Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaweza Kupigana na Shetani—na Kupata Ushindi!

Unaweza Kupigana na Shetani—na Kupata Ushindi!

‘Muchukue musimamo mukamupinge [Shetani], mukiwa imara katika imani.’1 PET. 5:9.

1. (a) Sababu gani leo vita yenye tunapigana na Shetani inaendelea kuwa nguvu? (b) Ni nini inaonyesha kwamba tunaweza kupata ushindi katika vita yenye tunapigana na Shetani?

SHETANI anapigana na mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta na “kondoo wengine.” (Yoh. 10:16) Kwa sababu anabakia na muda mufupi, Ibilisi anajikaza sana ili ameze watumishi wa Yehova wengi zaidi. (Soma Ufunuo 12:9, 12.) Tunaweza kupigana na Shetani na kupata ushindi? Ndiyo! Biblia inasema hivi: ‘Mumupinge Ibilisi, naye atawakimbia ninyi.’—Yak. 4:7.

2, 3. (a) Sababu gani Shetani anapenda watu wasiamini kwamba iko kabisa? (b) Ni nini inakuhakikishia kwamba Shetani iko kabisa?

2 Watu wengi wanazarau wazo la kwamba Shetani iko kabisa. Wanaamini kwamba Shetani na mashetani wake ni watu wa kuwazia tu wenye kuzungumuziwa katika vitabu, wenye kuonyeshwa katika filme zenye kuogopesha, na katika michezo ya video. Watu hao wanafikiri kwamba mutu mwenye kuwa na akili hawezi kuamini kwamba kuko viumbe wa roho wabaya. Unawaza Shetani anahangaika wakati watu wanasema kwamba yeye na mashetani wake ni watu wa kuwazia tu? Hapana! Kwa hiyo, Shetani anaweza kwa urahisi kupofusha akili za watu wenye hawaamini kabisa kwamba yeye iko. (2 Kor. 4:4) Kueneza habari yenye kusema kwamba viumbe hao wa roho hawako kabisa, ni njia moja kati ya njia nyingi zenye Shetani anatumia ili kudanganya watu.

3 Sisi watumishi wa Yehova, hatuamini uongo huo kama watu wengine wenye kudanganywa. Tunajua kwamba Ibilisi iko kabisa. Kwanza, alitumia nyoka ili kuzungumuza na Eva. (Mwa. 3:1-5) Pili, alizungumuza na Yehova kuhusu uaminifu wa Ayubu. (Ayu. 1:9-12) Tatu, alimujaribu Yesu. (Mt. 4:1-10) Ine, kisha Ufalme wa Mungu kuanza kutawala katika mwaka wa 1914, Shetani alianza “kupigana vita” na mabaki ya Wakristo watiwa-mafuta. (Ufu. 12:17) Vita hiyo inaendelea kwa sababu Shetani anajaribu kuvunja imani ya mabaki ya wale 144000 na kondoo wengine. Ili kupigana na Shetani na kupata ushindi, tunapaswa kumupinga na kuendelea kuwa imara katika imani. Habari hii inazungumuzia njia tatu zenye zitatusaidia kufanya hivyo.

UEPUKE MAJIVUNO

4. Namna gani Shetani alionyesha kwamba ni mwenye majivuno sana?

4 Shetani ni mwenye majivuno sana. Malaika huyo mubaya alijipatia ujasiri wa kupinga haki ya Mungu ya kutawala na alichochea watu wamuabudu yeye kuliko kumuabudu Yehova. Kwa hiyo, njia moja yenye tunaweza kutumia ili kumupinga Shetani ni kuwa na unyenyekevu na kuepuka kuwa na majivuno. (Soma 1 Petro 5:5.) Majivuno, maana yake nini? Je, aina yote ya majivuno ni mubaya?

5, 6. (a) Je, aina yote ya majivuno ni mubaya? Eleza. (b) Mungu anachukia aina gani ya majivuno, na Maandiko inatutolea mifano gani?

