Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtu Anayekubalika kwa Moyo wa Yehova

Mtu Anayekubalika kwa Moyo wa Yehova

Mtu Anayekubalika kwa Moyo wa Yehova

NI NINI kinachokuja akilini mwako unapomfikiria Daudi anayetajwa kwenye Biblia? Je, ni jinsi alivyomshinda Goliathi, lile jitu la Wafilisti? Je, ni wakati alipokimbilia nyikani ili asiuawe na Mfalme Sauli mwenye chuki? Je, ni dhambi aliyotenda na Bath-sheba na matatizo yaliyompata kwa sababu ya dhambi hiyo? Au je, labda unakumbuka mashairi aliyoandika kwa mwongozo wa roho ya Mungu na ambayo yamehifadhiwa katika kitabu cha Biblia cha Zaburi?

Daudi alipata mapendeleo, ushindi, na misiba mingi katika maisha yake. Hata hivyo, zaidi ya mambo yote, kinachotuvutia kwake ni jambo ambalo nabii Samweli alisema kumhusu Daudi—angethibitika kuwa “mtu anayekubalika kwa moyo [wa Yehova].”—1 Samweli 13:14.

Unabii wa Samweli ulitimizwa Daudi alipokuwa bado kijana. Je, hungefurahia kutajwa kuwa mtu anayekubalika kwa moyo wa Yehova? Kwa hiyo, ni mambo gani unayoweza kujifunza katika maisha ya Daudi, hasa alipokuwa kijana, ambayo yanaweza kukusaidia ukubalike kwa Yehova? Acheni tuone.

Kazi na Familia Yake

Yaelekea kwamba Yese, aliyekuwa baba ya Daudi na mjukuu wa Ruthu na Boazi, alikuwa mtumishi mwaminifu wa Yehova. Wakati Daudi, ndugu zake saba, na dada zake wawili walipokuwa wadogo, Yese aliwafundisha Sheria ya Musa. Katika mojawapo ya zaburi zake, Daudi anajitaja kuwa mwana wa “kijakazi” wa Yehova. (Zaburi 86:16) Jambo hilo limefanya watu fulani waseme kwamba mama ya Daudi, ambaye hatajwi katika Biblia, alihusika pia katika kumsaidia kuwa mtu wa kiroho. Msomi mmoja anasema hivi: “Inaelekea Daudi alijifunza kutoka kwa mama yake mambo yenye kusisimua kuhusu jinsi Mungu alivyoshughulika zamani na watu wake,” kutia ndani Ruthu na Boazi.

Anapotajwa kwa mara ya kwanza, Daudi ni mvulana mchungaji ambaye ana jukumu la kuchunga kondoo za baba yake. Inawezekana jukumu hilo lilitia ndani kukaa malishoni akiwa peke yake kwa siku kadhaa. Hebu wazia hali hiyo.

Familia ya Daudi iliishi Bethlehemu, mji mdogo uliokuwa kwenye kilele na miteremko ya eneo fulani kwenye milima ya Yuda. Mashamba yenye mawemawe yaliyokuwa katika eneo hilo la Bethlehemu yalitoa mazao mengi ya nafaka. Nayo mashamba ya matunda, mizeituni, na mizabibu yalikuwa kwenye bonde na katika miteremko isiyo mikali sana. Katika siku za Daudi, yaelekea maeneo yaliyoinuka ambayo hayakuwa yakilimwa yalitumiwa kwa malisho. Maeneo hayo yalikuwa karibu na nyika ya Yuda.

Daudi alikabili hatari mbalimbali akiwa mchungaji. Ni katika milima hiyo ambapo Daudi alipambana na simba na dubu waliojaribu kuchukua kondoo aliokuwa akichunga. * Kijana huyo mjasiri aliwakimbiza wanyama hao wawindaji, akawaua, na kuwaokoa kondoo wake kutoka midomoni mwao. (1 Samweli 17:34-36) Huenda ni wakati huo ambapo Daudi alipata ustadi wa kutumia kombeo. Eneo la kabila la Benyamini lilikuwa karibu na mji wao. Walenga shabaha wa kabila hilo walitupa mawe kwa kombeo na wangeweza “kupiga shabaha unywele, bila kukosea.” Daudi pia alikuwa na ustadi kama huo wa kutumia kombeo.—Waamuzi 20:14-16; 1 Samweli 17:49.

