa. (Mhubiri 1:15) Lakini wengi wamegundua kwamba kuwa na imani katika ahadi ya Mungu ya ulimwengu mpya wenye uadilifu kumewasaidia kupata utulivu wa ndani na amani ya akili licha ya ukosefu wa haki.

a Yehova ndilo jina la kibinafsi la Mungu.—Zaburi 83:18.