Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ee Yehova, . . . Unanijua”

“Ee Yehova, . . . Unanijua”

Mkaribie Mungu

“Ee Yehova, . . . Unanijua”

“HAKUNA mzigo mkubwa zaidi ambao mtu anaweza kubeba kuliko kujua kwamba hakuna mtu anayemjali wala kumwelewa.” * Je, nyakati nyingine unahisi hivyo? Je, umewahi kuhisi kwamba hakuna mtu anayekujali wala anayeelewa hali zako na hisia zako? Ikiwa ndivyo, maneno yanayofuata yanaweza kukufariji: Yehova anawajali sana waabudu wake hivi kwamba anazingatia mambo yote yanayowapata wanapoendelea na shughuli zao za kila siku. Maneno ya Daudi kwenye Zaburi 139 yanatuhakikishia jambo hilo.

Daudi aliandika hivi akiwa na uhakika kwamba Mungu anamjali: “Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua.” (Mstari wa 1) Hapa Daudi anatumia usemi wa mfano wenye kupendeza. Kitenzi cha Kiebrania kinachotafsiriwa ‘kuchunguza kabisa’ kinaweza kurejelea tendo la kuchimba madini (Ayubu 28:3), kupeleleza nchi (Waamuzi 18:2), au kuchunguza mambo ya hakika kuhusu kesi fulani (Kumbukumbu la Torati 13:14). Ndiyo, Yehova anatujua vizuri sana, ni kana kwamba amechunguza kila sehemu ya maisha yetu. Kwa kutumia neno “umenichunguza,” Daudi anatufundisha kwamba Mungu anapendezwa kibinafsi na watumishi wake. Anawachunguza kabisa na anajua kila mmoja wao.

Daudi anatoa ufafanuzi zaidi unaoonyesha kwamba Mungu anatuchunguza kwa makini sana, akisema hivi: “Wewe mwenyewe umepata kujua kuketi kwangu na kusimama kwangu. Umeichunguza fikira yangu tokea mbali.” (Mstari wa 2) Kwa njia fulani, Yehova anakaa “mbali,” yaani, mbinguni. Hata hivyo, anajua wakati tunapoketi chini, labda baada ya siku yenye shughuli nyingi, na tunapoamka asubuhi na kuanza shughuli zetu za kila siku. Pia, anajua mawazo, tamaa, na nia zetu. Je, Daudi anaogopa kuchunguzwa kwa undani hivyo? Hapana. Anafurahia jambo hilo. (Mstari wa 23, 24) Kwa nini?

Daudi anajua kwamba Yehova anawachunguza waabudu wake akiwa na nia nzuri. Anarejelea nia hiyo anapoandika: “Umepima kusafiri kwangu na kulala kwangu nikiwa nimejinyoosha, nawe umezijua njia zangu zote.” (Mstari wa 3) Kila siku, Yehova anaona ‘njia zetu zote,’ yaani, makosa yetu na pia matendo yetu mazuri. Je, anakazia fikira mambo mabaya au anakazia yale mazuri? Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “umepima” linaweza kumaanisha “kupepeta,” sawa na vile mkulima anavyopepeta makapi ili kupata nafaka. Neno “umezijua” ni tafsiri ya neno la Kiebrania linaloweza kumaanisha “kuthamini.” Anapochunguza mambo ambayo waabudu wake husema na kufanya kila siku, Yehova anathamini yale mazuri. Kwa nini? Anathamini jitihada zao za kumpendeza.

Zaburi sura ya 139 inatufundisha kwamba Yehova anawajali sana waabudu wake. Anawachunguza kwa makini na kuwatazama wanapoendelea na shughuli zao za kila siku. Hivyo, anajua matatizo wanayopata, na anaelewa maumivu ya moyoni na ya akilini ambayo yanaweza kusababishwa na hali hizo ngumu. Je, unachochewa kumwabudu Mungu huyo mwenye kujali? Ikiwa ndivyo, basi unaweza kuwa na uhakika huu: Yehova ‘hatasahau kazi yako na upendo unaoonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Waebrania 6:10.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Septemba:

Zaburi 119-150

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Maneno ya mwandishi Arthur H. Stainback.