Alitumia Wakati Wake Vizuri

Mchungaji alitumia wakati wake mwingi akiwa ametulia na akiwa peke yake. Lakini Daudi hakuruhusu achoshwe na maisha hayo. Badala yake, hali hiyo ya utulivu ilimwezesha Daudi kupata nafasi nyingi za kutafakari. Inaonekana kwamba mambo fulani ambayo Daudi anataja katika zaburi zake aliyatafakari alipokuwa kijana. Je, ni wakati huo alipokuwa peke yake alipotafakari kuhusu mahali pa mwanadamu katika mpango wa Mungu na pia kuhusu uumbaji wenye kustaajabisha ulio mbinguni, yaani, jua, mwezi, na nyota, “kazi za vidole [vya Yehova]”? Je, ni katika mashamba yaliyokuwa Bethlehemu alipotafakari kuhusu ardhi yenye rutuba, mifugo na ng’ombe wa kulima, ndege na “wanyama wa porini”?—Zaburi 8:3-9; 19:1-6.

Bila shaka, mambo ambayo Daudi alipitia akiwa mchungaji yalimfanya ajionee kwa njia iliyo wazi hata zaidi jinsi Yehova anavyowatendea watumishi wake waaminifu kwa wororo. Hivyo Daudi aliimba hivi: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote. Ananilaza katika malisho yenye majani mengi; ananiongoza kando ya mahali pa kupumzika palipo na maji ya kutosha. Hata ingawa ninatembea katika bonde lenye kivuli kizito, siogopi chochote kibaya, kwa maana wewe uko pamoja nami; fimbo yako na gongo lako ndivyo vitu vinavyonifariji.”—Zaburi 23:1, 2, 4.

Huenda ukajiuliza mambo hayo yote, yanakuhusu jinsi gani? Jibu ni kwamba sababu moja iliyomfanya Daudi awe na uhusiano wa karibu na Yehova na kuitwa “mtu anayekubalika kwa moyo wake” ni kwamba alitafakari kwa uzito sana kazi za Yehova na uhusiano wake na Mungu. Je, wewe unaweza kuwa kama Daudi?

Je, umewahi kusukumwa kumsifu na kumtukuza Muumba baada ya kuchunguza kwa makini kitu fulani alichoumba? Je, umewahi kuhisi moyo wako umejaa upendo kwa Yehova baada ya kuona sifa zake kupitia jinsi anavyoshughulika na wanadamu? Kwa kawaida, ili uwe na uthamini kama huo, unapaswa kusali kwa Yehova na utenge wakati wa kutafakari kwa utulivu Neno la Mungu na uumbaji wake. Kutafakari kwa njia hiyo kunaweza kukusaidia kumjua Yehova kwa undani zaidi—na hivyo kumpenda. Vijana kwa wazee wanaweza kuwa na pendeleo hilo. Inaelekea Daudi alikuwa na uhusiano wa karibu na Yehova tangu alipokuwa kijana. Tunajuaje hilo?

Daudi Atiwa Mafuta

Mfalme Sauli aliposhindwa kuwaongoza watu wa Mungu, Yehova alimwambia nabii Samweli hivi: “Ni mpaka wakati gani utamwombolezea Sauli, huku mimi, kwa upande mwingine, nimemkataa asitawale akiwa mfalme juu ya Israeli? Jaza pembe yako mafuta, nawe uende. Nitakutuma kwa Yese Mbethlehemu, kwa maana nimejipatia mfalme kati ya wanawe.”—1 Samweli 16:1.

Nabii wa Mungu alipofika Bethlehemu, alimwambia Yese awaite watoto wake wa kiume. Samweli angemtia mafuta mwana yupi awe mfalme? Baada ya kumwona Eliabu, mwana wa kwanza, ambaye alikuwa na sura nzuri, Samweli aliwaza hivi: ‘Huyu ndiye.’ Lakini Yehova akamwambia: “Usiangalie sura yake wala urefu wa umbo lake, kwa maana nimemkataa. Kwa kuwa Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona, kwa maana mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” Vivyo hivyo, Yehova alimkataa Abinadabu, Shama, na ndugu zao wengine wanne. “Mwishowe” simulizi hilo linaendelea kusema, “Samweli akamwambia Yese: ‘Je, hawa ndio wavulana wote?’ Naye akasema: ‘Aliye mdogo zaidi ameachwa mpaka sasa, na tazama! analisha kondoo.’”—1 Samweli 16:6, 7, 11.

Ni kana kwamba Yese alikuwa akisema: ‘Haiwezekani kwamba unamtafuta Daudi?’ Kwa kuwa Daudi ndiye aliyekuwa mdogo zaidi, baba yake alikuwa amempa kazi ya kuchunga kondoo. Lakini, Mungu alikuwa amemchagua yeye. Yehova huona jinsi moyo ulivyo, na bila shaka aliona jambo fulani lenye kupendeza sana katika moyo wa Daudi. Kwa hiyo, Yese aliposema Daudi aitwe, Yehova alimwambia Samweli: “‘Simama, mtie mafuta, kwa maana huyu ndiye!’ Basi Samweli akachukua ile pembe ya mafuta, akamtia mafuta katikati ya ndugu zake. Na roho ya Yehova ikaanza kutenda kazi juu ya Daudi kuanzia siku hiyo na kuendelea.”—1 Samweli 16:12, 13.

