Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | NDOA

Jinsi ya Kukomesha Tabia ya Kunyamaziana

Jinsi ya Kukomesha Tabia ya Kunyamaziana

KIKWAZO

Watu wawili walioapa kupendana wanawezaje kuacha kuzungumziana kwa saa—au hata kwa siku nyingi? Wanajiambia wenyewe, ‘Angalau tumeacha kugombana.’ Lakini bado tatizo halijatatuliwa, na wote wawili hawana furaha.

KWA NINI HILI HUTUKIA

Kulipiza kisasi. Wenzi fulani wa ndoa hunyamaza ili walipize kisasi. Kwa mfano, tuseme mume anafanya mipango ya mwisho juma bila kuwasiliana na mkewe. Mke anapogundua jambo hilo, anakasirika na kusema kwamba mumewe hamjali. Mume anamwambia mkewe kwamba anapenda kukasirika bila sababu. Mke anaondoka kwa hasira na anaacha kuongea na mume wake. Ni kana kwamba mke anasema, “Umeniumiza, kwa hiyo mimi nitakuumiza pia.”

Kutenda kwa hila. Wengine hutumia tabia ya kunyamaza kama njia ya kupata kile wanachotaka. Kwa mfano, wazia kwamba mume na mke wanapanga kusafiri, na mke angependa kusafiri pamoja na wazazi wake. Mume anakataa. “Nilikuoa wewe, sikuwaoa wazazi wako,” mume anasema. Kisha anaacha kuzungumza na mke wake, anamwepuka kabisa mpaka mke akate tamaa na kukubali anachotaka.

Bila shaka, nyakati nyingine wenzi wa ndoa wanapogombana, huenda itafaa kwao kunyamaza kwa muda hadi hasira yao ipoe. Kunyamaziana kwa njia hiyo kunaweza kuwa na manufaa. Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya.” (Mhubiri 3:7) Hata hivyo, tabia ya kunyamaziana inapotumiwa kama njia ya kulipiza kisasi au kupata kile mtu anachotaka, inarefusha ugomvi na pia inawafanya wenzi wa ndoa waache kuheshimiana. Mnaweza kuzuiaje hali hiyo isiwapate?

 MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Hatua ya kwanza ya kukomesha tabia ya kunyamaziana ni kutambua kwamba njia hiyo haitatui matatizo yenu. Ni kweli, huenda kutoongea kukakuwezesha kulipiza kisasi au kukamshurutisha mwenzi wako akubali mapendezi yako. Lakini je, hivyo ndivyo unavyotaka kumtendea mtu ambaye umeapa kumpenda? Kuna njia bora za kusuluhisha kutoelewana.

Uwe na utambuzi. Biblia inasema kwamba upendo “hauchokozeki.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Kwa hiyo uwe mtulivu mwenzi wako anaposema maneno kama haya akiwa amekasirika, “Wewe hunisikilizi kamwe” au “Wewe huchelewa kila wakati.” Badala yake, tambua anajaribu kukuambia nini. Kwa mfano, anaposema, “Wewe hunisikilizi kamwe” huenda akawa anamaanisha “Nahisi ni kana kwamba huchukui maoni yangu kwa uzito.”—Kanuni ya Biblia: Methali 14:29.

Kumbuka kwamba mwenzi wako yuko upande wako naye si mpinzani wako

Zungumza kwa sauti ya chini. Hali huzidi kuwa mbaya kadiri mabishano yanavyozidi kuendelea. Kwa upande mwingine, unaweza kuzuia mabishano yasiwe mabaya zaidi. Jinsi gani? Kitabu Fighting for Your Marriage (Jinsi ya Kuiokoa Ndoa Yako) kinasema hivi: “Kuongea kwa upole na kutambua maoni ya mwenzi wako ni mbinu unazoweza kutumia kuzuia hali ya kutoelewana isiendelee na kuwa mbaya. Mara nyingi hilo tu ndilo linalohitajika.”—Kanuni ya Biblia: Methali 26:20.

Usijifikirie tu. Biblia inasema hivi: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali ile ya yule mtu mwingine.” (1 Wakorintho 10:24) Ukikumbuka kwamba mwenzi wako yuko upande wako naye si mpinzani wako, hutaudhika kwa urahisi, hutabishana naye bila sababu, wala hutamnyamazia.—Kanuni ya Biblia: Mhubiri 7:9.

Tabia ya kunyamaziana haipatani na himizo hili la Biblia: “Kila mtu mmoja-mmoja kati yenu na ampende hivyo mke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe; kwa upande mwingine, mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33) Kwa nini wewe na mwenzi wako msikubaliane kuwa tabia ya kunyamaziana hairuhusiwi katika ndoa yenu?