Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUSITAWISHA MAZOEA MAZURI

1 Ona Mambo Kihalisi

1 Ona Mambo Kihalisi

Si rahisi kubadili mara moja kila kitu ambacho umezoea kufanya maishani. Huenda ukajiambia hivi, ‘Juma hili nitaacha kuvuta sigara, kutukana, kuchelewa kulala, nitaanza kufanya mazoezi, kula vyakula vyenye lishe, na kuwapigia simu bibi (nyanya) na babu.’ Hata hivyo, haiwezekani kufanya mambo hayo yote kwa wakati mmoja.

KANUNI YA BIBLIA: “Wenye kiasi wana hekima.”Methali 11:2.

Mtu mwenye kiasi huona mambo kihalisi. Anatambua kwamba muda, nguvu na mali zake zina mipaka. Hivyo, badala ya kujaribu kubadili kila kitu mara moja, atajitahidi kufanya maendeleo hatua kwa hatua.

Haiwezekani kufanya mambo hayo yote kwa wakati mmoja!

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Jitahidi kufanyia kazi zoea moja baada ya lingine. Hatua zifuatazo zinaweza kukusaidia:

  1. Andika ‘orodha’ mbili, moja kuhusu mazoea mazuri ambayo ungependa kusitawisha na nyingine mazoea mabaya ambayo unataka kuacha. Andika mambo mengi katika kila orodha.

  2. Panga mambo ambayo umeorodhesha ukitanguliza yaliyo muhimu zaidi.

  3. Chagua jambo moja au mawili katika kila orodha na kuyafanyia kazi. Kisha chagua jambo moja au mawili yanayofuata katika kila orodha.

Ili ufaulu haraka, hakikisha kwamba mazoea mazuri yanachukua nafasi ya mazoea mabaya. Kwa mfano, ikiwa orodha yako ya mambo mabaya inatia ndani kutazama televisheni kwa muda mrefu na ile ya mambo mazuri inatia ndani kuwasiliana na wapendwa wako, huenda ukaamua: ‘Kuwasiliana na rafiki au mshiriki wa familia badala ya kutazama televisheni mara tu unapofika nyumbani kutoka kazini.’