Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 44

Imarisha Urafiki Wako Pamoja na Wengine Kabla ya Mwisho Kufika

Imarisha Urafiki Wako Pamoja na Wengine Kabla ya Mwisho Kufika

“Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote.”—MET. 17:17.

WIMBO 101 Kufanya Kazi Pamoja kwa Umoja

MUHTASARI *

Tutahitaji kuwa na marafiki wazuri wakati wa “dhiki kuu” (Tazama fungu la 2) *

1-2. Kulingana na 1 Petro 4:7, 8, ni nini kitakachotusaidia kukabiliana na hali ngumu?

KADIRI tunavyokaribia mwishoni mwa “siku za mwisho,” huenda tukakabili majaribu makubwa sana. (2 Tim. 3:1) Kwa mfano, baada ya kampeni ya uchaguzi katika nchi moja ya Afrika Magharibi, mapigano na machafuko yalizuka. Kwa zaidi ya miezi sita, ndugu na dada zetu hawakuwa na uhuru wa kutembea kwa sababu walikuwa katikati ya eneo lenye machafuko. Ni nini kilichowasaidia kukabiliana na hali hiyo ngumu? Baadhi yao walikimbilia kwenye nyumba za akina ndugu walioishi katika eneo salama zaidi. Ndugu mmoja alisema hivi: “Nilipokuwa katika hali hiyo, nilithamini sana kuwa pamoja na marafiki. Tuliweza kutiana moyo.”

2 “Dhiki kuu” itakapoanza, tutathamini kuwa na marafiki wazuri wanaotupenda. (Ufu. 7:14) Hivyo, ni muhimu sana kwamba tusitawishe urafiki wenye nguvu pamoja na wengine sasa. (Soma 1 Petro 4:7, 8.) Tunaweza kujifunza mengi kutokana na mambo yaliyompata Yeremia ambaye rafiki zake walimsaidia kukabiliana na hali ngumu zilizokuwepo kabla ya Yerusalemu kuharibiwa. * Tunaweza kumwigaje Yeremia?

JIFUNZE KUTOKA KWA YEREMIA

3. (a) Ni nini ambacho huenda kingemfanya Yeremia ajitenge na wengine? (b) Yeremia alimfunulia nini Baruku, na matokeo yalikuwa nini?

3 Kwa miaka arobaini hivi, Yeremia aliishi miongoni mwa watu ambao hawakuwa washikamanifu, kutia ndani jirani zake na huenda pia baadhi ya watu wake wa ukoo kutoka katika mji wa nyumbani kwao wa Anathothi. (Yer. 11:21; 12:6) Hata hivyo, hakujitenga na wengine. Isitoshe, alifunua hisia zake kwa Baruku, mwandishi wake mshikamanifu, na mwishowe kwetu pia. (Yer. 8:21; 9:1; 20:14-18; 45:1) Tunaweza kuwazia jinsi Baruku na Yeremia walivyositawisha upendo wenye nguvu na heshima, Baruku alipokuwa akiandika masimulizi kumhusu Yeremia.—Yer. 20:1, 2; 26:7-11.

4. Yehova alimwambia Yeremia afanye nini, na mgawo huo uliimarishaje urafiki kati ya Yeremia na Baruku?

4 Kwa miaka mingi, Yeremia aliwaonya Waisraeli kwa ujasiri kuhusu mambo ambayo yangelipata jiji la Yerusalemu. (Yer. 25:3) Katika jitihada nyingine ya kuwachochea watu wake ili watubu, Yehova alimwambia Yeremia aandike maonyo Yake kwenye kitabu cha kukunjwa. (Yer. 36:1-4) Yeremia na Baruku walipokuwa wakifanya kwa ukaribu kazi hiyo waliyopewa na Mungu ambayo huenda waliifanya kwa miezi kadhaa, bila shaka walikuwa na mazungumzo yenye kuimarisha imani.