5 Kamusi moja inaeleza kwamba kujivuna “ni kujiona kuwa wa maana sana na mwenye kuheshimiwa.” Tena ni “kutosheka kwa sababu wewe ao watu wenye unapenda sana wametimiza jambo fulani nzuri ao wamepata kitu fulani kizuri.” Kujisikia hivyo haiko mubaya. Mutume Paulo aliwaambia Wakristo Wathesalonike hivi: ‘Sisi wenyewe tunajivunia ninyi kati ya makutaniko ya Mungu kwa sababu ya uvumilivu wenu na imani katika mateso yenu yote na ziki munazovumilia.’ (2 Tes. 1:4) Kwa hiyo, kufurahia kazi yenye wengine wametimiza na kujivuna kwa kiasi fulani, kunaweza kutusaidia tujisikie muzuri. Hatuwezi kusikilia haya familia yetu, desturi za kwetu, ao nafasi kwenye tumekomalia.—Mdo. 21:39.

6 Lakini, kuna aina fulani ya majivuno yenye inaweza kubadilika na kuwa kiburi. Aina hiyo ya majivuno inaweza kutufanya tupoteze uhusiano wetu na wengine na kuharibu urafiki wetu pamoja na Yehova. Kujivuna kwa namna hiyo kunaweza kutufanya tuchukie wengine na kukataa mashauri mazuri yenye wanatutolea. (Zab. 141:5) Aina hiyo ya majivuno ni “kujitumainia kwa njia isiyofaa” ao kuwa na “kiburi kama watu wenye kujiona kuwa wao ni wa maana sana kuliko wengine.” Yehova anachukia kiburi. (Eze. 33:28; Amo. 6:8) Kwa sababu Shetani ni mwenye kiburi, anafurahi sana wakati anaona wanadamu wanaonyesha kiburi na majivuno. Kwa mufano, alifurahi sana wakati Nimrodi, Farao, na Absalomu walionyesha kiburi. (Mwa. 10:8, 9; Kut. 5:1, 2; 2 Sam. 15:4-6) Mungu alimukataa Kaini kwa sababu ya kiburi. Alimushauria, lakini kwa sababu alikuwa mwenye kiburi sana, alikataa mashauri hayo; na hilo lilimuletea musiba.—Mwa. 4:6-8.

7, 8. (a) Ubaguzi wa rangi ya ngozi ni nini, na sababu gani kufanya hivyo ni njia moja ya kuonyesha majivuno? (b) Eleza namna gani majivuno inaweza kuvuruga amani ya kutaniko.

7 Leo, watu wanaonyesha aina mbaya za majivuno. Wakati fulani, majivuno inaonekana kupitia ubaguzi wa rangi ya ngozi. Kamusi moja inaeleza kwamba kuchukia watu wengine kwa sababu ya rangi ya ngozi yao ni “kuwabagua ao kuwachukia” na pia “ni kuamini kwamba watu wa rangi ingine ya ngozi wako na uwezo na sifa zenye kuachana, na kwamba watu wa rangi fulani ya ngozi ni wa hali ya juu sana ao wa maana zaidi kuliko watu wengine.” Ubaguzi wa rangi ya ngozi umetokeza maandamano, vita, na hata mauaji makubwa.

8 Bila shaka, katika kutaniko Wakristo wanapaswa kuepuka kuwa na mawazo kama hayo. Hata hivyo, mabishano inaweza kutokea kati ya Wakristo wawili kwa sababu ya majivuno, na inaweza kuwa vigumu kumaliza mabishano hayo. Wakristo fulani wa wakati wa mitume walikuwa na mabishano. Ndiyo sababu mutume Yakobo aliwauliza ulizo hili lenye kuwagusa moyo: “Vita vinatoka chanzo gani na mapigano yanatoka chanzo gani katikati yenu?” (Yak. 4:1) Ikiwa tunachukia sana watu wengine na kujiona kuwa wa maana sana, tunaweza kufikia kuwaumiza kupitia maneno na matendo yetu. (Met. 12:18) Bila shaka, majivuno inaweza kuvuruga amani ya kutaniko.

