Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Olivétan—“Mtafsiri Mnyenyekevu” wa Biblia ya Kifaransa

Olivétan—“Mtafsiri Mnyenyekevu” wa Biblia ya Kifaransa

Olivétan​—“Mtafsiri Mnyenyekevu” wa Biblia ya Kifaransa

Ilikuwa Septemba 13, 1540, na polisi walikuwa wakipekua nyumba ya Collin Pellenc. Katika chumba fulani cha siri, walipata hati walizoshuku, kutia ndani kitabu fulani kikubwa. Katika ukurasa wa pili wa kitabu hicho kulikuwa na maneno: “P. Robert Olivetanus, mtafsiri mnyenyekevu.” Ilikuwa Biblia ya Wawaldo! Collin Pellenc alikamatwa, akashtakiwa kuwa mwasi wa kidini, na kuteketezwa akiwa hai.

NCHINI Ufaransa wakati huo, kama tu sehemu nyingine za Ulaya, Kanisa Katoliki lilikuwa likiwatafuta viongozi wa Marekebisho Makubwa ya Kidini ili kukomesha mafundisho yao “hatari.” Mmoja wa viongozi hao, Guillaume Farel aliyetetea vikali marekebisho hayo, aliazimia kuyashawishi mataifa yaliyozungumza Kifaransa yafuate maoni ya Martin Luther, kiongozi mkuu wa Marekebisho Makubwa ya Kiprotestanti. Farel, kutoka Mkoa wa Dauphiné ulio kusini-mashariki mwa Ufaransa, alijua kwamba njia moja kuu ya kubadili maoni ya watu ni kupitia vitabu. Ili atimize jambo hilo alihitaji vijitabu, makala mbalimbali, na Biblia pia. Lakini ni nani angelipia kazi hiyo? Aliamua kutafuta msaada kutoka kwa Wawaldo, kikundi cha kidini chenye kujitegemea ambacho kilikuwa kimejitolea kuhubiri kuhusu Biblia.

Mkutano wa Kidini Wafanywa Chanforan

Katikati ya mwezi wa Septemba 1532, makasisi wa Wawaldo walioitwa barbes walifanya mkutano, au kongamano la kidini, huko Chanforan, mji mdogo ulio karibu na Turin, nchini Italia. Kwa miaka kadhaa, Wawaldo na viongozi wa Marekebisho Makubwa ya Kidini walikuwa wakibadilishana mawazo. Hivyo, Farel na wanaume wengine wachache wakaalikwa kwenye mkutano huo. Wawaldo walitaka kujua ikiwa mafundisho yao yalipatana na mafundisho ya Luther na wanafunzi wake. *

Farel aliongea kwa njia yenye kushawishi katika mkutano huo wa Chanforan. Makasisi wa Wawaldo walipomwonyesha Biblia yao iliyozeeka ambayo ilikuwa imeandikwa kwa mkono na kwa lugha yao wenyewe, Farel aliwashawishi watoe pesa za kusimamia kuchapwa kwa Biblia katika Kifaransa. Tofauti na Biblia iliyotafsiriwa na Lefèvre d’Étaples mwaka wa 1523 kutoka kwa Kilatini, Biblia hii ingetafsiriwa kutoka kwa Kiebrania na Kigiriki. Lakini ni nani angeweza kufanya kazi hiyo?

Farel alijua mtu ambaye angeweza kuifanya. Aliitwa Pierre Robert, lakini alijulikana kama Olivétan, * mwalimu kijana aliyezaliwa katika eneo la Picardy, kaskazini mwa Ufaransa. Olivétan, ambaye alikuwa binamu ya John Calvin, aliunga mkono Marekebisho Makubwa ya Kidini na alikuwa mwenye kutegemeka. Pia, kwa miaka kadhaa alikaa huko Strasbourg akijifunza kwa makini lugha za Biblia.

Kama Farel na wengine wengi, Olivétan pia alikuwa mkimbizi nchini Uswisi. Rafiki zake walimsihi akubali kazi hiyo ya kutafsiri. Baada ya kukataa mara kadhaa, mwishowe alikubali kutafsiri Biblia “katika Kifaransa kutoka kwa Kiebrania na Kigiriki.” Wakati huohuo, Wawaldo walitoa kiasi kikubwa cha pesa kati ya zile zilizohitajiwa.