5. Baruku alithibitikaje kuwa rafiki mzuri kwa Yeremia?

5 Wakati ulipofika wa kufunua mambo yaliyoandikwa kwenye kitabu hicho cha kukunjwa, Yeremia alimtegemea Baruku rafiki yake, ili kuwasilisha ujumbe huo. (Yer. 36:5, 6) Kwa ujasiri, Baruku alitimiza mgawo huo hatari. Je, unaweza kuwazia jinsi Yeremia alivyojivunia kwamba Baruku alienda kwenye ua wa hekalu na kufanya yale aliyoagizwa? (Yer. 36:8-10) Wakuu wa Yuda walisikia kuhusu jambo ambalo Baruku alikuwa amefanya, nao wakamwamuru awasomee kwa sauti kitabu hicho cha kukunjwa! (Yer. 36:14, 15) Wakuu hao waliamua kumwambia Mfalme Yehoyakimu mambo ambayo Yeremia alisema. Kwa fadhili, walimwambia Baruku hivi: “Nenda ujifiche, wewe pamoja na Yeremia, na msiache mtu yeyote ajue mahali mlipo.” (Yer. 36:16-19) Huo ulikuwa ushauri mzuri!

6. Yeremia na Baruku walitendaje walipokabili upinzani?

6 Mfalme Yehoyakimu alikasirika sana aliposikia maneno ambayo Yeremia aliandika hivi kwamba akakiteketeza kitabu hicho cha kukunjwa na kuamuru Yeremia na Baruku wakamatwe. Hata hivyo, Yeremia hakuogopa. Alichukua kitabu kingine cha kukunjwa, akampa Baruku, naye Yeremia alipokuwa akimwambia ujumbe wa Yehova, Baruku aliandika ‘maneno yote yaliyokuwa katika kile kitabu cha kukunjwa ambacho Mfalme Yehoyakimu wa Yuda alikuwa amekiteketeza motoni.’—Yer. 36:26-28, 32.

7. Huenda kulikuwa na matokeo gani Yeremia na Baruku walipofanya kazi pamoja?

7 Mara nyingi, watu wanaokabili hali ngumu pamoja husitawisha uhusiano wa karibu. Hivyo, inawezekana kwamba Yeremia na Baruku walipokuwa wakifanya kazi pamoja ili kuandika upya kitabu cha kukunjwa kilichoharibiwa na Mfalme mwovu Yehoyakimu, walifahamiana vizuri na kuwa marafiki wa karibu. Mfano wa wanaume hao waaminifu unaweza kutunufaishaje?

MAZUNGUMZO YA KUTOKA MOYONI

8. Ni mambo gani yanayoweza kutuzuia kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na wengine, na kwa nini hatupaswi kufa moyo?

8 Huenda ikawa vigumu kwetu kufunua hisia zetu ikiwa mtu fulani alitukosea wakati uliopita. (Met. 18:19, 24) Au huenda tunahisi kwamba hatuna muda na nguvu za kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na wengine. Hata hivyo, hatupaswi kufa moyo. Ikiwa tunataka ndugu zetu watutegemeze majaribu yatakapokuja, ni lazima tujifunze kuwatumaini sasa kwa kuwafunulia hisia na mawazo yetu. Hiyo ni hatua muhimu itakayotusaidia kuwa marafiki wa kweli.—1 Pet. 1:22.

9. (a) Yesu alionyeshaje kwamba anawatumaini rafiki zake? (b) Kuzungumza waziwazi kuhusu hisia na mawazo yako kunaweza kuimarishaje uhusiano wako pamoja na wengine? Toa mfano.

