Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 57

Yesu Amponya Msichana na Mwanamume Kiziwi

Yesu Amponya Msichana na Mwanamume Kiziwi

MATHAYO 15:21-31 MARKO 7:24-37

  • YESU AMPONYA BINTI YA MWANAMKE MFOINIKE

  • AMPONYA MWANAMUME ALIYE KIZIWI NA BUBU

Baada ya kuwashutumu Mafarisayo kwa sababu ya desturi zao za kibinafsi, Yesu anaondoka pamoja na wanafunzi wake. Anaelekea kwenye eneo la Tiro na Sidoni huko Foinike, kilomita nyingi upande wa kaskazini magharibi.

Yesu anapata makao katika nyumba fulani lakini hataki watu wajue kwamba yuko huko. Ingawa hivyo, hata huku hawezi kujificha. Mwanamke fulani mwenye asili ya Ugiriki aliyezaliwa katika eneo hili anampata Yesu na kuanza kumsihi: “Nihurumie, Bwana, Mwana wa Daudi. Binti yangu anasumbuliwa kikatili na roho mwovu.”—Mathayo 15:22; Marko 7:26.

Baada ya muda wanafunzi wa Yesu wanamsihi: “Mwambie aende, kwa sababu anaendelea kutufuata akipaza sauti.” Yesu anajibu kwa kueleza sababu inayofanya ampuuze: “Sikutumwa kwa yeyote isipokuwa kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” Hata hivyo, yule mwanamke hafi moyo. Anakaribia na kuanguka mbele za Yesu, akimsihi: “Bwana, nisaidie!”—Mathayo 15:23-25.

Labda ili kujaribu imani ya mwanamke huyo, Yesu anataja maoni yasiyofaa ya Wayahudi kuelekea watu wa mataifa mengine: “Haifai kuuchukua mkate wa watoto na kuwatupia mbwa wadogo.” (Mathayo 15:26) Kwa kuwataja “mbwa wadogo,” au watoto wa mbwa, Yesu anafunua hisia zake nyororo kuelekea watu wasio Wayahudi. Vilevile uso wake na sauti yake yenye huruma inaonyesha hisia hizo.

Badala ya kuudhika, yule mwanamke pia anazungumzia ubaguzi wa Wayahudi na kwa unyenyekevu anasema: “Ndiyo Bwana, lakini hata hao mbwa wadogo hula makombo yanayoanguka kutoka kwenye meza ya mabwana wao.” Yesu anatambua hali yake nzuri ya moyoni na kusema: “Ewe mwanamke, imani yako ni kubwa; na itendeke kama unavyotaka.” (Mathayo 15:27, 28) Na inatukia hivyo, hata ingawa msichana huyo hayuko hapo! Yule mwanamke anaporudi nyumbani, anamkuta binti yake akiwa amelala kitandani, akiwa amepona kabisa—“yule roho mwovu alikuwa amemtoka”!—Marko 7:30.

Baada ya kutoka eneo la Foinike, Yesu na wanafunzi wake wanavuka nchi kuelekea sehemu ya juu ya Mto Yordani. Inaelekea wanavuka Yordani sehemu fulani iliyo upande wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya na kwenda kwenye eneo la Dekapoli. Wakiwa huko, wanapanda mlima fulani, lakini umati unawapata. Watu wanamletea Yesu viwete, vilema, vipofu, na mabubu. Wanawalaza wagonjwa hao miguuni pa Yesu, naye anawaponya. Wakiwa wameshangaa, watu hao wanamtukuza Mungu wa Israeli.

Yesu anamkazia fikira mtu fulani aliye kiziwi na bubu. Unaweza kuelewa jinsi anavyohisi akiwa katika umati mkubwa. Labda akitambua jinsi mtu huyo alivyo na wasiwasi, Yesu anampeleka mbali na umati. Wakiwa peke yao, Yesu anamwonyesha jambo atakalomfanyia. Anaweka vidole vyake katika masikio ya mtu huyo, na baada ya kutema mate, anaugusa ulimi wa mtu huyo. Kisha akitazama mbinguni, Yesu anasema maneno fulani ya Kiyahudi yanayomaanisha “Funguka.” Papo hapo, yule mtu anaanza kusikia, na kuanza kuzungumza vizuri. Yesu hataki jambo hilo litangazwe, angependa watu wamwamini kwa kutegemea mambo wanayojionea na kusikia wenyewe.—Marko 7:32-36.

Uwezo wa Yesu wa kuponya kwa njia hiyo unawachochea sana watazamaji, ambao ‘wanashangaa sana.’ Wanasema: “Amefanya mambo yote vema. Hata anafanya viziwi wasikie na wasio na uwezo wa kusema, wazungumze.”—Marko 7:37.