Waamuzi 21:1-25

  • Kabila la Wabenjamini laokolewa (1-25)

21  Sasa wanaume Waisraeli walikuwa wameapa hivi kule Mispa:+ “Hakuna yeyote kati yetu atakayekubali binti yake aolewe na mwanamume Mbenjamini.”+  Kwa hiyo, watu wakaja Betheli+ na kukaa huko mbele za Mungu wa kweli mpaka jioni, wakipaza sauti na kulia kwa uchungu.  Nao walikuwa wakisema hivi: “Ee Yehova Mungu wa Israeli, kwa nini jambo hili limetokea katika Israeli? Kwa nini tukose kabila moja la Israeli leo?”  Siku iliyofuata, watu wakaamka mapema na kujenga madhabahu hapo ili watoe dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika.+  Kisha Waisraeli wakaulizana, “Ni kabila gani kati ya makabila yote ya Israeli ambalo halikukusanyika mbele za Yehova?” kwa kuwa walifanya kiapo kikubwa kwamba yeyote ambaye hakufika Mispa mbele za Yehova lazima auawe.  Basi Waisraeli wakahuzunika kwa sababu ya mambo yaliyowapata ndugu zao Wabenjamini. Wakasema, “Leo kabila moja limekatwa kutoka Israeli.  Kwa kuwa tumeapa mbele za Yehova+ kwamba hatutakubali kamwe binti zetu waolewe nao, tutapata wapi wake kwa ajili ya wanaume waliobaki?”+  Wakaulizana, “Ni kabila gani la Israeli ambalo halikufika Mispa mbele za Yehova?”+ Wakagundua kwamba hakuna yeyote kutoka Yabesh-gileadi aliyekuja kambini kukusanyika na Waisraeli wengine.  Watu walipohesabiwa, wakagundua kwamba hakuna mkaaji hata mmoja wa Yabesh-gileadi aliyekuwepo. 10  Basi wakawatuma wanaume 12,000 waliokuwa mashujaa zaidi. Wakawaamuru hivi: “Nendeni, mkawaue kwa upanga wakaaji wa Yabesh-gileadi, msiache wanawake wala watoto.+ 11  Hivi ndivyo mnavyopaswa kufanya: mnapaswa kumwangamiza kila mwanamume, na pia kila mwanamke ambaye amefanya ngono na mwanamume.” 12  Miongoni mwa wakaaji wa Yabesh-gileadi walipata mabikira 400 ambao hawajawahi kufanya ngono na mwanamume. Basi wakawaleta kambini huko Shilo,+ katika nchi ya Kanaani. 13  Kisha Waisraeli waliokusanyika wakawatumia ujumbe wa amani Wabenjamini waliokuwa kwenye mwamba wa Rimoni.+ 14  Basi Wabenjamini wakarudi wakati huo. Waisraeli wakawapa Wabenjamini wanawake waliowachukua kule Yabesh-gileadi,+ lakini walikuwa wachache kuliko wanaume. 15  Na watu wakahuzunika kwa sababu ya mambo yaliyowapata Wabenjamini+ kwa kuwa Yehova alileta mgawanyiko katika makabila ya Israeli. 16  Wazee wa Waisraeli wakauliza, “Kwa kuwa wanawake wote Wabenjamini waliuawa, tufanye nini ili tupate wake kwa ajili ya wanaume waliobaki?” 17  Wakajibu, “Wabenjamini waliobaki wanapaswa kupewa urithi ili kabila lolote lisiangamizwe kutoka Israeli. 18  Lakini haturuhusiwi kuwapa binti zetu wawe wake zao, kwa sababu Waisraeli wameapa hivi: ‘Alaaniwe yeyote anayempa Mbenjamini mke.’”+ 19  Ndipo wakasema, “Jamani! Kuna sherehe ya Yehova inayofanywa kila mwaka kule Shilo,+ jiji lililo upande wa kaskazini wa Betheli na upande wa mashariki wa barabara kuu inayopanda kutoka Betheli kwenda Shekemu na upande wa kusini wa Lebona.” 20  Kisha wakawaamuru hivi wanaume Wabenjamini: “Nendeni mkavizie katika mashamba ya mizabibu. 21  Mtakapoona wasichana wa* Shilo wakitoka ili kucheza dansi za mzunguko, tokeni katika mashamba ya mizabibu na kila mmoja wenu ajichukulie mke miongoni mwa wasichana hao wa Shilo, kisha mrudi katika nchi ya Benjamini. 22  Na baba zao au ndugu zao wakija kutulalamikia, tutawaambia, ‘Tutendeeni kwa fadhili kwa niaba yao, kwa sababu tulipoenda vitani hatukuweza kupata mke kwa ajili ya kila mmoja wao,+ nanyi hamngeweza kuwapa wake na kuepuka hatia.’”+ 23  Basi hivyo ndivyo wanaume Wabenjamini walivyofanya; walijichukulia wake miongoni mwa wanawake waliokuwa wakicheza dansi. Kisha wakarudi katika urithi wao, wakajenga tena majiji yao,+ na kuishi humo. 24  Wakati huo Waisraeli wakatawanyika kutoka huko, na kila mmoja akarudi kwa kabila lake na kwa ukoo wake, kila mmoja akarudi katika urithi wake. 25  Siku hizo hakukuwa na mfalme katika Israeli.+ Kila mtu alifanya jambo aliloona ni jema machoni pake.*

Maelezo ya Chini

Tnn., “mabinti wa.”
Au “alilofikiri linafaa.”