9 Yesu alionyesha kwamba aliwatumaini rafiki zake kwa kuzungumza nao waziwazi kuhusu mawazo na hisia zake. (Yoh. 15:15) Tunaweza kumwiga kwa kuwaeleza wengine mambo yanayotuletea shangwe, yanayotuhangaisha, na yanayotuvunja moyo. Unaposikiliza kwa makini mtu fulani anapozungumza nawe, huenda ukatambua kwamba mawazo, hisia, na malengo yake mengi yanafanana na yako. Fikiria mfano wa Cindy, dada mwenye umri wa miaka 29. Alianzisha urafiki na Marie-Louise, dada painia mwenye umri wa miaka 67. Cindy na Marie-Louise huhubiri pamoja kila Alhamisi asubuhi, nao huzungumza pamoja kwa uhuru kuhusu mambo mbalimbali. Cindy anasema, “Ninafurahia kuwa na mazungumzo yenye kina pamoja na rafiki zangu kwa sababu hilo hunisaidia niwajue na kuwaelewa vizuri zaidi.” Urafiki husitawi watu wanapozungumza waziwazi kutoka moyoni. Kama Cindy, ikiwa utachukua hatua ya kwanza ili kuzungumza na wengine waziwazi kutoka moyoni, urafiki wako pamoja nao unaweza kusitawi.—Met. 27:9.

FANYA KAZI PAMOJA NA WENGINE

Marafiki wazuri hufanya kazi pamoja katika huduma (Tazama fungu la 10)

10. Kulingana na Methali 27:17, ni nini kinachoweza kutokea tunapofanya kazi pamoja na waamini wenzetu?

10 Kama ilivyokuwa katika kisa cha Yeremia na Baruku, tunapofanya kazi pamoja na waamini wenzetu na kujionea moja kwa moja sifa zao zenye kuvutia, tunajifunza kutoka kwao na kuzidi kuwa karibu nao. (Soma Methali 27:17.) Kwa mfano, unahisije unapokuwa katika huduma na kusikia rafiki yako akitetea imani yake kwa ujasiri au akizungumza kwa usadikisho na kutoka moyoni kumhusu Yehova na makusudi yake? Hapana shaka kwamba utampenda hata zaidi.

11-12. Toa mfano wa jinsi kushiriki katika huduma kunavyoweza kutusaidia kuimarisha urafiki wetu pamoja na wengine.

11 Fikiria mifano miwili inayoonyesha jinsi kufanya kazi pamoja katika huduma kunavyoweza kuwafanya watu wapendane zaidi. Adeline, dada mwenye umri wa miaka 23, alimwomba Candice, rafiki yake, waambatane pamoja ili kwenda kuhubiri kwenye eneo lisilohubiriwa kwa ukawaida. Anaeleza hivi: “Tulitaka kuhubiri kwa bidii zaidi na kufurahia huduma yetu zaidi. Sote tulihitaji kuchochewa zaidi kiroho.” Walinufaikaje? Adeline anasema hivi: “Kila siku baada ya utumishi, tulizungumzia jinsi tulivyohisi, mazungumzo yenye kugusa moyo tuliyofurahia, na jinsi tulivyojionea mwongozo wa Yehova katika huduma yetu. Sote tulifurahia mazungumzo hayo yenye kina na tukafahamiana vizuri hata zaidi.”

12 Laïla na Marianne, dada wawili waseja kutoka Ufaransa, walienda kuhubiri kwa majuma matano huko Bangui, mji mkuu wenye shughuli nyingi wa Jamhuri ya Afrika ya Kati. Laïla anakumbuka hivi: “Mimi na Marianne tulikabili hali ngumu, lakini kwa kuwa tulikuwa na mawasiliano mazuri na tulipendana kutoka moyoni, urafiki wetu uliimarika hata zaidi. Nilipojionea jinsi Marianne alivyozoea hali mpya, jinsi alivyowapenda wenyeji, na bidii yake katika huduma, nilimheshimu hata zaidi.” Si lazima uhamie nchi nyingine ili ufurahie faida hizo. Kila mara unapofanya kazi ya kuhubiri pamoja na ndugu au dada yako katika eneo lenu, una fursa ya kumjua vizuri zaidi na kuimarisha kifungo cha urafiki wenu.