Kunguru na Kurumbiza

Mwanzoni mwa mwaka wa 1534, Olivétan alijitenga na kwenda kwenye milima ya Alps na akaanza kazi yake, akiwa amezungukwa na “walimu wake,” yaani, vitabu vyake. Maktaba yake ilikuwa na vitabu vizuri ambavyo msomi yeyote wa kisasa angetamani kuwa navyo. Maktaba hiyo ilikuwa na Biblia za lugha ya Kisiria, Kigiriki na Kilatini, vitabu vya maelezo ya Warabi, vitabu vya sarufi ya Wakaldayo, na vingine vingi. Jambo la maana zaidi ni kwamba alikuwa na tafsiri ya karibuni zaidi ya Biblia ya Venice iliyoandikwa kwa Kiebrania cha awali.

Olivétan alitafsiri sehemu inayojulikana kama Agano Jipya akitegemea tafsiri ya Kifaransa ya Lefèvre d’Étaples, ingawa mara nyingi alitumia pia maandishi ya Kigiriki ya msomi Mholanzi aliyeitwa Erasmus. Mara nyingi, Olivétan alichagua maneno ambayo yalipunguza nguvu mafundisho ya Kikatoliki. Kwa mfano alichagua neno “mwangalizi” badala ya “askofu,” “siri” badala ya “fumbo,” na “kutaniko” badala ya “kanisa.”

Olivétan aliazimia kutafsiri sehemu ya Agano la Kale neno kwa neno kutoka kwa maandishi ya awali ya Kiebrania. Alisema kwa utani kwamba kutafsiri Kifaransa kutoka kwa Kiebrania ni kama “kumfundisha kurumbiza mwenye sauti nzuri kuimba wimbo wa kunguru mwenye sauti isiyopendeza”!

Katika maandishi ya Kiebrania, Olivétan alipata mara nyingi sana jina la Mungu likiwa katika herufi za Tetragramatoni. Aliamua kutafsiri jina hilo kuwa “Wa Milele,” maneno ambayo baadaye yalitumiwa sana katika Biblia za Kiprotestanti za Kifaransa. Hata hivyo, katika mistari fulani alichagua kutumia jina “Yehova,” hasa katika andiko la Kutoka 6:3.

Jambo la kushangaza ni kwamba Februari 12, 1535 (12/2/1535), baada ya mwaka mmoja hivi, Olivétan alitangaza kuwa amemaliza kazi yake! Kwa kuwa alikubali kwamba “tayari alikuwa amebeba mzigo huo [wa kutafsiri] kwa muda mrefu akiwa peke yake,” ni wazi kwamba mwaka wa 1534/1535 ulikuwa umalizio wa kazi ngumu aliyokuwa ameifanya kwa miaka mingi. Alisema hivi kwa unyenyekevu, “Nimefanya yote ninayoweza.” Sasa kazi iliyokuwa imebaki ni kuchapa Biblia hiyo ya kwanza ya Kifaransa ambayo ilitafsiriwa kwa kuzingatia lugha za awali.

Chumba cha Kuchapia cha Pirot

Sasa, Pierre de Wingle, kwa jina lingine Pirot Picard, ambaye alikuwa rafiki ya Farel na pia mchapaji aliyeunga mkono Marekebisho Makubwa ya Kidini, alianza kazi hiyo ya kuchapa. Baada ya Kanisa Katoliki kumfukuza jijini Lyon, de Wingle alihamia Neuchâtel, nchini Uswisi, mwaka wa 1533. Akitumia pesa zilizotolewa na Wawaldo, de Wingle alianza kuchapisha kwa wingi habari za “uchochezi.” Kwa mfano, alichapisha mabango yenye ujumbe ulioshtumu Misa na baadhi ya mabango hayo yalimfikia Mfalme Francis wa Kwanza wa Ufaransa aliyekuwa Mkatoliki.

Mashine za de Wingle zilianza kazi tena—wakati huu alikuwa akichapa Biblia! Ili kazi hiyo ifanywe kwa haraka, mashine mbili zilitumiwa na kila mashine ilikuwa na wafanyakazi wanne au watano, ambao walipanga maandishi na kuyachapa kwenye karatasi. Mwishowe, “tarehe 4, mwezi wa Juni mwaka wa 1535,” de Wingle aliweka sahihi kwenye ukurasa wa mchapishaji katika Biblia hiyo ya Olivétan. Katika utangulizi wa Biblia hiyo Olivétan alisema kwamba alifanya kazi hiyo kwa ajili ya waamini maskini ambao “walikandamizwa na kulemezwa” na “mapokeo yasiyo na maana.”