9. Namna gani Biblia inatusaidia kupiganisha ubaguzi wa rangi ya ngozi na aina mubaya ya majivuno? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

9 Ikiwa tunatambua kwamba tumeanza kujiona kuwa watu wa maana sana kuliko wengine, tunapaswa kukumbuka kwamba ‘kila mutu mwenye kiburi moyoni ni chukizo kwa Yehova.’ (Met. 16:5) Ni vizuri pia tujichunguze ili kujua mawazo yetu juu ya watu wa rangi, inchi, na desturi zingine. Ikiwa tunaanza kuchukia watu wa rangi ingine ya ngozi, ao kujivunia inchi yetu, tunasahau kwamba Mungu ‘alifanya kutoka kwa mutu mumoja kila taifa la watu.’ (Mdo. 17:26) Kwa hiyo, tunaweza kusema kwamba kuna aina moja tu ya watu kwa sababu sisi wote tuko na tate (nkambo) mumoja, ni kusema, Adamu. Kwa hiyo, ni kukosa akili kufikiri kwamba watu wa rangi fulani ya ngozi ni wa maana sana kuliko wengine. Ikiwa tunakuwa na mawazo kama hayo, tunapatia Shetani nafasi ya kuvuruga upendo na umoja wetu wa Kikristo. (Yoh. 13:35) Ili kupigana na Shetani na kupata ushindi, tunapaswa kuepuka aina mubaya ya majivuno.—Met. 16:18.

USIPENDE ULIMWENGU WALA VITU VYA KIMWILI

10, 11. (a) Sababu gani inaweza kuwa vyepesi kwa Mukristo kuanza kupenda ulimwengu? (b) Namna gani Dema alifikia kuupenda ulimwengu?

10 Shetani ni ‘mutawala wa ulimwengu huu,’ na ulimwengu muzima unakaa katika nguvu zake. (Yoh. 12:31; 1 Yoh. 5:19) Kwa hiyo, mambo mengi yenye ulimwengu huu unatuchochea kufanya, inapinga kanuni za Biblia. Lakini, mambo yote yenye kupatikana katika ulimwengu haiko ya mubaya. Hata hivyo, tunapaswa kujua kwamba Shetani anaweza kutumia ulimwengu huu ili kuchochea tamaa yetu na kujaribu kutufanya tuangukie katika zambi ao kutufanya tuanze kupenda sana vitu vya kimwili na kukosa kumuabudu Yehova kwa moyo wote.—Soma 1 Yohana 2:15, 16.

11 Ni wazi kwamba Wakristo fulani wa wakati wa mitume walipenda ulimwengu. Kwa mufano, mutume Paulo aliandika hivi: ‘Dema ameniacha kwa sababu aliupenda mufumo wa mambo.’ (2 Tim. 4:10) Biblia haionyeshe kabisa mambo ya ulimwengu yenye ilimufanya Dema amuache mutume Paulo. Pengine Dema alianza kupenda sana vitu vya kimwili kuliko mambo ya kiroho. Ikiwa ni hivyo, Dema alipoteza pendeleo lake nzuri sana la kumutumikia Mungu. Je, mambo yenye ulimwengu ungemutolea Dema ingekuwa ya lazima sana kuliko baraka zenye Yehova angemupatia kwa kutumika pamoja na mutume Paulo?—Met. 10:22.