KAZIA FIKIRA SIFA ZAO NZURI, NA UWE MWENYE KUSAMEHE

13. Ni changamoto gani tunayoweza kukabili tunapofanya kazi kwa ukaribu pamoja na rafiki zetu?

13 Nyakati nyingine tunapofanya kazi kwa ukaribu pamoja na rafiki zetu, hatuoni tu sifa zao nzuri lakini pia tunaanza kuona udhaifu wao mbalimbali. Ni nini kinachoweza kutusaidia kushughulika na changamoto hiyo? Fikiria tena mfano wa Yeremia. Ni nini kilichomsaidia kuona sifa nzuri za wengine na kutokazia udhaifu wao?

14. Yeremia alijifunza nini kumhusu Yehova, na jambo hilo lilimsaidiaje?

14 Inaelekea Yeremia ndiye aliyeandika kitabu cha kwanza na cha pili cha Wafalme na vilevile kitabu cha Yeremia. Bila shaka, mgawo huo ulimfanya atambue hata zaidi jinsi Yehova alivyo na rehema nyingi kuwaelekea wanadamu wasio wakamilifu. Kwa mfano, alijua kwamba Mfalme Ahabu alipotubu matendo yake maovu, Yehova alimwambia kwamba hangeharibu familia yake wakati wa uhai wake. (1 Fal. 21:27-29) Pia, Yeremia alijua kwamba Manase alimtendea Yehova uovu mwingi sana kuliko Ahabu. Licha ya hilo, Yehova alimsamehe Manase kwa sababu alitubu. (2 Fal. 21:16, 17; 2 Nya. 33:10-13) Bila shaka, masimulizi hayo yalimsaidia Yeremia kuiga subira na rehema ya Mungu alipokuwa akishughulika na rafiki zake wa karibu.—Zab. 103:8, 9.

15. Yeremia aliiga subira ya Yehova jinsi gani Baruku alipokengeuka?

15 Fikiria jinsi Yeremia alivyoshughulika na Baruku ambaye alikengeuka kidogo kwenye mgawo wake. Badala ya kufikiri kwamba Baruku hangeweza kubadilika, Yeremia alimsaidia rafiki yake kwa kumpa ujumbe wenye fadhili lakini ulio wazi kutoka kwa Mungu. (Yer. 45:1-5) Tunajifunza nini kutokana na simulizi hilo?

Marafiki wazuri husameheana kwa hiari (Tazama fungu la 16)

16. Kama inavyotajwa kwenye Methali 17:9, tunahitaji kufanya nini ili kuendeleza urafiki tulioanzisha?

16 Kihalisi, hatuwezi kutarajia ukamilifu kutoka kwa ndugu na dada zetu. Hivyo, baada ya kuanzisha urafiki wa karibu pamoja nao, tunahitaji kujitahidi sana kuendeleza vifungo vya urafiki tulivyoanzisha. Ikiwa rafiki zetu watafanya kosa fulani, huenda tukahitaji kuwapa shauri lenye fadhili lakini lililo wazi na linalotegemea Neno la Mungu. (Zab. 141:5) Na ikiwa wametuumiza au kutukosea, tunahitaji kuwasamehe. Baada ya kuwasamehe, ni lazima tuepuke mtego wa kuzungumzia tena jambo hilo wakati ujao. (Soma Methali 17:9.) Ni jambo la muhimu sana katika nyakati hizi ngumu kukazia fikira sifa nzuri za ndugu na dada zetu badala ya udhaifu wao! Kufanya hivyo kunaimarisha kifungo cha urafiki wetu, na ni muhimu kufanya hivyo sasa kwa sababu tutahitaji marafiki wa karibu wakati wa dhiki kuu.

