Waamuzi 20:1-48

  • Wabenjamini washambuliwa (1-48)

20  Ndipo Waisraeli wote kutoka Dani+ hadi Beer-sheba na kutoka nchi ya Gileadi+ wakakusanyika kwa umoja* mbele za Yehova kule Mispa.+  Basi wakuu wa watu na wa makabila yote ya Israeli wakachukua nafasi zao katika kutaniko la watu wa Mungu—wanajeshi 400,000 wenye mapanga waliotembea kwa miguu.+  Wabenjamini wakasikia kwamba wanaume Waisraeli walikuwa wameenda Mispa. Ndipo wanaume Waisraeli wakauliza, “Tuambieni, jambo hili linalochukiza lilitendekaje?”+  Kwa hiyo yule Mlawi,+ mume wa mwanamke aliyeuawa, akajibu: “Mimi na suria wangu tulifika Gibea+ katika nchi ya Wabenjamini ili tulale usiku.  Kisha wakaaji* wa Gibea wakaja kunishambulia na kuizingira nyumba usiku. Walitaka kuniua, lakini wakambaka suria wangu, naye akafa.+  Basi nikachukua maiti ya suria wangu na kuikatakata vipandevipande, kisha nikavipeleka vipande hivyo katika maeneo* yote ya urithi ya Waisraeli,+ kwa sababu walitenda jambo la aibu na lenye kufedhehesha katika Israeli.  Sasa enyi Waisraeli wote, toeni ushauri na mapendekezo yenu+ kuhusu jambo hili.”  Basi watu wote wakasimama pamoja* na kusema, “Hakuna yeyote kati yetu atakayerudi katika hema lake au nyumbani kwake.  Hivi ndivyo tutakavyowatendea watu wa Gibea: Tuchague watu kwa kura ili waende kupigana nao.+ 10  Tutachukua wanaume 10 kati ya 100 kutoka katika makabila yote ya Israeli, na 100 kati ya 1,000 na 1,000 kati ya 10,000 wawatafutie chakula wanajeshi, ili wawaadhibu wakaaji wa Gibea katika nchi ya Benjamini, kwa sababu ya jambo hili la aibu walilotenda katika Israeli.” 11  Kwa hiyo wanaume wote Waisraeli wakakusanyika na kuungana pamoja* ili kulishambulia jiji hilo. 12  Kisha makabila ya Israeli yakatuma wanaume kwa watu wa kabila la Benjamini, wakawauliza, “Kwa nini mmetenda jambo hili linalochukiza? 13  Sasa waleteni wahuni hao wa Gibea,+ ili tuwaue na kuondoa kabisa uovu katika Israeli.”+ Lakini Wabenjamini walikataa kuwasikiliza ndugu zao Waisraeli. 14  Ndipo Wabenjamini wakakusanyika kutoka katika majiji yao kwenda Gibea ili kupigana na wanaume Waisraeli. 15  Siku hiyo Wabenjamini walikusanya wanaume 26,000 wenye mapanga kutoka katika majiji yao, na pia wanaume 700 mashujaa kutoka Gibea. 16  Jeshi hilo lilikuwa na wanaume 700 mashujaa waliotumia mkono wa kushoto. Kila mmoja wao aliweza kurusha jiwe kwa kombeo na kulenga unywele* bila kukosea. 17  Waisraeli kwa upande wao walikusanya wanaume 400,000 wenye mapanga,+ na kila mmoja wao alikuwa mpiganaji mwenye uzoefu. 18  Wakapanda kwenda Betheli kumwomba Mungu ushauri.+ Basi Waisraeli wakamuuliza hivi: “Ni nani kati yetu anayepaswa kutuongoza kupigana na Wabenjamini?” Yehova akajibu, “Kabila la Yuda litaongoza.” 19  Baada ya hayo, Waisraeli wakaamka asubuhi na kupiga kambi ili kushambulia Gibea. 20  Basi wanaume Waisraeli wakaenda kupigana na Wabenjamini; wakajipanga kivita ili kushambulia Gibea. 21  Kisha Wabenjamini wakatoka Gibea na kuwaua wanaume 22,000 Waisraeli siku hiyo. 22  Hata hivyo, wanajeshi Waisraeli wakaonyesha ujasiri na kujipanga tena kwa ajili ya vita mahali walipojipanga siku ya kwanza. 23  Ndipo Waisraeli wakapanda kwenda kumlilia Yehova mpaka jioni na kumuuliza hivi Yehova: “Je, twende tena kupigana na ndugu zetu, Wabenjamini?”+ Yehova akawaambia, “Pandeni mkapigane nao.” 24  Basi Waisraeli wakawakaribia Wabenjamini siku ya pili. 25  Nao Wabenjamini wakatoka Gibea ili kupigana nao siku ya pili, wakawaua Waisraeli wengine 18,000,+ wote wakiwa na mapanga. 26  Ndipo wanaume wote wa Israeli wakapanda kwenda Betheli. Wakalia na kukaa huko mbele za Yehova,+ nao wakafunga+ siku hiyo mpaka jioni na kumtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa+ na dhabihu za ushirika.