Matokeo ya mwisho yalitimiza matazamio yao yote. Mambo yaliyofanya Biblia hiyo ya Kifaransa iwe yenye kuvutia na rahisi kusoma ni kwamba iliandikwa kwa maandishi yenye kupendeza ya Wagothi ambayo yalipangwa katika safu mbili na kugawanywa katika sura na mafungu. Maelezo ya pambizoni yanaonyesha kwamba Olivétan alikuwa mtafsiri stadi. Maelezo ya utangulizi, nyongeza, chati, na mashairi pia yaliboresha kazi hiyo. Mwishoni mwa Biblia hiyo, maneno haya ya kishairi yanaonyesha kwamba “Wawaldo, ambao ni wahubiri wa Injili, waliwasaidia watu kupata hazina hii.”

Kazi Bora . . . Ambayo Haikufanikiwa

Ingawa Biblia ya Olivétan ilidharauliwa mwanzoni, leo inatambuliwa kuwa mojawapo ya kazi ambayo imefanywa kwa ustadi mkubwa zaidi. Isitoshe, kwa karne tatu, tafsiri yake ilitumiwa kama msingi wa tafsiri nyingine za Biblia za Waprotestanti.

Ingawa walitokeza Biblia elfu moja hivi, hazikununuliwa sana. Hiyo ni kwa sababu hakukuwa na mpango mzuri wa kusambaza Biblia hizo, na pia kwa sababu wakati huo lugha ya Kifaransa ilikuwa ikibadilika haraka sana. Zaidi ya hayo, Biblia hiyo yenye uzito wa kilo 5 haikuwafaa wasafiri wala watu waliotaka kuisoma kisiri.

Ingawa nakala moja ya Biblia ya Olivétan ilimfikia Collin Pellenc huko Ufaransa, kama iliyotajwa mwanzoni mwa habari hii, bado hazikuuzwa kwa wingi. Katika mwaka wa 1670, karibu karne moja na nusu hivi baadaye, bado duka moja la vitabu jijini Geneva lilikuwa na nakala ya Biblia hiyo.

“Asiye na Jina Wala Makao”

Olivétan alipokamilisha kazi yake, hakujitokeza tena waziwazi. Akitumia majina bandia, alianza kusahihisha Agano Jipya na sehemu fulani za Agano la Kale. Pia, alianza kufanya kazi nyingine aliyoipenda sana, yaani, kufundisha. Kwa sababu alikuwa mwalimu aliyewafikiria sana wanafunzi wake, Olivétan alisahihisha kitabu Mafundisho kwa Watoto, ambacho kilikusudiwa kuwafundisha watoto maadili yanayofaa na kuwafundisha kusoma Kifaransa. Mafundisho hayo yote yalitegemea Biblia. Mojawapo ya majina bandia ambayo alitumia ni Belisem de Belimakom, linalomaanisha “Asiye na Jina Wala Makao.”

Inaelekea Olivétan alifia jijini Rome mwaka wa 1538, akiwa na miaka 30 hivi. Ni watu wachache wanaofahamu jukumu muhimu ambalo msomi huyu kijana kutoka Picardy alitimiza katika kusambazwa kwa Biblia ya Kifaransa. Jina lake linapatikana mara chache sana katika kamusi za Kiingereza. Huenda hilo lingemfurahisha “mtafsiri mnyenyekevu,” Louys Robert, ambaye pia alijulikana kama Olivétan!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Kwa habari zaidi kuhusu jinsi Wawaldo walivyokuja kujiunga na yale Marekebisho Makubwa ya Kidini, ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2002, ukurasa wa 20-23.

^ fu. 7 Alipozaliwa alipewa jina Louys Robert, kisha akajipa jina Pierre. Inaonekana jina la utani Olivétan, katika Kifaransa linarejelea mafuta mengi ya zeituni aliyotumia katika taa ili apate mwangaza kwa kuwa alifanya kazi kwa saa nyingi.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]

Archives de la Ville de Neuchâtel, Suisse /Photo: Stefano Iori

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 19]

Left photo: Alain Leprince - La Piscine-musée, Roubaix / Courtesy of the former Bouchard Museum, Paris

Center and right: Société de l’Histoire du Protestantisme Français, Paris

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

Société de l’Histoire du Protestantisme Français, Paris