Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Huuliza

Ninaweza Kuboreshaje Sala Zangu?

Ninaweza Kuboreshaje Sala Zangu?

“Unapopatwa na mkazo mwingi shuleni, kazini, au kutoka kwa marafiki na washiriki wa familia, nyakati nyingine unamsahau mtu muhimu zaidi, yaani, Mungu.”—Faviola, 15, Marekani.

“SALINI bila kuacha.” (1 Wathesalonike 5:17) “Dumuni katika sala.” (Waroma 12:12) “Maombi yenu na yajulishwe Mungu.” (Wafilipi 4:6) Ikiwa wewe ni Mkristo, huenda unafahamu maandiko hayo vizuri. Pia huenda unatambua kwamba sala ndiyo mawasiliano ya ajabu zaidi. Hebu fikiria hilo, eti unaweza kuzungumza na Mungu Mweza-Yote wakati wowote iwe mchana au usiku! Na Biblia inasema: “Yeye hutusikia.” *1 Yohana 5:14.

Hata hivyo, kama kijana aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, huenda ikawa vigumu kwako kusali. Hivyo, unaweza kufanya nini? Makala hii itakusaidia (1) kutambua vizuizi, (2) kujiwekea mradi kuhusu sala, na (3) kufungua “mlango” huo ili uufikie mradi wako.

Kwanza tambua vizuizi. Ni mambo gani yanayohusu sala yanayokutatanisha?

Hatua nyingine ni kujiwekea mradi. Tia alama kwenye mradi ambao ungetaka kuufikia, au andika mradi wako kando ya mstari ulioandikwa “Mradi mwingine.”

  • Ningependa kusali mara nyingi zaidi.

  • Ningependa kusali kuhusu mambo mengi zaidi.

  • Ningependa kutoa sala zenye hisia zaidi.

  • Mradi mwingine ․․․․․

Kuufungua “Mlango”

Sala ni kama mlango unaoweza kufungua wakati wowote. Hata hivyo, vijana wengi wanaweza kusema kwamba hawaufungui mlango huo mara nyingi kama wanavyopaswa. Ikiwa ni hivyo, usife moyo! Tayari umetambua tatizo na ukajiwekea mradi. Sasa unahitaji tu ufunguo wa kuufungua mlango huo. Fikiria baadhi ya vizuizi ambavyo huenda ukakabili na mapendekezo ya jinsi unavyoweza kuvishinda.

Mlango Uliofungwa: KUPUUZA.

“Kwa sababu ya shughuli nyingi, wakati mwingine, mimi hupuuza sala.”—Preeti, 20, Uingereza.

Ufunguo: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.”—Waefeso 5:15, 16.

Pendekezo: Amua mapema wakati unaofaa kwa ajili ya sala kila siku. Hata unaweza kuandika kikumbusho hicho, kama unavyofanya na vikumbusho vingine. “Nisipoweka wakati hususa wa kusali, mimi hujishughulisha na mambo mengine,” anasema Yoshiko mwenye umri wa miaka 18 anayeishi Japani.

Mlango Uliofungwa: KUKENGEUSHWA.

“Ninapokengeushwa, sikazii fikira kile ninachosema.”—Pamela, 17, Mexico.

Ufunguo: “Kinywa kinasema kutokana na mambo yaliyojaa katika moyo.”—Mathayo 12:34.

Pendekezo: Ikiwa akili yako hutangatanga unaposali, jaribu kutoa sala fupi hadi utakapoweza kukaza fikira kwa muda mrefu zaidi. Pendekezo lingine: Sali kuhusu mambo yanayokugusa moyo. “Nilipoanza kubalehe,” anasema Marina mwenye umri wa miaka 14 anayeishi nchini Urusi, “nilianza kufikiria kwa uzito kuhusu wazo la kwamba sala ni kuzungumza na Mungu. Jambo hilo lilinichochea kumweleza yaliyo moyoni mwangu.”

Mlango Uliofungwa: KURUDIA-RUDIA.

“Ninaposali, mimi hujipata nikisema maneno yaleyale tena na tena.”—Dupe, 17, Benin.

Ufunguo: “Hakika nitautafakari utendaji wako wote, nami nitajishughulisha mwenyewe na matendo yako.”—Zaburi 77:12.