TENDA KWA UPENDO MSHIKAMANIFU

17. Nabii Yeremia alithibitikaje kuwa rafiki wa kweli katika nyakati zenye taabu?

17 Nabii Yeremia alithibitika kuwa rafiki wa kweli katika nyakati zenye taabu. Kwa mfano, baada ya Ebed-meleki ofisa wa makao ya mfalme kumwokoa Yeremia ili asife katika tangi lililokuwa limejaa matope, Ebed-meleki aliogopa kwamba wakuu wangemdhuru. Yeremia alipopata habari hizo, hakukaa kimya, akifikiri kwamba kwa njia fulani rafiki yake atakabiliana na hali hiyo mwenyewe. Ingawa Yeremia alikuwa gerezani, alifanya yote aliyoweza ili kumtia moyo Ebed-meleki rafiki yake kwa kumweleza kuhusu ahadi yenye kufariji kutoka kwa Yehova.—Yer. 38:7-13; 39:15-18.

Marafiki wazuri huwasaidia ndugu na dada zao wenye uhitaji (Tazama fungu la 18)

18. Kulingana na Methali 17:17, tunapaswa kutendaje rafiki yetu anapopitia hali ngumu?

18 Leo, ndugu na dada zetu hukabili changamoto mbalimbali. Kwa mfano, wengi hukumbwa na majanga yanayosababishwa na wanadamu au misiba ya asili. Mambo hayo yanapotokea, huenda baadhi yetu tukafaulu kuwakaribisha ndugu na dada zetu katika nyumba zetu. Huenda wengine wakatoa msaada wa kifedha. Lakini sisi sote tunaweza kumwomba Yehova awasaidie ndugu na dada zetu. Ukipata habari kwamba ndugu au dada amevunjika moyo, huenda usijue jambo la kumwambia au la kufanya. Lakini sote tunaweza kutimiza mengi. Kwa mfano, tunaweza kutenga wakati ili kuwa pamoja na rafiki yetu. Tunaweza kumsikiliza kwa huruma anapozungumza. Na tunaweza kumsomea andiko lenye kufariji tunalolipenda. (Isa. 50:4) Jambo muhimu zaidi ni kwamba tunapatikana ili kuwasaidia rafiki zetu wanapotuhitaji.—Soma Methali 17:17.

19. Kuimarisha urafiki wenye nguvu sasa kutatusaidiaje wakati ujao?

19 Ni lazima tuazimie sasa kuimarisha na kudumisha urafiki wenye nguvu pamoja na ndugu na dada zetu. Kwa nini? Kwa sababu adui zetu watajaribu kutugawanya kwa kutumia habari za uwongo au zisizo za kweli. Watajaribu kutufanya tuwatilie shaka ndugu zetu. Lakini jitihada zao hazitafanikiwa. Hawatafaulu kuvunja vifungo vyetu vya upendo. Hakuna chochote watakachofanya kitakachoweza kuvunja urafiki tuliositawisha pamoja na ndugu na dada zetu. Ukweli ni kwamba, urafiki huo hautadumu tu kufikia mwisho wa mfumo huu wa mambo bali utaendelea milele na milele!

WIMBO 24 Njooni Kwenye Mlima wa Yehova

^ fu. 5 Kadiri mwisho unavyozidi kukaribia, sote tunahitaji kuimarisha uhusiano wetu pamoja na waamini wenzetu. Katika makala hii, tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mambo yaliyompata Yeremia. Pia, tutazungumzia jinsi ambavyo kusitawisha urafiki wa karibu pamoja na wengine leo, kunavyoweza kutusaidia katika nyakati ngumu.

^ fu. 2 Masimulizi yaliyo kwenye kitabu cha Yeremia hayajapangwa kulingana na mfuatano wa matukio.

^ fu. 57 MAELEZO YA PICHA: Picha hii inaonyesha jambo linaloweza kutokea wakati wa “dhiki kuu.” Ndugu na dada kadhaa wanakutana mahali salama kwenye nyumba ya ndugu. Wanafarijika kwa kushirikiana pamoja wakati huo wa majaribu. Picha tatu zinazofuata zinaonyesha kwamba ndugu na dada hawa walikuwa wameimarisha urafiki wenye nguvu kwa muda mrefu kabla ya dhiki kuu kuanza.