Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA

Vita Iliyobadilisha Ulimwengu

Vita Iliyobadilisha Ulimwengu

Miaka mia moja iliyopita, mamilioni ya vijana wanaume waliacha hali ya usalama ya nyumbani kwao na wakaenda kupigana vita. Walienda wakiwa na furaha, wakichochewa na roho ya kupenda inchi zao, roho ambayo ilienea sana. Katika mwaka wa 1914, askari mumoja wa Amerika aliandika hivi: “Mimi ni mwenye furaha sana na ninangojea kwa hamu siku zilizo mbele.”

Lakini, bila kukawia furaha yao iligeuka kuwa uchungu. Hakuna mutu aliyewazia kwamba majeshi hayo makubwa yangepambana kwa miaka mingi katika inchi ya Ubelgiji na ya Ufaransa. Wakati huo, watu waliita vita hiyo “Vita Kubwa.” Leo, watu wanaiita Vita ya Kwanza ya Ulimwengu.

Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilikuwa kubwa kabisa kwa sababu ya hesabu ya watu walioumia na watu waliokufa. Kulingana na uchunguzi fulani, vita hiyo iliua watu karibu milioni 10 na milioni 20 waliumia. Pia vita hiyo ilikuwa matokeo ya makosa makubwa. Viongozi wa siasa wa Ulaya hawakuweza kuzuia ugomvi kati ya mataifa mengi usifikie kuwa vita ya ulimwenguni pote. Jambo la maana zaidi ni kwamba, labda “Vita Kubwa” hiyo iliacha ulimwengu katika hali ya uharibifu wenye kudumu. Ilibadilisha ulimwengu katika njia ambazo zinatuumiza mupaka leo.

MAKOSA YALIYOFANYA WATU WASIAMINIANE

Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilitokea kwa sababu ya kukadiria mambo kwa njia yenye makosa. Kitabu kimoja kinasema kwamba viongozi wa Ulaya hawakujua kuwa maamuzi ambayo walikuwa wanafanya yangetokeza musiba mukubwa. (The Fall of the Dynasties​—The Collapse of the Old Order 1905-1922)

Kisha majuma machache, kuuawa kwa Mwana-mufalme wa Austria kuliingiza inchi zote zenye nguvu za Ulaya katika vita ambayo hawakutaka. Kiongozi wa Ujerumani aliulizwa hivi siku chache kisha vita kuanza, “Mambo yote hayo yalitokea namna gani?” Alijibu kwa huzuni hivi: “Ah, ikiwa tu mutu fulani angejua!”

Viongozi waliofanya maamuzi mabaya yaliyotokeza vita hawakuwa wanafikiria matokeo mabaya ya maamuzi yao. Lakini maaskari waliokuwa katika mashimo ya mapigano walitambua haraka mambo yaliyokuwa yanatendeka. Walitambua kwamba viongozi wao wa siasa waliwavunja moyo, viongozi wao wa dini waliwadanganya, na majenerali wao wa jeshi waliwasaliti. Walifanya hivyo namna gani?

Viongozi wao wa siasa waliwavunja moyo, viongozi wao wa dini waliwadanganya, na majenerali wao wa jeshi waliwasaliti

Viongozi wa siasa waliahidi kwamba vita ingesaidia kuleta ulimwengu mupya na ulio muzuri zaidi. Kiongozi wa Ujerumani alitangaza hivi: “Tunapigana ili tufanye kazi yetu kwa amani, ili tulinde desturi zetu tulizopata kutoka kwa vizazi vyetu vya zamani na kwa ajili ya wakati unaokuja wa inchi yetu.” Raisi wa Amerika Woodrow Wilson alisaidia kuunda usemi uliopendwa na watu wengi na uliowahakikishia kwamba vita ingefanya “ulimwengu uwe na demokrasia.” Na katika inchi ya Uingereza, watu waliwaza kwamba vita hiyo ingekuwa “vita ya kumaliza vita.” Wote walidanganyika.

Viongozi wa dini waliunga vita hiyo mukono kwa bidii. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Viongozi wa dini ambao walipaswa kufundisha watu Biblia waliwachochea waende kwenye vita. Vita ya mataifa yote ilifikia kumaanisha chuki kati ya mataifa yote.” (The Columbia History of the World) Na viongozi wa dini walichochea chuki kuliko kusaidia ipunguke. Kitabu kingine kinasema hivi: “Viongozi wa dini hawakuwa na uwezo, na kwa sehemu kubwa hawakutaka, kutia imani ya Kikristo mbele ya taifa. Wengi kati yao walichagua njia nyepesi na wakafanya Ukristo kuwa sawa na upendo wa taifa. Maaskari Wakristo wa dini zote walitiwa moyo wauane katika jina la Mwokozi wao.” (A History of Christianity)

Majenerali wa vita waliahidi kwamba watashinda haraka na kwa vyepesi sana, lakini mambo hayakuwa kama walivyowazia. Kisha mapigano marefu, majeshi yaliyopigana yalijikuta katika vita kali isiyoisha. Kisha hapo, mamilioni ya maaskari walipambana na jambo ambalo mwanahistoria mumoja aliita kuwa “labda ndilo pigano lenye mauaji makubwa ambayo mwili na roho ya mwanadamu vilikuwa havijapata kuvumilia.” Hata ikiwa watu walikufa wengi, majenerali waliendelea kutuma watu wao waende kwenye uwanja wa mapambano ambako masasi yalikuwa yanamwagika kama maji. Haishangaze kwamba mauaji yalienea sana.

Vita ya Kwanza ya Ulimwengu ilikuwa na matokeo gani juu ya watu? Kitabu kimoja cha historia kinataja maneno ya askari aliyeshiriki katika vita kwa muda murefu aliyesema hivi: “Vita . . . iliharibisha akili na tabia ya watu wa wakati huo.” Kwa kweli, matokeo ya vita hiyo ni kwamba falme nzima-nzima zilipotea. Vita hiyo mbaya sana ilikuja kuwa mwanzo wa kipindi cha miaka 100 yenye umwangaji mukubwa wa damu ambao wanadamu walikuwa hawajapata kuona. Karibu kila mahali, watu waliandamana na kuacha kufanya kazi.

Sababu gani vita hiyo ilibadilisha kabisa ulimwengu? Vita hiyo lilikuwa tukio kubwa lililojitokeza lenyewe tu? Majibu ya maulizo hayo yanafunua jambo fulani juu ya wakati wetu unaokuja?