12. Ni katika njia gani tunaweza kuangukia katika mutego wa “nguvu za udanganyifu wa utajiri”?

12 Sisi pia tunaweza kuanza kupenda ulimwengu na vitu vya kimwili. Kwa kawaida, sisi Wakristo tunatafuta mahitaji yetu ya kimwili na ya familia yetu. (1 Tim. 5:8) Tunajua kwamba Yehova anapenda tufurahie maisha, kwa sababu wakati aliumba Adamu na Eva, aliwatia katika shamba nzuri, ni kusema, paradiso. (Mwa. 2:9) Lakini, Shetani anaweza kutumia vibaya tamaa yetu kupitia “nguvu za udanganyifu wa utajiri.” (Mt. 13:22) Watu wengi wanafikiri kwamba feza na vitu vya kimwili vinaweza kuwaletea furaha ya kweli. Kufikiri hivyo ni kujidanganya kabisa, kwa sababu hilo linaweza kutufanya tupoteze kitu cha lazima sana chenye tuko nacho, ni kusema, urafiki wetu pamoja na Yehova. Yesu aliwashauria wafuasi wake hivi: ‘Hakuna anayeweza kuwatumikia mabwana wawili; kwa maana ama atamuchukia mumoja na kumupenda ule mwengine, ama atashikamana na mumoja na kumuzarau ule mwengine. Hamuezi kutumikia Mungu na Utajiri.’ (Mt. 6:24) Ikiwa tunajiachilia kabisa kuwa watumwa wa Utajiri, tutaacha kumutumikia Yehova, na hilo ndilo kusudi kubwa la Shetani! Tusiache hata kidogo feza ao vitu vya kimwili vitie urafiki wetu pamoja na Yehova katika hatari. Ili tupigane na Shetani, tunapaswa kuepuka kupenda sana vitu vya kimwili.—Soma 1 Timotheo 6:6-10.

TUEPUKE MAMBO YA UASHERATI

13. Watu wa ulimwengu huu wako na mawazo gani juu ya ndoa na ngono?

13 Mambo ya uasherati ni mutego mwengine wenye ulimwengu wa Shetani unatumia. Leo, watu wengi wanaona kwamba kubakia mwaminifu katika ndoa ni mambo ya zamani. Pia, wanaona ndoa yenyewe kuwa mambo ya zamani na kwamba inawazuia kutumia uhuru wao. Kwa mufano, mwanamuke moja muchezaji mwenye kujulikana sana, alisema hivi: “Haiwezekane kuwa na bibi ao bwana moja tu. Sijaona bibi ao bwana mwenye iko mwaminifu ao mwenye anapenda akuwe mwaminifu.” Mwanaume mumoja muchezaji alisema pia hivi: “Siko hakika kabisa kwamba tuliumbwa ili tuishi na bibi ao bwana moja tu katika maisha yetu yote.” Bila shaka, Shetani anafurahi sana wakati watu hao wenye kujulikana sana wanachafua mupango wa ndoa ambao ni zawadi kutoka kwa Mungu. Ibilisi haunge mukono mupango wa ndoa na hapendi bibi na bwana wakuwe na furaha. Kwa hiyo, ili tupigane na Shetani na kupata ushindi, tunapaswa kuunga mukono mupango wa Mungu wa ndoa.

14, 15. Namna gani tunaweza kukimbia mambo ya uasherati?

14 Iwe tumeoa, tumeolewa, ao hapana, tunapaswa kujikaza sana ili kuepuka namna zote za uasherati. Je, ni vyepesi kufanya hivyo? Hapana! Kwa mufano, ikiwa wewe ni kijana, unaweza kusikia wanafunzi wenzako wanajitapa kwamba walifanya uasherati na mutu fulani ao walitumiana ujumbe ao picha za ngono kupitia telefone ao Internete. Katika maeneo fulani, kutumia mutu ujumbe ao picha za ngono ni jambo mbaya sana sawasawa na kutumia mutu picha za pornografia zenye kuhusisha watoto. Biblia inasema hivi: ‘Yeye aliye na mazoea ya kufanya uasherati anautendea zambi mwili wake mwenyewe.’ (1 Kor. 6:18) Magonjwa yenye kuambukizwa kupitia ngono imeenea sana, na imeleta mateso mengi na kuua watu wengi. Pia, vijana wengi wenye hawajaoa ao kuolewa wenye wamepoteza ubikira wao wanasema kwamba wanahuzunika sana kwa sababu ya matendo yao. Vyombo vya habari, kama vile radio ao televizyo, vinaweza kutuchochea tufikiri kwamba tunaweza kuvunja sheria za Mungu zenye kutuonya juu ya mambo ya uasherati bila kupata matokeo mabaya; lakini kufikiri hivyo ni kujidanganya. Mawazo kama hayo, inawafanya watu waangukie katika ‘nguvu za udanganyifu za zambi.’—Ebr. 3:13.

