Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Urembo

Urembo

Kuwa na usawaziko kuhusu urembo kunaweza kusaidia kuona tofauti kati ya kuwa na furaha na kuwa na huzuni.

Kwa nini tunapenda urembo?

Kwa njia fulani isiyoeleweka, ubongo wa mwanadamu unatambua urembo. Biblia haielezi jinsi jambo hilo linavyotukia, lakini inafunua sababu inayotufanya tuvutiwe na vitu vizuri, yaani, tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. (Mwanzo 1:27; Mhubiri 3:11) Mungu ameumba mwili wetu kwa njia ya pekee, nao unafanya kazi kwa njia ya kustaajabisha sana. Ndiyo sababu mwandishi wa kale wa nyimbo alisema hivi: “Nitakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa njia ya ajabu yenye kuogopesha.”—Zaburi 139:14.

Leo, mtazamo wa watu kuhusu urembo umebadilika sana na mwelekeo huo unatokana na ushawishi wa wafanyabiashara wa nguo za kisasa na vyombo vya habari. Kulingana na kitabu Body Image, uchunguzi mwingi uliofanywa katika nchi za Magharibi unaonyesha kuwa utamaduni wa nchi hizo “unafunua kwamba jambo pekee linalotambulisha jinsi mtu alivyo ni mwonekano wake.” Hata hivyo, mtazamo huo unafanya watu wasikazie jambo fulani la muhimu sana, yaani, jinsi moyo wao ulivyo.—1 Samweli 16:7.

Utamaduni mwingi unakazia maoni yasiyofaa kuhusu jinsi mtu anavyoonekana na mahusiano ya ngono

Kukazia uangalifu kupita kiasi jinsi mtu anavyoonekana, hasa wanawake, kumefanya wajipambe katika njia ambayo inaamsha tamaa ya ngono. Ripoti ya mwaka 2007 ya American Psychological Association (APA) inasema hivi; “Karibu vyombo vyote vya habari vinatoa uthibitisho ulio wazi wa kutumiwa kwa wanawake kuamsha tamaa ya ngono.” Biblia inatuhimiza tuepuke mwenendo huo, na jambo hilo lina faida kwetu.—Wakolosai 3:5, 6.

“Kujipamba kwenu . . . , kuwe yule mtu wa siri wa moyoni katika vazi lisiloharibika la roho ya utulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kubwa machoni pa Mungu.1 Petro 3:3, 4.

Kwa nini inafaa tuwe na usawaziko?

Inapohusu urembo, baadhi ya watu husema hivi: “Kama wewe ni mrembo, onyesha urembo wako!” Ripoti ya APA inaeleza kwamba katika maeneo ambayo watu wanakubaliana na wazo hilo, wasichana ambao wamefikia umri wa kubalehe na hata ambao bado hawajafikia umri huo, wanajifunza kujipamba kwa njia inayofanya “mwonekano wao uwashawishi wengine . . . , uwavutie wengine na waonekane kuwa watu wa maana sana.” Maoni hayo yanaweza kuwa na madhara makubwa. Kwa hakika, yanaweza kutokeza tatizo kubwa la kijamii na kiafya, kulingana na APA, inaweza kufanya “watu wengi wawe na hali mbaya za kihisia.” Hali hizo zinatia ndani mahangaiko na “hata kujichukia . . . , matatizo ya kula, kujiona hawafai, na kushuka moyo.”

“Ondoa masumbuko moyoni mwako, nawe uondolee mbali msiba kutoka katika mwili wako; kwa maana ujana na upeo wa maisha ni ubatili.”Mhubiri 11:10.

Ni mtazamo gani unaoonyesha utimamu wa akili?

Biblia inahusianisha “utimamu wa akili,” au busara, na sifa ya kiasi. (1 Timotheo 2:9) Fikiria jambo hili: Mtu mwenye kiasi anajiheshimu, anajali jinsi anavyoonekana na hata ana maoni yanayofaa na yaliyosawazika kujihusu. Pia anajali hisia za wengine, hivyo anaheshimiwa sana na zaidi ya yote ana kibali cha Mungu. (Mika 6:8) Isitoshe, inaelekea kwamba atapata marafiki wa kweli na atamvutia mtu anayefaa kuwa mwenzi wake, yaani, mtu ambaye anapendezwa si na urembo tu bali na muungano wa ndoa wa kudumu na wenye furaha.

Tunapata sababu nyingi nzuri za kufuata himizo la Biblia kuhusu kukazia fikira utu wetu yaani, “mtu wa siri wa moyoni.” (1 Petro 3:3, 4) Baada ya muda urembo unaweza kupotea lakini utu mzuri haubadiliki. Bila shaka kadiri muda unavyosonga ndivyo utu huo mzuri unavyoboreka! Andiko la Methali 16:31 linasema hivi: “Kichwa chenye mvi ni taji la uzuri kinapopatikana katika njia ya uadilifu.” Hivyo, watu wanaotii ushauri bora wa Biblia, iwe ni vijana au wazee, wataweza kutambua siri ya kupata urembo unaodumu pamoja na heshima na kuridhika.

“Uvutio unaweza kudanganya, nayo sura yenye kupendeza inaweza kuwa ubatili; lakini mwanamke anayemwogopa Yehova ndiye anayejiletea sifa.”Methali 31:30.