Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jina zuri, hufanya watu wakutumaini na kukuheshimu

‘Jina Zuri Ni Bora Kuliko Utajiri Mwingi’

‘Jina Zuri Ni Bora Kuliko Utajiri Mwingi’

JINA zuri, au heshima, lina thamani sana hivi kwamba katika baadhi ya nchi linalindwa kisheria. Hilo linaweza kutia ndani kulinda jina lisichafuliwe kupitia maandishi au kwa maneno. Jambo hilo linatukumbusha usemi huu wa kale: “Ni afadhali kuchagua jina badala ya utajiri mwingi; kibali ni bora kuliko hata fedha na dhahabu.” (Methali 22:1) Tunaweza kufanya nini ili tuwe na jina zuri na kuheshimiwa na wengine? Mapendekezo bora zaidi yanapatikana kwenye Biblia.

Kwa mfano, fikiria yale ambayo Biblia inasema katika Zaburi ya 15. Ili kujibu swali, “Ni nani atakayekuwa mgeni katika hema la [Mungu]?” mtunga zaburi aliandika hivi: “Yeye . . . [anayezoea] kutenda uadilifu na kusema kweli katika moyo wake. Yeye hakuchongea . . . , hakumfanyia mwenzake jambo lolote baya, wala hakumshutumu rafiki yake. Machoni pake mtu yeyote mwenye kudharaulika hakika amekataliwa . . . Ameapa juu ya jambo lililo baya kwake, na bado yeye habadiliki. . . . Wala hakuchukua rushwa.” (Zaburi 15:1-5) Bila shaka utamheshimu mtu anayeishi kupatana na kanuni hizo, sivyo?

Sifa nyingine inayoweza kufanya mtu aheshimiwe ni unyenyekevu. Andiko la Methali 15:33 linasema hivi: “Kabla ya utukufu hutangulia unyenyekevu.” Fikiria jambo hili: Mtu mnyenyekevu huona sehemu anazohitaji kufanyia maendeleo naye hujitahidi kuziboresha. Pia, yuko tayari kuomba msamaha kwa hiari anapomkosea mwingine. (Yakobo 3:2) Tofauti na hilo, mtu mwenye kiburi hukasirika upesi na kujitetea. Methali 16:18 inasema hivi: “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.”

Hata hivyo, namna gani ikiwa mtu fulani amechafua jina lako? Je, utachukua hatua haraka, labda ukiwa na ghadhabu nyingi? Jiulize hivi, ‘Ikiwa nitajitahidi kutetea jina langu, je, sitakuwa nikieneza zaidi uwongo huo?’ Ingawa nyakati fulani inaweza kufaa kuchukua hatua za kisheria, Biblia inatoa ushauri huu wenye hekima: “Usiende kwa haraka kufanya kesi.” Badala yake, “jitetee kwa mwenzako.” (Methali 25:8, 9) * Kushughulikia mambo kwa njia hii kunaweza pia kuokoa pesa nyingi ambazo ungetumia kuendeshea mashtaka.

Biblia si kitabu cha kidini tu. Ni mwongozo unaotegemeka wa maisha. Wote wanaofuata hekima yake wanasitawisha sifa zinazofanya waheshimiwe sana na kupata jina zuri.

^ fu. 5 Kanuni nyingine za Biblia ambazo zinaweza kukusaidia kusuluhisha kutoelewana zinapatikana katika Mathayo 5:23, 24; 18:15-17.