15 Unaweza kufanya nini ikiwa unapambana na jaribu la kufanya uasherati? Utambue uzaifu wako. (Rom. 7:22, 23) Usali kwa Mungu ili akupatie nguvu. (Flp. 4:6, 7, 13) Uepuke mambo yote yenye inaweza kukuchochea kufanya uasherati. (Met. 22:3) Na wakati unajaribiwa kufanya uasherati, ukimbie.—Mwa. 39:12.

16. Yesu alitenda namna gani wakati Shetani alimujaribu, na mufano wake unaweza kutufundisha nini?

16 Yesu alituachia mufano muzuri sana kuhusu namna ya kupambana na majaribu. Hakudanganywa na ahadi za Shetani, ao kuchukua wakati wa kufikiria ahadi hizo. Lakini aliamua bila kukawia kwa kusema hivi: “Imeandikwa.” (Soma Mathayo 4:4-10.) Yesu alikuwa anajua vizuri Neno la Mungu; ndiyo sababu aliamua bila kukawia na kutaja maandiko wakati Shetani alimujaribu. Ili kupigana na Shetani na kupata ushindi, tunapaswa kuepuka mambo yenye inaweza kutuchochea kufanya uasherati.—1 Kor. 6:9, 10.

UKIVUMILIA UTAPATA USHINDI

17, 18. (a) Shetani iko na silaha gani zingine, na sababu gani hatupaswe kushangaa? (b) Ni jambo gani litamupata Shetani, na namna gani kujua hivyo kunakusaidia kuvumilia?

17 Majivuno, kupenda vitu vya kimwili, na mambo ya uasherati, ni silaha tatu kati ya silaha zenye Shetani anatumia ili kutupiganisha. Shetani iko na silaha zingine nyingi. Kwa mufano, Wakristo fulani wanapingwa na watu wa familia yao, ao wanazarauliwa na wanafunzi wenzao, ao wakubwa wa serikali wamekataza kazi yao ya kuhubiri. Majaribu hayo haitushangaze kwa sababu Yesu alionya wafuasi wake hivi: ‘Mutachukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini ule atavumilia mupaka mwisho ndiye ataokolewa.’—Mt. 10:22.

Shetani anahabiriwa milele(Ona fungu la 18)

18 Namna gani tunaweza kupigana na Shetani na kupata ushindi? Yesu aliwaambia wanafunzi wake hivi: ‘Nanyi kwa kuvumilia mutajipatia nafsi zenu.’ (Lu. 21:19) Hakuna jambo lenye mwanadamu anaweza kufanya ili kutuangamiza milele. Hakuna mutu anaweza kutuzuia kuendelea kuwa na urafiki wa sana pamoja na Mungu, isipokuwa tu sisi wenyewe. (Rom. 8:38, 39) Hata kama watumishi fulani wa Yehova wanakufa, hilo halimaanishe kwamba Shetani amepata ushindi, kwa sababu Yehova atawafufua! (Yoh. 5:28, 29) Lakini, Shetani hana tumaini lolote. Kisha ulimwengu huu muovu kuhabiriwa, atatupwa katika abiso kwa miaka 1000. (Ufu. 20:1-3) Mwishoni mwa Miaka Elfu ya Utawala wa Yesu, Shetani “atafunguliwa kutoka katika gereza lake” kwa muda mufupi ili ajaribu kudanganya wanadamu wakamilifu kwa mara ya mwisho. Kisha hapo, Ibilisi ataharibiwa. (Ufu. 20:7-10) Shetani hana tumaini lolote kwa ajili ya wakati unaokuja, lakini wewe uko na tumaini! Uendelee kuwa na imani yenye nguvu ili kupigana na Shetani. Unaweza kupigana na Shetani na kupata ushindi!