+ 27  Baada ya hayo, wanaume Waisraeli wakaomba ushauri wa Yehova,+ kwa kuwa sanduku la agano la Mungu wa kweli lilikuwa huko siku hizo. 28  Basi Finehasi+ mwana wa Eleazari, mwana wa Haruni, alikuwa akihudumu* mbele ya sanduku hilo siku hizo. Wakamuuliza, “Je, twende tena kupigana na ndugu zetu Wabenjamini, au tusiende?”+ Yehova akawajibu hivi: “Nendeni, kwa sababu kesho nitawatia mikononi mwenu.” 29  Ndipo Waisraeli wakaweka wanaume kuzunguka Gibea ili walivizie.+ 30  Waisraeli wakapanda kwenda kupigana na Wabenjamini siku ya tatu, wakajipanga kivita ili kushambulia Gibea kama walivyofanya awali.+ 31  Wabenjamini walipoenda kupigana na jeshi hilo, walivutwa mbali na jiji.+ Kisha, kama awali, wakaanza kuwashambulia na kuwaua watu kwenye barabara kuu; barabara moja inaenda Betheli na nyingine Gibea, wakawaua wanaume Waisraeli wapatao 30 mashambani.+ 32  Wabenjamini wakasema, “Tunawashinda kama awali.”+ Lakini Waisraeli wakasema, “Tukimbieni na kuwavuta mbali na jiji lao waje kwenye barabara kuu.” 33  Basi wanaume wote wa Israeli wakatoka walipokuwa na kwenda kujipanga kivita kule Baal-tamari, na Waisraeli waliokuwa wakivizia wakatoka mahali walipokuwa wamejificha karibu na Gibea. 34  Kisha wanaume 10,000 mashujaa kutoka kotekote Israeli wakaja mbele ya Gibea, na mapigano yakawa makali. Lakini Wabenjamini hawakujua kwamba walikuwa karibu kuangamizwa. 35  Yehova akawashinda Wabenjamini+ mbele ya Waisraeli; siku hiyo Waisraeli waliwaua wanaume 25,100 Wabenjamini waliokuwa na mapanga.+ 36  Hata hivyo, wanaume Waisraeli walipokimbia kutoka Benjamini,+ Wabenjamini walifikiri kwamba wangewashinda, lakini walikimbia kwa sababu waliwategemea Waisraeli wenzao waliokuwa wakivizia jiji la Gibea.+ 37  Na wale waliokuwa wakivizia wakatoka haraka na kukimbia kuelekea Gibea. Wakasambaa na kuwaua kwa upanga watu wote waliokuwa jijini. 38  Basi wanaume wa Israeli walikuwa wamepanga kwamba wanaume waliovizia jiji watoe ishara kwa kufanya moshi upande juu kutoka jijini. 39  Waisraeli walipogeuka na kukimbia, wanaume Wabenjamini wakaanza kuwashambulia, wakawaua wanaume Waisraeli wapatao 30,+ huku wakisema, “Ni wazi kwamba tunawashinda tena, kama tulivyowashinda awali.”+ 40  Lakini ile ishara ya wingu la moshi ikaanza kupanda kutoka jijini. Wabenjamini walipogeuka, waliona moto ukiteketeza jiji lote na moshi ukipanda angani. 41  Kisha wanaume Waisraeli wakageuka kwa ghafla na kuwakimbiza, Wabenjamini wakashtuka, kwa kuwa waliona kwamba wataangamizwa. 42  Basi wakawakimbia wanaume Waisraeli na kuelekea nyikani, lakini Waisraeli wakawakimbiza na kuwashambulia; wanaume Waisraeli waliotoka majijini wakawashambulia pia na kuwaua. 43  Wakawazingira Wabenjamini na kuwafuata himahima. Wakawakanyaga-kanyaga mbele ya Gibea, upande wa mashariki. 44  Hatimaye wanaume 18,000 Wabenjamini wakaangamizwa, wote walikuwa mashujaa hodari.+ 45  Basi wanaume Wabenjamini wakageuka na kukimbilia nyikani kwenye mwamba wa Rimoni,+ na Waisraeli wakawaua Wabenjamini 5,000 kwenye barabara kuu, nao wakaendelea kuwafuatia mpaka Gidomu; wakawaua wanaume wengine 2,000. 46  Siku hiyo, Wabenjamini 25,000 wenye mapanga waliuawa,+ wote walikuwa mashujaa hodari. 47  Lakini wanaume 600 walikimbilia nyikani kwenye mwamba wa Rimoni, na kukaa kwenye mwamba huo kwa miezi minne. 48  Na wanaume Waisraeli wakarudi kuwashambulia Wabenjamini na kuwaua kwa upanga watu wote waliokuwa jijini pamoja na mifugo, kila kitu kilichobaki. Pia, waliteketeza kwa moto majiji yote katika maeneo waliyopitia.

Maelezo ya Chini

Tnn., “kama mtu mmoja.”
Au labda, “wamiliki wa mashamba.”
Au “makabila.”
Tnn., “kama mtu mmoja.”
Tnn., “kama mtu mmoja.”
Au “shabaha.”
Tnn., “akisimama.”