Biblia haitaji Daudi alikuwa na umri gani mambo hayo yalipotukia. Hata hivyo, muda fulani baadaye, ndugu watatu wa Daudi, Eliabu, Abinadabu, na Shama, walianza kutumikia katika jeshi la Sauli. Huenda wale wengine watano walikuwa na umri mdogo sana hivi kwamba hangeweza kujiunga na jeshi. Inawezekana kwamba walikuwa chini ya umri wa miaka 20, umri ambao wanaume waliruhusiwa kujiunga na jeshi la Israeli. (Hesabu 1:3; 1 Samweli 17:13) Vyovyote vile, Daudi alikuwa na umri mdogo sana Yehova alipomchagua. Hata hivyo, inaonekana tayari Daudi alikuwa mtu wa kiroho sana. Inaelekea alikuwa na uhusiano wa karibu na Yehova, ambao alisitawisha kwa kutafakari mambo aliyojua kumhusu Mungu.

Leo, vijana wanapaswa kutiwa moyo wafanye hivyo pia. Kwa hiyo, je, wazazi mnawatia moyo watoto wenu watafakari mambo ya kiroho, wathamini uumbaji wa Mungu, na kujifunza mambo ambayo Biblia inasema kumhusu Muumba? (Kumbukumbu la Torati 6:4-9) Nanyi vijana, je, mnafanya mambo hayo bila kusukumwa? Machapisho yanayotegemea Biblia kama vile magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! * yamekusudiwa kuwasaidia.

Mwenye Ustadi wa Kupiga Kinubi

Kama vile tu maneno ya zaburi nyingi za Daudi yanavyoonyesha kuhusu siku zake akiwa mchungaji, yaelekea pia muziki wake unafunua jambo fulani kumhusu. Bila shaka, muziki uliochezwa ili kuambatana na nyimbo hizo takatifu haupatikani leo. Hata hivyo, tunajua kwamba mtunzi wa muziki huo alikuwa mwanamuziki stadi. Kwa kweli, sababu iliyofanya Daudi aitwe kutoka malishoni ili amtumikie Mfalme Sauli ni kwamba alikuwa mwenye ustadi wa kupiga kinubi.—1 Samweli 16:18-23. *

Daudi alisitawisha ustadi huo wakati gani na akiwa wapi? Inaonekana ni wakati alipokuwa malishoni akichunga kondoo. Inapatana na akili kusema kwamba hata alipokuwa na umri mdogo, tayari Daudi alikuwa akimwimbia Mungu sifa kutoka moyoni. Kwa kweli, Yehova alimchagua kwa sababu alikuwa amejitolea na hali yake ya kiroho ilikuwa nzuri.

Tumezungumzia tu maisha ya Daudi alipokuwa kijana. Lakini roho aliyoonyesha katika maisha yake yote inaonekana katika maneno ambayo huenda yalichochewa na mambo yaliyompata zamani akiwa malishoni karibu na Bethlehemu. Hebu wazia Daudi akimwimbia Yehova hivi: “Nimezikumbuka siku za zamani za kale; nimetafakari juu ya utendaji wako wote; kwa kupenda niliendelea kuhangaikia kazi ya mikono yako mwenyewe.” (Zaburi 143:5) Maneno yenye kugusa moyo ya zaburi hii, na nyingine nyingi za Daudi, yanaweza kumchochea yeyote anayetamani kukubalika kwa moyo wa Yehova.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 9 Dubu wa rangi ya kahawia wa Siria waliopatikana katika eneo la Palestina, walikuwa na uzito wa kilo 140 hivi na walikuwa na uwezo wa kuua mnyama au mwanadamu kwa kumpiga kwa miguu yao mikubwa ya mbele. Wakati fulani kulikuwa na simba wengi katika eneo hilo. Andiko la Isaya 31:4 linasema kuwa hata “hesabu kamili ya wachungaji” hawangeweza kumfukuza “mwana-simba mwenye manyoya shingoni” kutoka kwa windo lake.

^ fu. 20 Yanayochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 22 Mshauri wa mfalme aliyempendekeza Daudi alisema kwamba Daudi alikuwa “msemaji mwenye akili na mwanamume mwenye umbo zuri, na Yehova [alikuwa] pamoja naye.”—1 Samweli 16:18.