Hamia kwenye habari

Mashahidi wa Yehova Wana Maoni Gani Kuhusu Mazishi?

Mashahidi wa Yehova Wana Maoni Gani Kuhusu Mazishi?

 Maoni yetu kuhusiana na mazishi yanategemea mafundisho ya Biblia. Yafuatayo ni baadhi ya mafundisho hayo:

  •   Ni jambo la kawaida kuhuzunika mpendwa wetu anapokufa. Wanafunzi wa Yesu waliomboleza walipofiwa na wapendwa wao. (Yohana 11:33-35, 38; Matendo 8:2; 9:39) Hivyo, hatuoni mazishi kuwa pindi ya sherehe. (Mhubiri 3:1, 4; 7:1-4) Badala yake, tunaiona kuwa pindi ya kuwafariji waliofiwa.​—Waroma 12:15.

  •   Wafu hawajui lolote. Hata iwe tumetoka kabila gani au tuna malezi gani, tunaepuka mila au desturi zinazotegemea imani zisizo za kimaandiko kwamba wafu wanaendelea kuishi na wanaweza kuwaathiri walio hai. (Mhubiri 9:5, 6, 10) Desturi hizo zinatia ndani kukesha, sherehe za mazishi zenye gharama kubwa, sherehe za kila mwaka za kukumbuka siku ya mazishi, kutoa dhabihu kwa ajili ya wafu, kuzungumza na kuomba wafu watusaidie, na desturi za kuwatakasa wajane. Tunaepuka mila na desturi hizo kwa kuwa tunatii amri hii ya Biblia: ‘Jitengeni, na mwache kugusa kitu kilicho najisi.’​—2 Wakorintho 6:17.

  •   Kuna tumaini kwa wafu. Biblia inafundisha kwamba kutakuwa na ufufuo na kutakuwa na wakati ambapo kifo hakitakuwapo tena. (Matendo 24:15; Ufunuo 21:4) Tumaini hilo linatusaidia kuepuka desturi za kuomboleza kupita kiasi, kama tu lilivyowasaidia Wakristo wa mapema.​—1 Wathesalonike 4:13.

  •   Biblia inatushauri tuwe na kiasi. (Methali 11:2) Hatuamini kwamba mazishi yanapaswa kutumiwa ‘kuonyesha’ hali yetu ya kiuchumi au jinsi tunavyoheshimika katika jamii. (1 Yohana 2:16) Hatupangi mazishi yenye madoido mengi yaliyokusudiwa tu kuwatumbuiza watu au kununua majeneza ya gharama kubwa sana au mavazi maalamu ili tu kujionyesha mbele za watu.

  •   Hatujaribu kuwalazimisha wengine wafuate maoni yetu kuhusu mazishi. Tunafuata kanuni hii: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:12) Hata hivyo, tukipewa nafasi, tunawaeleza wengine imani yetu “kwa tabia-pole na heshima kubwa.”​—1 Petro 3:15.

Mashahidi hufanyaje mazishi yao?

 Mahali: Familia ikipanga kuwe na hotuba ya mazishi, inaweza kutolewa mahali popote ambapo familia hiyo itachagua, kama vile kwenye Jumba la Ufalme, nyumba ya mazishi, nyumbani kwa mtu, nyumba ya kuchomea maiti, au kwenye eneo la kaburi.

 Hotuba: Hotuba hutolewa kuwafariji waliofiwa kwa kueleza mambo ambayo Biblia inasema kuhusu kifo na tumaini la ufufuo. (Yohana 11:25; Waroma 5:12; 2 Petro 3:13) Hotuba ya mazishi inaweza kutaja sifa nzuri za mtu aliyekufa, na labda kukazia mambo yenye kutia moyo tunayojifunza kutokana na mfano wa uaminifu wa mtu huyo.—2 Samweli 1:17-27.

 Wimbo unaotegemea Maandiko unaweza kuimbwa. (Wakolosai 3:16) Programu yote hufungwa kwa sala yenye kufariji.​—Wafilipi 4:6, 7.

 Malipo au sadaka: Hatudai malipo yoyote kwa ajili ya huduma za kidini tunazotoa, kutia ndani mazishi, wala hatukusanyi sadaka katika mikutano yetu.​—Mathayo 10:8.

 Wahudhuriaji: Watu ambao si Mashahidi wanakaribishwa kuhudhuria programu ya mazishi inayofanywa kwenye Jumba la Ufalme. Kama tu mikutano yetu mingine, watu wote wanaweza kuhudhuria programu hiyo.

Je, Mashahidi huhudhuria mazishi yanayoendeshwa na dini nyingine?

 Kila Shahidi hujiamulia kwa kutegemea dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia. (1 Timotheo 1:19) Hata hivyo, hatushiriki katika desturi za kidini zinazopingana na Biblia.​—2 Wakorintho 6:14-17.