Pendekezo: Ikiwa sala zako zinaonekana kuwa za kidesturi, kila siku andika baraka hususa ambayo umepata maishani. Kisha, umshukuru Yehova kwa ajili ya baraka hiyo. Fanya hivyo kwa juma moja na utakuwa umesali kuhusu mambo saba tofauti bila kujirudia-rudia. Fanya vivyo hivyo kuhusu matukio ya kila siku. “Ninaposali, mimi hujaribu kukazia fikira mambo ambayo yametukia siku hiyo,” anasema Bruno, mwenye umri wa miaka 21 anayeishi Brazili. Samantha, mwenye umri wa miaka 18 anayeishi Marekani hufanya vivyo hivyo. “Mimi hujaribu kukumbuka kila kitu ambacho leo kilikuwa tofauti na siku nyingine, kisha mimi husali kuhusu mambo hayo,” anasema. “Hilo hunisaidia nisirudie mambo yaleyale.” *

Mlango Uliofungwa: MASHAKA.

“Siku moja niliposali kuhusu tatizo shuleni, halikuondoka. Badala yake, matatizo mengi zaidi yalitokea. Nilijiuliza, ‘Kuna haja gani ya kuendelea kusali? Yehova hanisikilizi!’”—Minori, 15, Japani.

Ufunguo: “Pamoja na hilo jaribu [Yehova Mungu] ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Wakorintho 10:13.

Pendekezo: Jambo moja ni hakika: Yehova ni “Msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Kwa hiyo, baada ya kusali kuhusu jambo fulani, jaribu kuelewa mambo yote yanayohusika. Badala ya kungojea jibu unalotazamia, fikiria sala yako imejibiwa kwa njia gani. Kwa kuwa tayari unavumilia ukiwa Mkristo, inawezekana kwamba Yehova alijibu sala yako, si kwa kuondoa tatizo bali kwa kukupa nguvu za kulivumilia.—Wafilipi 4:13.

Mlango Uliofungwa: KUAIBIKA.

“Ninapofikiria wanafunzi wenzangu watasema nini wakiniona nikisali kabla ya kula chakula cha mchana, mimi huaibika.”—Hikaru, 17, Japani.

Ufunguo: “Kuna . . . wakati unaofaa kwa kila kitu tunachotaka kufanya.”—Mhubiri 3:1, Beck.

Pendekezo: Ingawa huenda watu wakaona ni jambo zuri kwamba unasali, si lazima ujionyeshe unaposali. Kwa mfano, mwanamume mwaminifu Nehemia alitoa sala fupi kimyakimya mbele ya Mfalme Artashasta, na hakuna rekodi inayoonyesha kuwa mfalme alijua kwamba Nehemia alikuwa akisali. (Nehemia 2:1-5) Wewe pia unaweza kusali kwa Yehova kimyakimya bila wengine kutambua.—Wafilipi 4:5.

Mlango Uliofungwa: KUHISI HUFAI.

“Yehova tayari anajua matatizo yangu. Na ikiwa yamenichosha mimi, nahisi huenda hata yeye amechoshwa nayo pia! Nyakati nyingine nahisi sifai kuzungumza naye.”—Elizabeth, 20, Ireland.

Ufunguo: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu ya Mungu, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’—1 Petro 5:7.

Pendekezo: Unapofanya funzo lako la kibinafsi, fanya utafiti na utafakari maandiko yafuatayo: Luka 12:6, 7; Yohana 6:44; Waebrania 4:16; 6:10; 2 Petro 3:9. Maandiko hayo yatakusaidia kutambua kwamba Yehova anataka kukusikiliza na si lazima uwe jitu kiroho ili akusikilize. Mtunga-zaburi Daudi ambaye alikabiliana na mahangaiko na taabu alisema kwa uhakika kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” *Zaburi 34:18.

Uhakika wa kwamba Yehova mwenyewe ndiye anayesikiliza sala zako unaonyesha kwamba anapendezwa nawe. “Yehova hajawapa malaika jukumu la kusikiliza sala zetu,” anasema Nicole mwenye umri wa miaka 17, anayeishi Italia. “Bila shaka, kwa kuwa ndiye anayesikiliza sala zetu, ni lazima anaziona kuwa muhimu.”

 

^ fu. 4 Kwa sababu Muumba hategemei mawimbi ya sauti, anaweza “kusikia” hata mambo tunayosema moyoni.—Zaburi 19:14.

^ fu. 32 Ukihisi kwamba sala zako zinazuiwa kwa sababu ya dhambi nzito uliyofanya, usikose kuzungumza na wazazi wako. Pia, ‘waite wanaume wazee wa kutaniko wakusaidie.’ (Yakobo 5:14) Wazee wanaweza kukusaidia usitawishe tena uhusiano mzuri pamoja na Mungu.

MAMBO YA KUFIKIRIA

  • Unaweza kusali kuhusu mambo gani yaliyo muhimu kwa Yehova?

  • Ni mambo gani yanayohusu watu wengine unayoweza kumweleza Yehova?