Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 71

Mafarisayo Wamhoji Mtu Aliyekuwa Kipofu

Mafarisayo Wamhoji Mtu Aliyekuwa Kipofu

YOHANA 9:19-41

  • MAFARISAYO WAMHOJI MTU ALIYEKUWA KIPOFU

  • VIONGOZI WA KIDINI NI “VIPOFU”

Mafarisayo hawaamini kwamba Yesu alimwezesha mtu aliyezaliwa kipofu kuona, basi wanawaita wazazi wake. Wazazi hao wanajua kwamba wanakabili uwezekano wa ‘kufukuzwa katika sinagogi.’ (Yohana 9:22) Kukatishwa huko kwa ushirikiano pamoja na Wayahudi wengine kungekuwa na matokeo mabaya kijamii na kifedha kwa familia hiyo.

Mafarisayo wanauliza maswali mawili: “Je, huyu ni mwana wenu ambaye mnasema alizaliwa kipofu? Basi, imekuwaje kwamba sasa anaona?” Wazazi wake wanajibu: “Tunajua kwamba huyu ni mwana wetu na alizaliwa akiwa kipofu. Lakini hatujui jinsi alivyoanza kuona, wala hatujui mtu aliyemfungua macho.” Hata kama mwana wao alikuwa amewaambia kilichofanyika, wazazi wanajibu kwa tahadhari na kusema: “Muulizeni. Yeye ni mtu mzima. Anaweza kujieleza.”—Yohana 9:19-21.

Basi, Mafarisayo wanamwita tena yule mtu na kumtisha kwa kudai kwamba wana ushahidi dhidi ya Yesu. “Mpe Mungu utukufu,” wanadai. “Tunajua mtu huyu ni mtenda dhambi.” Yule mtu aliyekuwa kipofu anahepa madai yao akisema: “Kama yeye ni mtenda dhambi mimi sijui.” Kisha anasema: “Ninachojua ni kwamba nilikuwa kipofu, lakini sasa ninaona.”—Yohana 9:24, 25.

Wakitaka kuendeleza mazungumzo hayo Mafarisayo wanauliza: “Alikufanyia nini? Aliyafunguaje macho yako?” Yule mtu anaonyesha ujasiri anapojibu hivi: “Tayari nimewaambia, lakini hamkusikiliza. Kwa nini mnataka kusikia tena? Je, ninyi pia mnataka kuwa wanafunzi wake?” Wakiwa wamekasirika, Mafarisayo wanamshutumu hivi: “Wewe ni mwanafunzi wa mtu huyo, lakini sisi ni wanafunzi wa Musa. Tunajua kwamba Mungu alizungumza na Musa; lakini mtu huyu, hatujui alikotoka.”—Yohana 9:26-29.

Yule mtu anasema hivi kwa mshangao: “Kwa kweli inashangaza kwamba hamjui alikotoka, ingawa ndiye aliyefungua macho yangu.” Kisha mtu huyo anasema jambo linalopatana na akili kuhusu mtu ambaye Mungu humsikiliza na kumkubali: “Tunajua kwamba Mungu hawasikilizi watenda dhambi, lakini humsikiliza mtu yeyote anayemwogopa na kufanya mapenzi yake. Tangu zamani haijasikiwa kamwe mtu yeyote ameyafungua macho ya mtu aliyezaliwa kipofu.” Kisha anafikia kauli hii: “Kama mtu huyu hakutoka kwa Mungu, hangeweza kufanya lolote.”—Yohana 9:30-33.

Wanaposhindwa kupinga sababu za mtu huyo, Mafarisayo wanamtukana wakisema: “Wewe ulizaliwa katika dhambi, na bado unajaribu kutufundisha?” Kisha wanamfukuza.—Yohana 9:34.

Yesu anaposikia jambo lililotokea, anampata mtu huyo na kumuuliza: “Je, unamwamini Mwana wa binadamu?” Yule mtu aliyeponywa anajibu: “Bwana, huyo ni nani, niambie ili nimwamini?” Yesu anasema hivi moja kwa moja: “Tayari umemwona, na kwa kweli, yeye ndiye anayezungumza nawe.”—Yohana 9:35-37.

Yule mtu anajibu: “Ninamwamini, Bwana.” Akionyesha imani na heshima, yule mtu anainama mbele ya Yesu, ambaye anasema maneno haya muhimu: “Nilikuja ulimwenguni kwa ajili ya hukumu hii, ili wale wasioona waweze kuona na wale wanaoona wawe vipofu.”—Yohana 9:38, 39.

Mafarisayo walio hapo wanajua kwamba wao si vipofu. Namna gani jukumu walilojitwika la kuwa viongozi wa kiroho? Wanauliza hivi ili kujitetea: “Je, sisi pia ni vipofu?” Yesu anasema: “Kama mngekuwa vipofu, hamngekuwa na dhambi. Lakini sasa mnasema, ‘Tunaona.’ Dhambi yenu inabaki.” (Yohana 9:40, 41) Kama hawangekuwa walimu katika Israeli, huenda ingeeleweka kwamba wanamkataa Yesu kuwa Masihi. Lakini kwa sababu ya ujuzi walio nao kuhusu Sheria, wanatenda dhambi kubwa kwa kumkataa.